Logo
Chapisha ukurasa huu

بسم الله الرحمن الرحيم

Jibu la Swali
Kuruhusiwa Kuweka Akiba kwa ajili ya Haja Hakubatilishi Wajibu wa Zaka
Kwa Abass Hammamaduh

Swali:

Uwekaji akiba dhahabu kwa miaka ambapo zaka juu yake haikulipiwa, je inalipwa kila mwaka au mara moja tu maishani? Na utoaji wake ni kwa thamani? Ahsante.

Jibu:
Wa Alaikum Assalam Wa Rahmatullah Wa Barakatuh

1 – Kabla kujibu swali lako nataka kutoa angalizo kwamba kuweka akiba dhahabu na fedha na pesa pasina haja maalumu inazingatiwa kuwa ni kuhodhi hata kama lau utailipia zaka juu yake, na kuhodhi ni haramu na dalili za kuharahamishwa ni:
Mwenyezi Mungu (swt) asema:

(وَالَّذِينَ يَكْنِزُونَ الذَّهَبَ وَالْفِضَّةَ وَلَا يُنْفِقُونَهَا فِي سَبِيلِ اللَّهِ فَبَشِّرْهُمْ بِعَذَابٍ أَلِيمٍ * يَوْمَ يُحْمَى عَلَيْهَا فِي نَارِ جَهَنَّمَ فَتُكْوَى بِهَا جِبَاهُهُمْ وَجُنُوبُهُمْ وَظُهُورُهُمْ هَذَا مَا كَنَزْتُمْ لِأَنْفُسِكُمْ فَذُوقُوا مَا كُنْتُمْ تَكْنِزُونَ) “Na wanao kusanya dhahabu na fedha, wala hawazitumii katika Njia ya Mwenyezi Mungu, wabashirie khabari ya adhabu iliyo chungu * Siku zitakapo tiwa moto katika Moto wa Jahannamu, na kwazo vikachomwa vipaji vya nyuso zao na mbavu zao na migongo yao, wakaambiwa: Haya ndiyo mlio jilimbikia nafsi zenu, basi onjeni mliyo kuwa mkilimbika.” [At-Taubah: 34 – 35]

-Ahmad amesimulia kupitia simulizi sahihi ya msururu wa wasimulizi kutoka kwa Abu Umamah aliyesema kwamba:

(تُوُفِّيَ رَجُلٌ مِنْ أَهْلِ الصُّفَّةِ، فَوُجِدَ فِي مِئْزَرِهِ دِينَارٌ، فَقَالَ رَسُولُ اللَّهِ صلى الله عليه وسلم «كَيَّةٌ»، قَالَ: ثُمَّ تُوُفِّيَ آخَرُ فَوُجِدَ فِي مِئْزَرِهِ دِينَارَانِ، فَقَالَ رَسُولُ اللَّهِ صلى الله عليه وسلم: «كَيَّتَانِ») “Mwanamume kutoka kwa Ahl Al-Suffah alifariki, na dinari moja ikapatikana ndani ya shuka yake (kujifunga kiuononi), Mtume wa Mwenyezi Mungu (saw) akasema: “atachomwa,” na mwengine akafariki na akapatikana na dinari mbili, na Mtume wa Mwenyezi Mungu (saw) akasema: “atachomwa mara mbili.”

Tabari amesimulia sawa na hivyo kutoka kwa Abu Umamah Al-Bahili. Hii ikimaanisha ni haramu kuhodhi dhahabu na fedha hata kama itakuwa ni dinari mbili n ahata dinari moja kwa sharti kuwa ni kuhodhi; hiyo ni kuweka akiba pesa pasina sababu. Na Mtume (saw) alisema hayo kuhusiana na wanaume wawili hao kwa sababu walikuwa wanaishi kwa kutegemea sadaka na ilhali walikuwa na vipande vya dhahabu, yeye (saw) alisema: «Kayat» na kusema: «Kayatan» akimaanisha aya ya Mwenyezi Mungu (swt):

(يَوْمَ يُحْمَى عَلَيْهَا فِي نَارِ جَهَنَّمَ فَتُكْوَى بِهَا جِبَاهُهُمْ وَجُنُوبُهُمْ) “Siku zitakapo tiwa moto katika Moto wa Jahannamu, na kwazo vikachomwa vipaji vya nyuso zao na mbavu zao na migongo yao,” [At-Taubah: 35]

Ambayo ni kipande cha aya ya kuhodhi, kwa maana aya ya kuhodhi. Hii ni dalili ya kukata ya kuharamisha kuhodhi, ima nisab ya zaka imetimia juu yake au la, na ima mtu ameilipia zaka au la, aina zote za kuhodhi ni haramu.

Ama kuhusu kuweka akiba kwa ajili ya haja, inaruhusiwa na dalili za kuhodhi hazitekelezwi juu yake. “Tofauti baina ya kuhodhi na kuweka akiba ni kwamba kuhodhi ni kukusanya pesa pasina haja nazo, ni kuzitoa pesa katika soko. Ama kuweka akiba, ni kukusanya pesa kwa ajili ya haja; kama kuweka akiba ili kujenga nyumba, kuoa, kununua kiwanda, kufungua biashara au mengineyo.”

2 – Lau mtu ataweka akiba dhahabu pasina haja, basi itakuwa ametenda dhambi kwa sababu ni kuhodhi dhahabu ambapo ni haramu … Lakini, anatakiwa kuilipia zaka dhahabu yake aliyoiweka akiba pasina haja kwa sababu kuhodhi kuliko haramishwa hakubatilishi wajibu wa zaka. Na ni hivyo hivyo kwa kuweka akiba kwa ajili ya haja ambapo sio haramu, lakini mwenyewe lazima alipe zaka kiwango cha nisab kinapofika na mwaka ukaipitia. Hii ni kwa sababu ya kuruhusiwa kwa kuweka akiba kwa ajili ya haja hakubatilishi wajibu wa zaka.

