Jumanne, 09 Ramadan 1445 | 2024/03/19
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

بسم الله الرحمن الرحيم

 Jibu la Swali

Mzozo Kati ya Uturuki na Ugiriki katika Eneo la Mashariki mwa Mediterranea
(Imetafsiriwa)

Swali:

Mnamo tarehe 8/10/2020, Waziri wa Mambo ya nje wa Uturuki Mevlut Cavusoglu alifichua kwamba alikuwa amefikia makubaliano mapya kati ya nchi yake na Ugiriki. Waziri huyu alisema katika taarifa zake, kulingana na wavuti wa Turkey Now: ​​[“Kwamba alikubaliana na mwenzake wa Uigiriki Nikos Dendias kufanya mazungumzo ya utafiti kati ya nchi hizo mbili. Hii ilikuja katika taarifa kufuatia mkutano wake na Dendias juu ya kadhia za pembeni za ushiriki wake katika Kikao cha Usalama cha Kiulimwenguni cha Bratislava nchini Slovakia. Alielezea kuwa Uturuki itakuwa mwenyeji wa mazungumzo hayo, huku Ugiriki ikiwasilisha mapendekezo ya makataa yake." (Wavuti wa Turkey Now, 8/10/2020)]. Hapo awali, Uturuki ilikuwa imezorotesha sana uhusiano wake na Ugiriki na kupambana nayo kupitia kutuma meli za utafiti za Uturuki pamoja na manuari za kusindikiza ... Je! Uhalisia wa mgogoro huu kati ya Uturuki na Ugiriki ni upi? Je! Ni upi uhalisia wa misimamo ya kimataifa juu ya mgogoro huu? Je! Amerika iko nyuma yake au Uturuki inafanya kazi peke yake? Na ni yapi maelezo ya taharuki kubwa iliyokuwa mwanzoni na kumalizika kwa makubaliano ya mazungumzo hayo? Asante.

Jibu:

Mgogoro wa Uturuki na Ugiriki lazima uangaliwe kwa upande wa sababu zake na athari za ndani nchini Uturuki, na vile vile vipimo vyake vya kiuchumi na kimataifa ... ili kujua, mambo yafuatayo yanapaswa kuhakikiwa, kuanzia kwa Mkataba wa Lausanne katika robo ya kwanza ya karne iliyopita:

Kwanza: Mkataba wa Lausanne:

1- Uturuki ina pwani ndefu zaidi kwenye Bahari ya Aegean na Mediterania ya Mashariki, lakini Mkataba wa Lausanne uliotiwa sainiwa tarehe 24/7/1923 na wawakilishi wa mhalifu wa zama hizo, Mustafa Kemal, kwa niaba ya serikali ya Bunge Kuu la Kitaifa la Uturuki jijini Ankara lililojitenga kutoka kwa Khilafah jijini Istanbul, ndio ulioifunga Uturuki na Bahari ya Aegean, ikiwa vigumu kuondoka kutoka katika pwani zake, kwani visiwa vilivyo ndani ya Bahari ya Aegean ima vyote au vingi vimekuwa mali ya Ugiriki! Hapo ndipo Mustafa Kemal alipowatuma wawakilishi wake hadi Lausanne nchini Uswizi, akipendekeza kwa Washirika kwamba serikali yake jijini Ankara, iliyokuwa imejitenga na Khilafah jijini Istanbul, inaweza kutia saini nao, washirika, mkataba ambao waliutaka! Kwa hivyo, Mkataba wa Lausanne ulitiwa saini na Uswisi kati ya wawakilishi wa Uingereza, Ufaransa na nchi zingine na wawakilishi wa Mustafa Kemal, walioongozwa na Ismet Inönü kwa niaba ya serikali ya Bunge Kuu la Kitaifa jijini Ankara ...

