Logo
Chapisha ukurasa huu

بسم الله الرحمن الرحيم

Habari na Maoni 

Wanawake Hawawezi Kuheshimiwa Chini ya Nidhamu ya Kijambazi ya Kidemokrasia

Habari:

Vyombo vya habari nchini Kenya vimeangazia habari kuhusu madhila wanayo fanyiwa wanawake (kina mama) katika Hospitali ya Kitaifa ya Kenyatta (KNH) waliokwenda kutafuta huduma za uzazi katika taasisi hiyo kwamba wanadhulumiwa, kubakwa na kufanyiwa vitendo vyengine visivyo semeka na wahudumu wa hospitali hiyo.

Maoni:

Mfumo batili wa kirasilimali na itikadi yake ya kisekula humtazama mwanamke kama chombo cha ngono. Hivyo basi, thamani na heshima yao hutegemea uwezo wao katika ngono. Kwa mtazamo huo muovu wanawake wanatarajiwa kuyakabili maisha na changamoto nyingi. Kuongeza chumvi kwenye kidonda; majambazi wa kirasilimali wameeneza hadithi batili kuhusu utetezi wa wanawake ili kupigia debe maslahi ya wanawake. Hiyo imepelekea kuibuka kwa wale wanaoitwa watetezi wa wanawake wanaodai kuwa sauti ya wanawake na kulingania kuhusishwa na kutambuliwa kwa wanawake katika sekta ambazo aidha zimetawaliwa na wanaume au kwa lengo tu la kupigana kumbo na wanaume kwa kile kinachoitwa usawa wa kijinsia.

Mvutano wa kupigania kutambuliwa kwa wanawake imepelekea mgongano hatari baina ya mwanamume na mwanamke kwa kuwa nidhamu ya kijamii yenyewe, ambayo ilipaswa kudhibiti mahusiano baina ya mwanamume na mwanamke, yenyewe imefeli kwa kuwa imechipuza kutokamana na akili finyo ya mwanadamu. Hivyo basi, imepelekea kuachwa wazi kwa mujtamaa na kutukuzwa kwa uhuru kama inavyo jitokeza katika nidhamu ya kijambazi ya kidemokrasia hususan uhuru wa kibinafsi. Uhuru wa kibinafsi umetoa mwanya kwa wanadamu kutenda chochote wapendacho na mahali popote kwa msingi wa hawaa na matamanio yao. Serikali za kisekula zinang'ang'ana kila uchao kudhamini kupatikana kwa uhuru hizi na hususan uhuru wa kibinafsi, ambao ndio uti wa mgongo wa mujtamaa huu huru wa kisekula.  

Ghasia na utovu wa usalama kwa wanawake daima zimekuwa kiwango cha juu na zinaendelea kuongezeka kila mujtamaa unapozidi kuachwa wazi. Hii imetupelekea kushuhudia matukio mabaya kwa mfano:

1. Watoaji huduma za afya kutekeleza vitendo vya kinyama kwa wagonjwa wao wa kike au wanaotafuta huduma hizo vikiwemo ubakaji chini ya uangalizi wao kama vile vinavyo ripotiwa katika kashfa ya sasa katika Hospitali ya Kitaifa ya Kenyatta (KNH). Taasisi maarufu ya afya ya serikali inayo tazamiwa na raia kutoa huduma bora, lakini; badala yake imegeuka kuwa sehemu yenye utovu zaidi wa usalama kwa wanawake kwenda kutafuta huduma ndani yake! Kashfa hii mpya, ambayo siyo ya kwanza kutoa sura ovu ya pango lililo jaa wabakaji, miaka iliyopita pia ilikuwemo machoni mwa watu kutokana na ubadhirifu wa mali wa mameneja wake! 

2. Vituo na wahudumu wa afya kuwalazimisha wanawake kuzaa kupitia njia ya upasuaji (CS); ili wapokee mamilioni ya pesa kama malipo kutoka kwa Shirika la Kitaifa la Bima ya Afya (NHIF). Hii imepelekea NHIF kutoa tahadhari juu ya kuongezeka kwa ghafla kwa uzazi wa kupitia upasuaji (CS) ambao pia umepelekea taasisi hiyo kulipa malipo makubwa ya kifedha kwa taasisi za afya zaidi ya kiwango chake cha bajeti. Athari za kiafya za wanawake hazitiliwi maanani; badala yake, manufaa ya kifedha/faida ndiyo yanayo chukua kipaumbele.

3. Wizara ya Afya ya Kenya kutekeleza sera ya mwanamke mmoja kwa watoto wawili, iliyo tokana na nadharia batili inayo pigiwa debe na majambazi wa kirasilimali kwa kutumia mfumo wao batitli wa kirasilimali. Kwamba tatizo la kiuchumi lenye kuwakabili wanadamu ni uhaba wa rasilimali na wingi wa watu, ilhali; ukweli ni kuwa rasilimali ziko za kutosha bali zimelimbikizwa kwa majambazi wachache wa kirasilimali wenye ubinafsi na hivyo tatizo kuu ni jinsi ya ugavi wa rasilimali hizo kunufaisha mujtamaa mzima.

Suluhisho la matatizo yanayowakumba wanawake na wanadamu kwa jumla liko katika kuung'oa mfumo batili wa kirasilimali na kuubadilisha kwa mfumo safi wa Kiislamu utokao kwa Muumba wa viumbe Anayejua zuri na baya kwao. Heshima ya wanawake imekita chini ya bendera ya Uislamu wenye kutekelezwa kama mfumo kamili wa maisha kupitia Khilafah yenye kuongozwa na Khalifah mcha Mungu mwenye kutaraji mabustani ya Pepo ya juu ya milele na na wala sio dunia hii yenye kupita na kumalizika ilojaa maovu! Ni Uislamu pekee utakao linda heshima na dori yake msingi kama mama na mke, na kuwadhamini wanawake haki na majukumu sawa kama wanaume isipokuwa yale yaliyo fafanuliwa na dalili za sheria kuwa ya wanaume pekee na wanawake pekee. Hivyo basi, mwanamke ana haki ya kufanya biashara, ukulima na uzalishaji, kushiriki katika mikataba na miamala; kumiliki aina zote za mali; kuwekeza fedha zake mwenyewe (au kupitia wengine); na kupeleka mambo yake yote ya kimaisha mwenyewe.

Imeandikwa kwa Ajili ya Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir na

Ali Nassoro Ali

Mwanachama wa Afisi ya Habari ya Hizb ut Tahrir Kenya

1. https://www.businessdailyafrica.com/analysis/editorials/Find-out-cause-of-sudden-rise-in-Caesarian-births/4259378-4273846-40ddfc/index.html

2. https://www.standardmedia.co.ke/health/article/2001265786/state-to-delay-policy-for-two-children-per-woman

Imebadilishwa mara ya mwisho mnamoJumapili, 09 Agosti 2020 07:11
Template Design © Joomla Templates | GavickPro. All rights reserved.