3 – Wajibu wa zaka upo kwa msingi wa mwaka wa (Hijria), lau pesa zitafikia nisab mfano “dhahabu,” na mwaka ukaipitia, basi inastahiki kulipiwa zaka nayo ni robo moja ya fungu la kumi au asilimia 2.5 yake. Lau mtu atalipia zaka pesa zake baada ya mwaka, itakuwa ametimiza wajibu. Lakini lau atachelewesha kulipa zake mwaka huo, inabakia wajibu kwake kuitekeleza mwaka huo. Ulipaji wa mwaka mmoja wa Hijria haizingatiwi kuwa umelipia mwaka mwingine wa Hijria, kwa sababu zaka kama ilivyotajwa hapo juu ni wajibu wa kila mwaka na kwamba kila mwaka unaanza upya kwa sharti kwamba sababu zake na masharti yake yanapatikana.

Kwa mfano mtu ameweka akiba dhahabu kwa miaka mitano ya Hijria na dhahabu ikafikia kiwango cha nisab mwanzoni mwa uwekaji akiba. Lazima alipe zaka ya miaka mitano mwishoni mwa mwaka watano lau atakuwa hakuilipia zaka dhahabu yake hapo awali. Kwa sababu kila mwaka wa Hijria ndani ya hiyo miaka mitano ni wajibu ulioshingoni mwake na lazima alipe.

Lazima alipe zaka mara tano (miaka 5) kwa kiwango cha asilimia 2.5 ya dhahabu aliyoweka akiba … Nukta muhimu ni kwamba sio wajibu kwake kulipa zaka juu ya kiwango ambacho alikilipia zaka mwaka wa kwanza kwa maana ile asilimia 2.5 bali anatakiwa kulipa zaka juu ya ile asilimia 97.5 iliyobakia kutoka kwa mwaka wa kwanza, kwa hiyo mwaka wa pili atalipa asilimia 2.5 ya kiwango kilichobakia. Na itakuwa hivyo kwa miaka inayofuatia, inazingatiwa kwamba kuna kupunguwa kwa pesa kwa mwenye kulipa zaka baada ya kulipa zaka ndani ya miaka ya awali.

4- Ama kuhusu kulipa zaka kwa kuzingatia thamani ya utajiri kuliko usawa wa mali hilo linaruhusiwa, kwa hiyo badala ya kutoa dhahabu kwa dhahabu, anaweza kutoa thamani ya dhahabu kwa kutumia noti za benki, fedha au mfano wake…

Katika kitabu cha “Mali ya Dola ya Khilafah” ukurasa 140 (Kiengereza) kinasema yafuatayo katika milango ya mapato ya Hazina:

(Pia inapatikana katika Sunnah ya Mtume wa Mwenyezi Mungu na maswahaba zake walikuwa wakiwajibisha haki juu ya pesa kisha kuibadilisha kuwa kitu chengine chepesi kwa mtoaji ili kutoa kuliko asili ya pesa. Katika hili ni barua ya Mtume kwa Muadh huko Yemen juu ya Jizya: “Kwa kila mtu aliye mzima atoe Dinari au kilicho sawa na hiyo dinari moja katika nguo (Mu’afir).” Kwa hiyo Mtume alichukua kitu chengine kuliko kitu chenyewe asili kwa maana alichukua nguo badala ya dhahabu. Na sawia na hivyo aliwaandikia watu wa Najran: “Juu yao ni maguo elfu mbili au kilichokuwa sawa wakia ya dhahabu na fedha.” Umar (ra) alikuwa akichukua ngamia kama Jizya badala ya dhahabu na fedha, naye Ali alikuwa akichukua sindano, kamba na sindano kubwa kama Jizya badala ya dhahabu na fedha.) Mwisho wa nukuu.
Katika kitabu cha “Mali ya Dola ya Khilafah” ukurasa 147 (Kiengereza) kinasema yafuatayo katika milango ya mapato ya Hazina:

(Zaka juu ya dhahabu inalipwa kwa dhahabu, au sarafu wakilishi na sarafu yenye kutegemewa). Zaka juu ya fedha inalipwa kwa fedha, au sarafu wakilishi na sarafu yenye kutegemewa. Vile vile zaka juu ya dhahabu inaweza ikalipwa kwa fedha na sarafu ya lazima ilhali Zaka juu ya fedha inaweza kulipwa kwa dhahabu na sarafu ya lazima, kwa kuwa zote ni sarafu na bei. Kwa hiyo baadhi yao zinaweza kuchukua sehemu ya nyingine na baadhi yao zinaweza kulipwa katika sehemu ya nyingine kwa kuwa lengo linathibitishwa katika hili. Imetajwa katika mlango wa Zaka juu ya mazao na matunda dalili za kuchukua thamani kama mbadala kwa mali ambayo inawajibu wa Zaka.) Mwisho wa nukuu.

Ni wazi kutoka hapo juu kwamba inaruhusiwa kulipa zaka juu ya dhahabu na fedha kwa kutumia noti za benki zinazotumika, kwa mujibu wa bei ya soko kwa dhahabu na fedha wakati wa kulipa zaka.
Nimatumaini yangu kwamba jibu hili linatosheleza.

Ndugu yenu,
Ata Bin Khalil Abu Al-Rashtah

01 Ramadhani 1440 H
Jumatatu, 06/05/2019 M

Imebadilishwa mara ya mwisho mnamoAlhamisi, 02 Aprili 2020 20:35
Template Design © Joomla Templates | GavickPro. All rights reserved.