2- Masuala ya kushtua yaliyofafanuliwa kwa kina katika mkataba huo yaliafikiwa na Mustafa Kemal na wawakilishi wake, pamoja na kile kilichokuja katika Kifungu cha 12, ambapo visiwa vyote au vingi vya Aegean vilikuwa mali ya Ugiriki, ingawa baadhi yake viko umbali wa kilomita 600 kutoka kwa bara ya Ugiriki, huku vikikutana na bara la Uturuki kwa umbali wa kilomita mbili wakati mwingine, kama ilivyo hali ya kisiwa cha Meis, ambacho ni cha Ugiriki ambacho wanakiita Kastellorizo, mbali na mji wa Kaş katika jimbo la Antalya. Ni mkataba huu ndio unaoipa Ugiriki (uhalali) kuitaka Uturuki isichimbe pwani za Uturuki kwa sababu ni haki ya kipekee ya Ugiriki chini ya Mkataba wa Lausanne! Na Ibara ya 15 inasema kwamba Uturuki inapaswa kuachilia, kwa manufaa ya Italia, haki zote na umiliki juu ya visiwa vifuatavyo: Stampalia (Astypalaia), Rhodes (Rhodes), Halki (Kharke) ... nk, na pia Kifungu cha 20: kwamba Uturuki inatambua kuunganishwa kwa Cyprus na serikali ya Uingereza kulikotangazwa na Uingereza mnamo Novemba 1914. Pia, yale yalitajwa katika kifungu cha 23 ambacho kinasema kuwa Pande (Kuu) za Mkataba zimekubali kutambua na kutangaza kanuni ya uhuru wa kupita na kusafiri, kwa bahari na anga, wakati wa amani na wakati wa vita, huko Dardanelles, Bahari ya Marmara na Bosporus! Kwa hivyo, Uturuki imepoteza, huku ikiwa na pwani ndefu zaidi mashariki mwa Mediterania, uhuru wa kusafiri ndani ya visiwa hivi katika bahari hizi, ambapo Erdogan anaikumbuka leo kama "Nchi yake ya Samawati iliyoibiwa"!

Analalamika kuhusiana nayo wakati picha ya mhalifu wa zama hizo Mustafa Kemal inaning'inia juu ya kichwa chake, ambaye ndiye aliyeidhinisha makubaliano haya huko Lausanne. Licha ya yote haya na kwamba hasubutu kumtaja Mustafa kwa neno la matusi!! Badala yake, yeye hucheza na hamasa za watu wa Uturuki kupitia kuzipa meli za utafiti majina ya viongozi wakuu wa Kiuthmani, Muhammad Al-Fatih na al-Qanuni, licha ya kuwa mbali kwake na viongozi hawa wakuu katika sera zake zote! Anatangaza, "Kila mtu anatambua kwamba Uturuki ina uwezo wa kisiasa, kiuchumi na kijeshi" kuzipasua nyaraka na ramani zisizo za haki zilizotokana na uovu na ugomvi dhidi yake." Aliongeza, "kwamba nchi yake iko tayari kufafanua jambo hili kwa kupitia uzoefu mchungu, iwe kwenye meza ya mazungumzo au katika uwanja." Al Jazeera, 5/9/2020), lakini anakomea hapa na kudhani kuwa amefanya vyema! Labda watu wa Uturuki waliona kwamba Ugiriki, ambayo haina jeshi lenye ushawishi vilivyo, ilituma wanajeshi wake kwenye kisiwa cha Meis, wakibainisha kuwa Mkataba wa Lausanne unaelezea kuondolewa kwa nguvu za kijeshi huko, na bado hawakuikabili Ugiriki kwa nguvu inayostahili!

3- Ingawa Mkataba huu ulikuwa mkataba wa hila ambao Mustafa Kemal aliukamilisha na washirika, lakini aliukamilisha kwa jina la serikali ya Bunge Kuu la Kitaifa jijini Ankara. Uingereza haikuridhika na hilo, lakini ilimtaka amalize masharti aliyowekewa, haswa kuivunja Khilafah kabisa na kuasisiwa kwa dola ya kisekula. Mustafa Kemal alitii, hii ilifanyika asubuhi ya 3 Machi 1924, wakati Khilafah ilipotangazwa kuvunjwa na dini kutengwa na serikali. Usiku huo huo, Mustafa Kemal alituma agizo kwa gavana wa Istanbul akisema kwamba Khalifa Abdul-Majid aondoke Uturuki kabla ya alfajiri ya siku iliyofuata, kwa hivyo akaenda na kikosi cha polisi na jeshi hadi katika kasri la Khalifa katikati ya usiku, na huko alimlazimisha Khalifa kupanda gari lililombeba kuvuka mpaka kuelekea Uswizi. Baada ya siku mbili, Mustafa Kemal alikusanya wana wa kiume na wa kike wa kifalme na kuwafurusha nje ya nchi. Nafasi zote za kidini zilifutiliwa mbali, wakfu za Waislamu zikawa mali ya dola, shule za kidini zilibadilishwa kuwa shule za serikali, na zikawa chini ya usimamizi wa Wizara ya Elimu.

Kwa hili, Mustafa Kemal alitimiza masharti manne ambayo Curzon aliyataka kutoka kwake, ambayo ni: kuivunja Khilafah kabisa, kufukuzwa kwa khalifa nje ya mipaka, kunyang'anywa fedha zake, na tangazo la usekula wa dola. Kwa hivyo, Mkataba wa Lausanne ambao ulikamilishwa kabla ya kuvunjwa kwa Khilafah ulithibitishwa na kutekelezwa baada ya kuvunjwa kwa Khilafah! Kwa hivyo, Mkataba wa Lausanne ulimalizika kwa kuvunjwa kwa dola ya Khilafah; dola ziliutambua uhuru wa Uturuki, na Waingereza waliondoka Istanbul. Matokeo yake, mmoja wa wabunge wa Uingereza alimpinga Curzon katika Bunge la House of Commons kwa kutambua kwake uhuru wa Uturuki. Curzon alimjibu akisema: "Hali sasa ni kwamba Uturuki imekufa na haitafufuka tena, kwa sababu tumeangamiza nguvu yake ya kimaadili, Khilafah na Uislamu." Kwa hivyo, Waingereza waliiondoa Khilafah na Uislamu kupitia Mustafa Kemal, licha ya upinzani wa Waislamu kote ulimwenguni kwa jumla, na licha ya upinzani wa Waislamu nchini Uturuki haswa. Kwa hivyo, hukmu kwa yale yote yaliyoteremshwa na Mwenyezi Mungu (swt) iliondolewa kutoka sehemu zote za ardhi, na hukmu kwa yasiyokuwa yale yaliyoteremshwa na Mwenyezi Mungu (swt), hukmu ya kikafiri ikabakia, na hukmu ya Taghut (ukafiri) peke yake ilibakia, ambayo inawadhibiti watu wote, na inatekelezwa kote ulimwenguni!

Pili: Mkataba huu uliotiwa saini na wawakilishi wa Mustafa Kemal katika jiji la Uswizi la Lausanne, ambapo Uturuki ilizuiliwa kutokana na Bahari ya Aegean, visiwa vyake na fukwe zilipewa Ugiriki, na Uturuki ilizuiwa kuichimba! Hali hii ambayo Uturuki ilikabiliwa nayo iliendelea kwa karibu miaka mia moja, kwa hivyo ni nini kilichoihamisha Uturuki sasa? Yule anayefuatilia mwenendo wa mambo atagundua kuwa kuna sababu mbili nyuma ya mgogoro huu: Kindani kwa sababu ya hali za uchumi wa Uturuki, na kinje, kwamba Amerika inasimama nyuma yake:

1- Sababu za Ndani:

a- Uturuki ni nchi inayotumia nishati na isiyozalisha, na hivi karibuni uzalishaji wake wa mafuta umefikia mapipa elfu 53 kwa siku (Shirika la Anadolu, 25/7/2020), ambayo ni idadi ndogo sana ikilinganishwa na matumizi ya mapipa milioni moja ya mafuta kila siku (Al-Araby Al-Jadeed, 22/4/2020). Inazalisha takriban mita za ujazo milioni 475 za gesi na kuagiza zaidi ya mita za ujazo bilioni 45 (Al-Jazeera Net, 31/8/2020). Kwa hivyo, Uturuki inakabiliwa na bili kubwa ya mafuta na gesi inayoingiza, ambayo ilifikia dolari bilioni 41 mnamo 2019, chini kutoka bilioni 43 kwa mwaka 2018 kwa sababu ya bei ya chini ya nishati ulimwenguni (Jarida la Uturuki la Sabah Daily, 27/2 / 2020). Hii ni sababu ambayo inaathiri sana uchumi wa Uturuki.

b- Na kwa sababu Uturuki iko kati ya nchi zinazozalisha mafuta katika eneo la Kiarabu, Iran na Azerbaijan, na kati ya nchi zinazotumia mafuta, ambazo ni nchi za Ulaya, imejenga mikakati yake mingi ya nishati kwa msingi wa kuwa "nchi ya ukanda", na bandari ya Ceyhan ya Uturuki imekuwa bandari ya kusafirisha mafuta ya Azerbaijan na mtandao wa mabomba umeanzishwa ndani yake na kupitia bandari hiyo. Sio ya mwisho ambayo ni bomba kubwa la Uturuki kusafirisha gesi ya Urusi kwenda magharibi mwa Uturuki na kutoka huko kwenda Ulaya, ambalo lilizinduliwa mnamo 8/1/2020. Licha ya ada ambayo Uturuki inakusanya kama ukanda wa nishati, bili ya mafuta na gesi bado ingali ghali sana kwa uchumi wake.

c- Tangu mwaka 2009, umbile la Kiyahudi na kampuni za kimataifa zimekuwa zikitoa matangazo mapya juu ya ugunduzi wa kiasi kikubwa cha gesi mashariki mwa Mediterania. Kwenye uwanja wa Tamar kilomita 80 magharibi mwa Haifa, futi za ujazo trilioni 9 za gesi inayoweza kutolewa iligunduliwa, kisha, miezi kadhaa baadaye, uwanja wa Dalit uligunduliwa magharibi mwa Palestina inayokaliwa kwa kati ilifikia futi za ujazo bilioni 500. Katika 2010 idadi iliyozidi mawazo iligunduliwa katika uwanja wa Jonathan magharibi mwa Palestina na futi za ujazo trilioni 16, Jarida la Sera ya Mambo ya nje la Amerika lilisema wakati huo, "Ni ugunduzi mkubwa zaidi wa gesi asilia ulimwenguni katika muongo mmoja."

d- Kwa hivyo, Uturuki imechukua hatua ya kuchukua na kununua meli ya kisasa na kubwa ya utafiti kutoka Korea Kusini, meli ya Al-Fatih, ambayo ilisafiri kwa mara ya kwanza mnamo 2011 na utafutaji wa mafuta na gesi ulianza. Halafu ulifuata mfululizo wa migogoro kati yake na Cyprus na Ugiriki kwa madai kwamba Uturuki ilikuwa ikichimba visima katika maeneo ya baharini ambayo ni milki ya Cyprus ya kipekee, na kisingizio cha Uturuki kilikuwa Wacyprus wa Kituruki na haki zao. Lakini, katika miezi ya hivi karibuni, Uturuki imeongeza kasi ya kazi ya utafiti baada ya kununua chombo kingine cha utafiti (uchimbaji wa pwani) kutoka Uingereza, ili kuwa na msururu wa vifaa vizuri vya uchimbaji baharini na meli za utafiti wa kijiolojia zinaweza kutafuta na kuchunguza kwa wakati mmoja katika Bahari Nyeusi, Pwani za magharibi ya Uturuki na kusini ya Cyprus katika mashariki mwa Mediterania.

Kwa hivyo, Uturuki ilihitaji kurekebisha hali yake ya kiuchumi kwa kukagua mafuta na gesi ... Labda inapaswa pia kutajwa kuwa uchumi wa Uturuki unakabiliwa na mapigo makubwa, maumivu ambayo yalionekana katika kuanguka kwa sarafu ya Kituruki, lira, ambayo ilimfanya Rais Erdogan kuongeza kasi ya utafutaji wa gesi kwa kutaraji kwamba atapata mwanga wa matumaini kwa uchumi huu, kwamba anaweza kudumisha umaarufu wake unaopungua kwa sababu ya kuanguka kwa lira na uasi wa viongozi wa chama chake dhidi yake na uundaji wa vyama vya upinzani ambavyo vinanyonyora umaarufu wa Erdogan. Kwa hivyo kazi ya utafiti wa Uturuki ilikuwa pana katika Bahari Nyeusi na haikufungika kwa maeneo inayozozania na Ugiriki katika Mediterania.

2- Sababu za nje:

a- Amerika inaunga mkono kuzinduliwa kwa juhudi hizi za Uturuki, kutoka pande mbili: Ya kwanza ni ya ndani: kwamba mtu wake nchini Uturuki, Erdogan, atakuwa katika nafasi nzuri ikiwa ataweza kuondoa vizuizi vya kiuchumi, kuongeza umaarufu wake na kuurudisha katika viwango vya juu kama ulivyokuwa kabla ya 2014, na hii inarahisisha utekelezaji wake wa sera za Amerika, kama vile kuingilia kati kwake Libya, ambapo anaweza kutumia katika hatua zake za kikanda kwa neema ya Amerika. Na ya pili: Amerika, wakati ambapo haitaki Ulaya iwe chini ya ushawishi wa kisiasa wa gesi ya Urusi, haitaki iwe huru katika suala la gesi. Ugiriki na Cyprus ni wanachama katika Muungano wa Ulaya na urefu wa mabomba unaanzia kutoka kwao hadi Ulaya, yote haya hayaipendezi Amerika, ndio sababu inaunga mkono tishio la uhuru wa Ulaya katika suala la gesi kupitia Uturuki. Kwa maana kwamba Rais wa Uturuki Erdogan anaitishia Ugiriki na kuchunguza kile inachokiona ni maeneo yake ya kipekee ya baharini bila makubaliano nayo kwa msaada fiche wa Amerika. Kwa hivyo, meli za jeshi la Amerika zilishiriki katika mazoezi ya kijeshi ya Kituruki. Wizara ya Ulinzi ya Uturuki ilitangaza ushiriki wa manuari ya USS Washington katika mazoezi hayo (Gazeti la Uturuki la Now, 26/8/2020),

Yote haya licha ya fedheha ya Amerika kuunga mkono nchi ndani ya muungano wake wa NATO dhidi ya nchi ya Ulaya, ambayo pia iko ndani ya NATO, na hiyo ilikuwa kwa badali ya ushiriki wa Ufaransa, ambayo pia ni kutoka nchi za NATO, katika harakati za kijeshi za Ugiriki, mienendo hiyo na baadhi ya uimarikaji wa kijeshi na sauti ya kukaidi ... yote haya yalisababisha hali ya hatari mashariki mwa Mediterania ambayo ilitishia kuzuka katika mapigano ya kijeshi kati ya nchi za NATO, ambayo ni kati ya Uturuki, ambayo inasaidiwa na Amerika kutoka nyuma ya pazia, na Ugiriki, ambayo inasaidiwa waziwazi na Ufaransa, ikiwa jambo hili halikudhibitiwa baadaye.

b- Kwa upande mwingine, ruhusa ya Amerika ya mzozo mkubwa kutokea ambayo karibu ilibadilika kuwa hatua za kijeshi kati ya nchi mbili wanachama wa muungano wa NATO ambayo inaongoza bila kutupa uzito wake mzito wa kutatua mgogoro huo inaonyesha kujishughulisha kwake na shida zake za ndani kama vile virusi vya Korona na uchaguzi ... na kwamba kwa sasa imekabidhi hatua hii upande wa Ulaya, haswa Ugiriki, kwa Erdogan kwa msaada wake kwake kwa njia ambazo huzingatia fedheha ya Amerika kwamba Uturuki na Ugiriki ni wanachama wa NATO inayoongozwa na Amerika, na kwa hivyo Amerika ilishiriki pamoja na Uturuki katika mienendo ya kijeshi kama msaada kwa hali hizi. Kwa upande mmoja, na kwa upande mwingine Pompeo alifanya ziara ya haraka huko Ugiriki, RT iliripoti "Pompeo alitoa wito kwa Uturuki kuondoa vikosi vyake kutoka Mashariki mwa Mediterania, ambapo meli ya utafiti ya Uturuki inayoungwa mkono na wahalifu wa jeshi inaendesha shughuli." (RT, 13/9/2020). Ikimaanisha kwamba Amerika, ambayo inaunga mkono Uturuki, ilijikuta mbele ya fedheha kubwa kutoka kwa washirika wake wa Ulaya, na ililazimika kumuagiza Rais Erdogan wa Uturuki kuondoa meli hiyo ya utafiti, ambapo ndilo lililofanyika, na kisha kuingia katika mazungumzo na majadiliano na Ugiriki, kwa sababu Ugiriki iliashiria sharti la mazungumzo hayo ni kuondolewa kwa meli ya kuchimba visima ya Kituruki.

Tatu: Misimamo ya Nchi Nyengine:

1- Msimamo wa Ufaransa ndio uliokuwa msimamo wenye nguvu zaidi wa Ulaya, kwani ilitangaza kutoka mwanzo kwamba imesimama na Ugiriki, na kutembea peke yake; Rais wake Macron alisema: ["Niliamua kuimarisha kwa muda uwepo wa jeshi la Ufaransa mashariki mwa Shirika la Kituruki la Anadolu, 13/8/2020)], na kisha kufanya mienendo pamoja ya majini na Ugiriki na kushiriki kwa ndege za Rafale ambazo ilizipelekwa nchini Cyprus, na kisha kufanya mienendo mingine mnamo 26/8/2020.

Iliihusisha Italy, pamoja na Ugiriki na Cyprus, ilifanya yote hata ingawa haina ushawishi katika eneo hilo! Yote hii inaonyesha kwamba inajaribu kujijengea tena ushawishi mkubwa. Kama ilivyo mienendo yake ya kijeshi pamoja na Ugiriki wakati ambapo Amerika inashiriki katika mienendo pamoja na Uturuki, hiyo inaleta changamoto fiche kwa Amerika, na kuihusisha kwake Italy nayo inaonyesha kwamba inasajili nchi za Ulaya pamoja nayo dhidi ya Uturuki, na vile vile mkutano ambao ilioufanya na baadhi ya nchi za Ulaya za Mediterrania (Italy, Malta na Uhispania pamoja na Ugiriki na Cyprus), na shinikizo lake ndani ya Muungano wa Ulaya na NATO kuchukua misimamo mikali dhidi ya Uturuki. [na Rais wa Ufaransa alisema: "Sisi kama Wazungu tunapaswa kuwa wazi na thabiti na serikali ya Rais Erdogan, ambayo leo inafanya tabia isiyokubalika ... na akaona kwamba "Uturuki sio mshirika tena katika eneo hili." (Ufaransa 24, 10/9/2020)]. Pia (Waziri wa Mambo ya nje wa Ufaransa Jean-Yves Le Drian alisema kuwa mkutano ujao wa Baraza la Ulaya umejitolea kuiadhibu Uturuki. Aliashiria kuwa Rais wa Uturuki, Recep Tayyip Erdogan, anaendelea kukola moto na Ugiriki ili kuficha hali ngumu ya kiuchumi ya nchi yake. " (The Independent Arabia, 7/9/2020).

Licha ya ujasiri wa msimamo wa Kifaransa dhidi ya Uturuki na jaribio lake la kuvunja mfupa wa rais wa Uturuki, na licha ya ukweli kwamba Rais wa Uturuki Erdogan siye "Al-Fatih" wala "Qanuni" ambao majina yao hutumiwa kuzipa majina meli zake, na kwamba hakuifundisha Ufaransa somo katika Mediterania na wala angalau hakuzamisha meli yao yoyote, kwa adhabu ya maelfu ya maili ambayo meli na ndege zilisafiri kuvunja mfupa wake katika ua wa nyumba yake. Licha ya hayo yote, sera za Ufaransa zilibaki kuwa za uchakachuaji na zilikosa kina, huku Malta ikikimbilia kuukana muungano wake na Ufaransa. Waziri wa Mambo ya nje wa Malta, Evarist Bartolo alisema wakati wa mkutano na waandishi wa habari aliofanya na mwenzake wa Uturuki Mevlut Cavusoglu [Umoja wa Ulaya unapaswa kuutazama uhusiano wake na Uturuki kwa mtazamo wa kimkakati. Bartolo aliongeza: Nadhani wakati umefika kwa Muungano wa Ulaya kuishughulikia kwa uzito Uturuki, haswa katika biashara, haki za binadamu, na vita dhidi ya ugaidi. "(Shirika la Kituruki la Anadolu, 12/9/2020)].

2- Ama Uingereza, haikutoa maoni juu ya mvutano katika Mashariki ya Mediterania, ambapo iliongeza hofu ya Ufaransa. Badala yake, tangu Brexit, Ufaransa imekuwa ikiitazama kwa wasiwasi dori ya Uingereza, na wakati mwingine inagongana nayo, kama nchini Algeria. Na ikiwa masoko makubwa ya kifedha jijini London yataipa Uingereza nafasi katika masoko ya mafuta na gesi, haswa kwa bei kutokana na ushirika wake na mafuta ghafi ya Brent na bei inayofuata ya aina zingine za mafuta, na hata gesi asilia pia, Ufaransa, inayoiona Uingereza ikiachana na Muungano wa Ulaya, inajitafutia nafasi katika sekta hii muhimu ya kimataifa. Ndio sababu iliamua kujiasisisha nchini Ugiriki, labda itaisaidia kuwa mtendaji, sio mtumiaji pekee katika maswala ya nishati.

Kwa upande mwingine, Uingereza, wakati inaangalia kile kinachoonekana kama sera ya adhabu ya Muungano wa Ulaya dhidi yake kwa sababu ya kujiondoa kwake katika Muungano wa Ulaya, inatengeza njia yake na kuchora sera yake yenyewe, na labda iliogopa kuzuka kwa ghafla kwa taharuki katika mashariki mwa Mediterania, kwa hivyo haikuchukua misimamo dhidi ya Uturuki, kwani Ugiriki haina thamani yoyote kwa Uingereza ikilinganishwa na maslahi yake ya Kituruki. Na ni shabiki kipofu pekee kama Ufaransa ndiye anayeweza kupanda wimbi la Ugiriki! Kwa kulinganisha Uingereza na Ujerumani, Ufaransa haina maono yoyote, ambayo inaisababisha kurudi mikono mitupu baada ya vitendo vikali vya kisiasa ambavyo inavifanya. Kwa haya yote, rais wa Uturuki alimshambulia vikali, akisema: “Bw. Macron, utakuwa na matatizo zaidi na mimi binafsi. ” Aliongeza: “Huna habari za kihistoria. Na wewe hujui historia ya Ufaransa, kwa hivyo usishughulike sana na Uturuki na watu wake "... (Al-Quds Al-Arabi, 12/9/2020).

3- Kwa upande wa Ujerumani, pia haikuteleza nyuma ya msimamo wa Ufaransa dhidi ya Uturuki, na ikatoa ofa ya upatanishi, wakati wengine walitafsiri kama ilicheza dori ambayo Washington ilipaswa kucheza. Iliendelea kujitenga na msimamo wa Ufaransa, kupatanisha na kutoa wito wa mazungumzo, na msimamo wake maarufu dhidi ya Uturuki ni kile Waziri wa Mambo ya nje wa Ujerumani, Heiko Maas, alichosema wakati wa ziara ya Athens ["Kuhusu utafiti wa Uturuki Mashariki mwa Meditterania, tuna msimamo wazi kabisa ... Sheria ya kimataifa lazima iheshimiwe. Kwa hivyo, maendeleo katika mahusiano ya Muungano wa Ulaya na Uturuki yatawezekana tu ikiwa Ankara itaacha uchochezi katika Mashariki mwa Mediterania… Utafiti wa Uturuki katika pwani ya Cyprus lazima ukome "(France 24 , 22/7/2020)].

4- Kwa upande wa Urusi, imejitolea kutumia uhusiano wake mzuri na Uturuki kupatanisha pande hizo mbili, lakini kama kawaida haiwezi kuchukua hatua yoyote, hata ikiwa ilitangaza mienendo ya kijeshi katika mashariki mwa Mediterania katika kujibu mienendo ya Ufaransa, na labda inataka kujikumbusha, [Urusi imepanga kuanza mazoezi ya kijeshi ya majini kwa risasi halisi katika Bahari ya Mediterania Jumanne ijayo, yenye kuendelea hadi Septemba 22, na nmengine kuanzia 17 hadi 25 Septemba, kulingana na Shirika la Bloomberg, ikinukuu Jeshi la Wanamaji la Uturuki, na msemaji wa Jeshi la Wanamaji la Urusi Igor Dygalo alisema, "Tuna uhusiano madhubuti wa kiuchumi na ulinzi na Uturuki. Lakini sera yetu ni kuzuia kuunga mkono upande wowote." Mienendo ya Urusi ilifuata mazoezi mengine ya kijeshi yaliyofanywa na Ufaransa katika eneo hilo, ambapo walipeleka ndege za kijeshi na manuari kusaidia Ugiriki na Cyprus katika mzozo huo. " (Independent Al-Arabiya, 7/9/2020)]. Hiyo ni kwamba, msimamo wa Urusi unabaki pambizoni, ukingojea ishara kutoka nyuma ya bahari, lakini inakumbusha nguvu yake.

Nne: Kwa yote yaliyotajwa hapo juu, mgogoro wa Uturuki na Ugiriki, ikiwa utarefushwa, utasababisha mpasuko mkubwa katika uhusiano wa kimataifa. Kuhusu uhusiano katika upande wa Atlantiki, nchi za Ulaya zinataka kuona nafasi yao katika ulimwengu ambao Amerika inajiondoa kutoka kwa uongozi wake kuelekea kulenga China na shida zake za ndani zinazoongezeka. Nchi hizi zinatafuta dori iliyotelekezwa na Amerika. Amerika chini ya utawala wa Trump haiachi kutishia maslahi ya Ulaya kwa kuwatumia wengine, kama dori za Urusi na Uturuki nchini Libya leo. Nchi za Ulaya zinaogopa sana kuwa mgogoro wa mashariki mwa Mediterania utasababisha kuharibu ndoto zao za chanzo salama cha gesi asilia iwapo Uturuki itadhibiti sehemu yake kubwa. Na kwa sababu Uturuki inaungwa mkono nyuma ya pazia na Washington, sera ya Ufaransa mashariki mwa Mediterania inajaribu kuzikataa dori ambazo yanatolewa Washington kwa Uturuki pamoja na Urusi.

Mzozo huu ndani ya atlantiki sio chini ya mzozo mwingine ndani ya Ulaya yenyewe. Msimamo wa Wajerumani ndio ulioizuia Ufaransa kushinikiza Ulaya iiadhibu Uturuki, ambayo ni kwamba haikufanikiwa kupata makubaliano ndani ya Muungano wa Ulaya dhidi ya Uturuki, kwa hivyo ilikwenda na kukusanya nchi za Mediterania za Ulaya! Ujerumani inafikiria mengi juu ya maslahi yake, na kwa kweli historia yake na Uturuki, ambapo Ujerumani na Dola la Uthmani zilipambana bega kwa bega dhidi ya washirika katika Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, na mahusiano ya Ujerumani yalibaki imara na Uturuki, na kuchafuliwa tu na (uchokozi) wa Rais Erdogan na mara nyingi ukisukumwa na sera za Amerika. Hii ni ikiongezewa na jamii kubwa ya Kituruki iliyo nchini Ujerumani.

Ya tano: Iwapo mgogoro huu umekwisha au la, Uturuki imetangaza ugunduzi muhimu wa gesi katika Bahari Nyeusi, ambao ni jumla ya mita za ujazo bilioni 320, na hii inaisukuma katika utafiti zaidi katika Bahari Nyeusi na Mashariki mwa Mediterania. Jitihada za Uturuki za kupunguza mzigo wake wa kiuchumi zinaendelea, na uungwaji mkono wa Amerika kwa hilo unaendelea, ili kuihangaisha na kuishinikiza Ulaya, haswa Ufaransa, ili isiende mbali kupingana na kuvuruga sera ya Amerika katika eneo hilo!

Lakini inatia uchungu sana kwamba wakati wa karne iliyopita baada ya kuanguka kwa Khilafah, dola halisi ya Uislamu na chanzo cha utukufu wa Waislamu, nchi hizi zimekuwa mkia wa mataifa, hatma zao zikihadaiwa na wakoloni makafiri kwa zana zao, watawala katika nchi za Waislamu!! Walakini, alfajiri huzaliwa baada ya giza tororo la usiku, haswa kwa kuwa Hizb ut Tahrir inafanya kazi kuziregesha kama zilivyokuwa zenye kuvikwa taji, ushindi na nuru, Mwenyezi Mungu akipenda.

]إِنْ هُوَ إِلَّا ذِكْرٌ لِلْعَالَمِينَ * وَلَتَعْلَمُنَّ نَبَأَهُ بَعْدَ حِينٍ]

“Hayakuwa haya ila ni mawaidha kwa walimwengu wote * Na bila ya shaka mtajua khabari zake baada ya muda.” [Sad: 87-88]

24 Safar Al-Khair 1442 H

11/10/2020 M

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

rudi juu

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu