Ijumaa, 10 Shawwal 1445 | 2024/04/19
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

بسم الله الرحمن الرحيم

Tutafuteni Radhi za Mwenyezi Mungu (swt) Katika Kila Jambo, Tutimize Lengo Lake Kama Mwenyezi Mungu (swt) Alivyotuamrisha

Moja ya masaibu katika Dini yetu kipindi hiki yanaanzia kwenye kufahamika vibaya kwa lengo la kila tendo tulifanyalo, pamoja na dhumuni tunalotaka kulifikia kutoka kwenye kila tendo Duniani. Ni masaibu yalioibua matatizo mengi. Baadhi wanafuata yalio kwenye Uislamu kukidhi matamanio na matashi yao tu. Baadhi wanayapamba matamanio na matashi yao kwa marejeo yasiyo wazi kwenye Uislamu. Wanaoathiriwa na fikra ya Majaaliwa, baadhi wanaikimbia dunia na kufanya ibada za kibinafsi, wakipuuza majukumu yao kuzilea na kuhudumia familia. Baadhi huhalalisha kutokuwa na hima, kutojali na uvivu kwa msingi wa Dini. Baadhi hutekeleza matendo kama ya kiroho pekee, bila lengo. Wakiathiriwa na fikra za Wamagharibi za kujali maslahi tu kwa watu (nafa’iyyah), baadhi wanafuata kwa shauku maslahi ya kushikika, wakiwa na bidii ya kuchuma kwa kiwango ambacho familia na kujifunga kwao kiroho kunaathirika. Wanafikia hata kufuatilia manufaa ya kushikika kwa kiwango ambacho huwa kinaharibu maadili yao na ibada za kiroho. Baadhi hujionyesha kwenye ibada zao.

Kueleweka vibaya kwa lengo na madhumuni ya matendo katika Uislamu ni masaibu kama ya kuenea kwa mchwa, wanaokula matendo yetu mema na kutuwacha kwenye maangamizi katika dunia hii na Akhera. Inawasibu vijana miongoni mwetu, watu wazima miongoni mwetu pamoja na wazee. Inatusibu sisi katika elimu na wale wenye elimu ndogo. Inawasibu wale matajiri na wale waliotahiniwa na umasikini, ugumu na madeni. Ni masaibu ambayo yanaweza tu kutibika kwa uangalifu wa karibu, mazingatio, tafakuri, kujihesabu na marekebisho kwa mujibu wa Wahyi.

Kuhusiana na lengo (ghaayah) kwa kila mtu katika matendo yetu, nalo ni kutaka Radhi za Mwenyezi Mungu (swt) na sio chengine. Kwa hiyo tunapotekeleza Swalah, kutafuta elimu ya Dini, kuamrisha mema na kukataza maovu, kuhukumu kwa Uislamu, kupigana Jihad katika njia ya Mwenyezi Mungu (swt), kuhifadhi maisha ya mwanaadamu, kuwalea watoto wa umri mdogo wasiojitigemea, kuwaangalia wazee, madhaifu na wagonjwa, kuwa mwaminifu katika biashara, kuwa mpole kwa wanyama, biashara, kulima au kuzalisha bidhaa kiwandani, tunafanya haya yote huku tukitaka radhi za Mwenyezi Mungu (swt). Tunajikinga na Ghadhabu za Mwenyezi Mungu (swt) kwa kufuata maamrisho Yake (swt) na kuyawacha makatazo. Hivyo tunayapatanisha matendo yetu yote na Wahyi, Quran Tukufu na Sunnah Zilizobarikiwa.

Mwenyezi Mungu (swt) amesema,

[إِنَّمَا كَانَ قَوْلَ الْمُؤْمِنِينَ إِذَا دُعُوا إِلَى اللَّهِ وَرَسُولِهِ لِيَحْكُمَ بَيْنَهُمْ أَن يَقُولُوا سَمِعْنَا وَأَطَعْنَا ۚ وَأُولَٰئِكَ هُم الْمُفْلِحُونَ * وَمَن يُطِعِ اللَّهَ وَرَسُولَهُ وَيَخْشَ اللَّهَ وَيَتَّقْهِ فَأُولَٰئِكَ هُمُ الْفَائِزُونَ]

“Haiwi kauli ya Waumini wanapoitwa kwa Mwenyezi Mungu na Mtume wake ili ahukumu baina yao, ila ni kusema: Tumesikia, na tunatii. Na hao ndio wenye kufanikiwa. Na wenye kumtii Mwenyezi Mungu na Mtume wake, na wakamwogopa Mwenyezi Mungu na kumcha, basi hao ndio wenye kufuzu.” [Surah An-Nuur 24:51-52]. Muislamu ana lengo la kutaka Radhi za Mwenyezi Mungu (swt) na sio kuridhisha matashi yake na matamanio, kulingana na kile anachokiona katika manufaa ya kidunia, Mwenyezi Mungu (swt) amesema,

[وَأَنِ احْكُم بَيْنَهُم بِمَا أَنزَلَ اللَّهُ وَلَا تَتَّبِعْ أَهْوَاءَهُمْ وَاحْذَرْهُمْ أَن يَفْتِنُوكَ عَن بَعْضِ مَا أَنزَلَ اللَّهُ إِلَيْكَ]

“Na wahukumu baina yao kwa aliyoyateremsha Mwenyezi Mungu, wala usifuate matamanio yao. Nawe tahadhari nao wasije kukufitini ukaacha baadhi ya aliyokuteremshia Mwenyezi Mungu.”  [Surah al Maaida 5:49]. Hivyo sisi kama Waislamu lazima tufahamu, kabla ya kutenda, ima matendo yetu yanaendana na maamrisho na makatazo ya Mwenyezi Mungu (swt) na Mjumbe Wake (saw) au yanapingana nayo.

Ni Mwenyezi Mungu (swt) Aliyeumba kwetu ghariza ya kuabudu ambayo ni kubwa kuliko sisi, kuliko kuchuma na kupata faida kuhifadhi utajiri wa vitu na pia kuilea familia, kujenga ukaribu na mwenza wako, kuwakuza watoto na kuwahudumia wazee. Ni Mwenyezi Mungu (swt) Aliyetupatia maamrisho na makatazo kuitikia ghariza hizi, kuzishibisha kwa namna bora iwezekanayo, ili kuwa na shakhsia iliyopevuka na jamii njema zaidi iliyojaa raha na utulivu.

Ama kwa ibada za kibinafsi, (ibaadat), hukumu za Uislamu zinakamilisha maadili ya kiroho, kuwa na khofu ya Mwenyezi Mungu (swt) na kuongeza uchamungu wetu. Hivyo kuhusiana na kutafuta elimu, Mwenyezi Mungu (swt) amesema,

  [إنَّمَا يَخْشَى اللَّهَ مِنْ عِبَادِهِ الْعُلَمَاءُ إِنَّ اللَّهَ عَزِيزٌ غَفُورٌ]

“Hakika wanaomcha Mwenyezi Mungu miongoni mwa waja wake ni wanazuoni.”  [Surah al-Faatir 35:28]. Abdullah ibn Masud (ra) amesema,  ليس العلم عن كثرة الحديث، ولكن العلم عن كثرة الخشية  “Elimu sio kuwa na wingi wa maelezo lakini elimu ni wingi wa khofu.” Bila shaka yule anayeusoma Uislamu katika kipengele chochote, kwa moyo safi kwa ajili ya Mwenyezi Mungu (swt) hatokuwa vyengine isipokuwa ni mnyenyekevu kwa Uadilifu na Uongozi wa Mwenyezi Mungu (swt), atajawa na khofu na atakulia kwenye uchamungu. Kuhusiana na utekelezaji wa Saumu ya Ramadhan, sio tu katika jambo la kawaida la kujizuilia kula na kunywa, bali ni kuongeza uchamungu wetu. Mwenyezi Mungu (swt) amesema,

[يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا كُتِبَ عَلَيْكُمُ الصِّيَامُ كَمَا كُتِبَ عَلَى الَّذِينَ مِن قَبْلِكُمْ لَعَلَّكُمْ تَتَّقُونَ]

“Enyi mlioamini! Mmeandikiwa Saumu kama walivyoandikiwa walio kabla yenu ili mpate kuwa wachamungu.” [Surah al-Baqarah 2:183]. Bila shaka, yule anayefunga Saumu kwa moyo safi kwa ajili ya Mwenyezi Mungu (swt) hukulia katika Taqwa na kuwa mja mtiifu kwa Mwenyezi Mungu (swt), baraka ambazo tunazihisi zaidi wakati wa Ramadhan, ikiwa ni miongoni mwa nyenzo na rehema zake.

Katika matendo ya ibaadaat, kupitia maamrisho ya Mwenyezi Mungu (swt), lazima tufikie maadili ya kiroho na sio chengine. Riyaa ni ile wakati mtu anakusudia kupata ridhaa za watu kupitia ibaadaat, wakati kile kinachohitajika ni kujikurubisha zaidi kwa Mwenyezi Mungu (swt). Ni kutokana na matendo ya moyoni na sio matendo ya ulimi au viungo. Hivyo katika suala la riyaa, badala ya kutenda matendo kwa ajili ya kujikurubisha kwa Mwenyezi Mungu (swt), hutendwa kwa ajili ya watu. Kama madhumuni ya matendo yanachangiwa baina ya Mwenyezi Mungu (swt) na watu basi tendo hili la kujikurubisha kwa Mwenyezi Mungu ni Haram, linakaribisha Ghadhabu za Mwenyezi Mungu (swt) juu yetu! Mwenyezi Mungu (swt) amesema,

[الَّذِينَ هُمْ يُرَاءُونَ]

“Ambao wanajionyesha.” [Surah al-Ma’un 107:6]. Imam at-Tabari amesherehesha aya hii akasema, "الذين هم يراءون الناس بصلاتهم إذا صلوا، لأنهم لا يصلون رغبة في ثواب، ولا رهبة من عقاب، وإنما يصلونها ليراهم المؤمنون فيظنونهم منهم"‏ “Wale wanaotekeleza Swala ili watu wawaone wakiswali, kwa sababu hawaswali kwa kutegemea thawabu, wala khofu ya adhabu, bali wanaswali ili waumini wawaone na wawadhanie ni miongoni mwao.” Mtume (saw) amesema katika hadith ya Jandab iliopokelewa na al-Bukhari, «مَنْ سَمَّعَ سَمَّعَ اللَّهُ بِهِ وَمَنْ يُرَائِي يُرَائِي اللَّهُ بِهِ» “Anayetenda ili watu wamsikie, Mwenyezi Mungu atawafanya wamsikie, na anayetenda ili watu wamuone basi Mwenyezi Mungu atawafanya  wamuone.”[Bukhari].

Hivyo tuwe waangalifu juu ya Swala zetu misikitini, kwani ni kwa ajili ya kuongeza Uchamungu wetu, kwani Mtume wa Mwenyezi Mungu (saw) amesema, «يَكْشِفُ رَبُّنَا عَنْ سَاقِهِ فَيَسْجُدُ لَهُ كُلُّ مُؤْمِنٍ وَمُؤْمِنَةٍ، وَيَبْقَى مَنْ كَانَ يَسْجُدُ فِي الدُّنْيَا رِئَاءً وَسُمْعَةً، فَيَذْهَبُ لِيَسْجُدَ فَيَعُودُ ظَهْرُهُ طَبَقًا وَاحِدًا» “Mola wetu ataufunua muundi Wake, na watamsujudia kila muumini mke na mume, watabakia wale waliokuwa wakisujudu duniani kwa kuonyesha watu na kutaka kujulikana. Watataka kusujudu lakini migongo yao itashupaa kama mfupa mmoja.” [Bukhari]. Na tutekeleze Tahajjud bila hata wenza wetu au watoto kujuwa ili kuweka mpaka imara baina yetu na Riyaa. Tuwe waangalifu katika ibada ya kutafuta elimu, kwani ni kwa ajili ya kujenga khofu kwa Mwenyezi Mungu (swt) pekee, na sio kujijengea sifa katika mijadala kupitia kujionyesha. Mtume wa Mwenyezi Mungu (swt) amesema,  «مَنْ طَلَبَ الْعِلْمَ لِيُمَارِيَ بِهِ السُّفَهَاءَ أَوْ لِيُبَاهِيَ بِهِ الْعُلَمَاءَ أَوْ لِيَصْرِفَ وُجُوهَ النَّاسِ إِلَيْهِ فَهُوَ فِي النَّارِ»  “Atakayetafuta elimu ili abishanie na wajinga au ajionyeshee mbele ya wasomi au avutie mazingatio ya watu, ataingia motoni.” [Ibn Majah]. Tuwe waangalifu katika ibada ya Hajj, kwani inatukurubisha zaidi kwa Mwenyezi Mungu (swt) peke yake na sio kwa ajili ya kujivuna na kujisifia, kana kwamba ishara ya uchaji Mungu. Mtume (saw) alitekeleza Hajj juu ya tandiko kuu kuu, huku amevaa koti la thamani ya Dirham nne au chini yake. Kisha Mtume (saw) alisema, «اللَّهُمَّ حِجَّةٌ لاَ رِيَاءَ فِيهَا وَلاَ سُمْعَةَ» “Ewe Mwenyezi Mungu, Hajj isiyo na riyaa wala sifa” [Ibn Majah]. Hivyo hivyo, jeshi letu na lipigane kwa kutaka radhi za Mwenyezi Mungu {swt), licha ya kuwepo manufaa ya kidunia. Alikuja mtu kwa Mtume (saw) na kuuliza, “Mtu anapigana kwa ajili ya ngawira; mwengine anapigana kwa ajili ya umaarufu na wa tatu anapigana kwa kujionyesha; ni yupi kati yao anayepigana katika njia ya Mwenyezi Mungu?” Mtume (saw) akasema, «مَنْ قَاتَلَ لِتَكُونَ كَلِمَةُ اللَّهِ هِيَ الْعُلْيَا فَهُوَ فِي سَبِيلِ اللَّهِ» “Anayepigana ili Neno la Mwenyezi Mungu (yaani Uislamu) liwe juu kabisa, basi anapigana katika Njia ya Mwenyezi Mungu.” [Bukhari].

Ama kwa mtawaliwa, na amuwajibishe mtawala kujiweka karibu na Mwenyezi Mungu (swt), kwa kumkhofia Yeye pekee, bila kusita sita kwa kumuogopa mtu, kwani Mtume (saw) amesema, «أَفْضَلُ الْجِهَادِ كَلِمَةُ عَدْلٍ عِنْدَ سُلْطَانٍ جَائِرٍ» “Jihad bora zaidi ni tamko la haki mbele ya mtawala jeuri,” [Abu Dawood]. Kwa hakika, ni khofu ya Mwenyezi Mungu (swt) pekee ambayo inamruhusu yule anayebeba jukumu kuishinda khofu kwa wale walio madarakani, kusimama mbele ya madhalimu makatili. Mwenyezi Mungu (swt) amesema, أَتَخْشَوْنَهُمْ فَاللَّهُ أَحَقُّ أَن تَخْشَوْهُ إِن كُنتُم مُّؤْمِنِينَ  “Je mnawaogopa? Basi Mwenyezi Mungu anastahiki zaidi mumwogope, ikiwa nyinyi ni Waumini.” [Surah at-Tawbah 9:13]. Kwa upande wa mtawala, na ajikurubishe zaidi kwa Mwenyezi Mungu (swt) kwa kuhukumu kwa yote aliyoyateremsha Yeye (swt). Asijidhalilishe mwenyewe, kukaribisha hasira za Mwenyezi Mungu (swt) kwa kuupuuza Uislamu kupitia mapenzi ya mitego ya utawala na hadhi. Mtume (saw) amesema, «إِنَّ أَحَبَّ النَّاسِ إِلَى اللَّهِ يَوْمَ الْقِيَامَةِ وَأَدْنَاهُمْ مِنْهُ مَجْلِسًا إِمَامٌ عَادِلٌ وَأَبْغَضَ النَّاسِ إِلَى اللَّهِ وَأَبْعَدَهُمْ مِنْهُ مَجْلِسًا إِمَامٌ جَائِرٌ»  “Hakika anayependeza zaidi mbele ya Mwenyezi Mungu siku ya Kiama, na atakayekuwa na hadhi ya karibu zaidi Kwake ni Kiongozi (Imam) muadilifu. Na anayechukiza zaidi kwa Mwenyezi Mungu na atakayekuwa na hadhi ya mbali zaidi Kwake ni kiongozi (Imam) jeuri.” [Tirmidhi]. Mtawala ajikurubishe zaidi kwa Mwenyezi Mungu (swt) kwa kujifunga na haki, kuitekeleza, badala ya kuiacha haki kutokana na matamanio yake kwa kuwaridhisha watu. Aisha (ra) amesema, Nimemsikia Mtume wa Mwenyezi Mungu (saw) akisema, «مَنِ الْتَمَسَ رِضَاءَ اللَّهِ بِسَخَطِ النَّاسِ كَفَاهُ اللَّهُ مُؤْنَةَ النَّاسِ وَمَنِ الْتَمَسَ رِضَاءَ النَّاسِ بِسَخَطِ اللَّهِ وَكَلَهُ اللَّهُ إِلَى النَّاسِ» “Anayetaka radhi za Mwenyezi Mungu kwa hasira za watu, Mwenyezi Mungu atamtosheleza kutokana na watu. Na anayetaka radhi za watu kwa hasira za Mwenyezi Mungu, Mwenyezi Mungu atamkabidhisha kwa watu.” [Tirmidhi]

Uangalifu huo kwa thamani ya kiroho huifanya shakhsia ya Muislamu kuwa ni shakhsia ilio ya juu, ambapo kuna mazingira ya kumkumbuka Mwenyezi Mungu (swt), kumshukuru na kutaka Radhi Zake. Hii iko mbali na jamii ya kisekula, ambayo inahangaika chini ya pengo jeusi la ombwe la kiroho.

Kwa upande wa miamala ya kiuchumi, wakati lengo letu ni kutaka radhi za Mwenyezi Mungu (swt) kupitia utekelezaji wa maamrisho ya Mwenyezi Mungu (swt), tunapata thamani ya kushikika, ambayo ni faida ya kushikika na pato la kushikika. Dini yetu, Uislamu, sio dini ya kisekula, inayotoa miongozo kwa ibada ya kibinafsi pekee, ni mkusanyiko wa sheria zote za kimaisha, zinazotawala mambo yetu yote. Hivyo unapoajiri, Uislamu unatutaka kutekeleza malipo. Mtume (saw) amesema, «إِذَا اسْتَأْجَرْتَ أَجِيرًا فَأَعْلِمْهُ أَجْرَهُ»‏ “Unapomuajiri mtu, mjuilishe mshahara wake.” [an-Nisaa’i]. Bila shaka, kumuajiri mfanyakazi ni kwa lengo la kutaka radhi za Mwenyezi Mungu (swt). Inalazimisha kukamilisha lengo la tendo, ambalo ni thamani ya kushikika, kwa hapa ni mshahara. Hivyo, kuajiri hakuwi bure bila lengo. Mfanyakazi lazima alipwe malipo yake; vyenginevyo, Mwenyezi Mungu (swt) atapambana kwa ajili yake. Mtume (saw) amesema, «قَالَ اللَّهُ ثَلَاثَةٌ أَنَا خَصْمُهُمْ يَوْمَ الْقِيَامَةِ رَجُلٌ أَعْطَى بِي ثُمَّ غَدَرَ وَرَجُلٌ بَاعَ حُرًّا فَأَكَلَ ثَمَنَهُ وَرَجُلٌ اسْتَأْجَرَ أَجِيرًا فَاسْتَوْفَى مِنْهُ وَلَمْ يُعْطِ أَجْرَهُ»  “Amesema Mwenyezi Mungu (swt), Watu watatu nitahusumiana nao siku ya Kiyama: Yule aliyefunga mkataba kwa jina langu kisha akauvunja; yule aliyemuuza mtu huru kuwa mtumwa na kula thamani yake; na mtu aliyemuajiri mfanyakazi na kukamilishiwa kazi yote kutoka kwake na asimpe ujira wake.” [Al-Bukhari]. Katika kilimo, Uislamu umeruhusu thamani ya kushikika, kama mapato ya ardhi maiti kwa kuilima. Mtume (saw) amesema, «مَنْ أَحْيَا أَرْضًا مَيْتَةً فَهِيَ لَهُ» “Anayeihuisha ardhi maiti basi huwa ni yake”. Kisha akaitowa hadith mfano wa hiyo iliotajwa juu. [Abu Dawuud]. Katika viwanda na biashara, Uislamu umeruhusu uundwaji wa makampuni na katika kitendo hichi, Waislamu hupata thamani ya kushikika ya faida. Kuhusiana na ushirika wa Mudharaba, ‘Abdurrazaq amenukuu katika Al-Jami’ kuwa Imam Ali (ra) amesema, "الْوَضِيعَةِ عَلَى الْمَالِ، وَالرِّبْحُ عَلَى مَا اصْطَلَحُوا عَلَيْهِ" “Hasara ni juu ya mtaji, na faida ni kulingana na mapatano.” Hivyo Muislamu ni mshirika katika kampuni akilenga kupata faida na huchukua fungu lake kutoka kwa kile kilichokubaliwa, na hii pia ni thamani ya kushikika.

Hivyo, tunapoingia kwenye biashara, tunakuwa waangalifu kupata thamani ya kushikika na hatuwi wenye kupuuza. Matendo hatuyachukulii hivi hivi tu au kuwa wavivu na wazito, katika msingi wa kuwa Rizqi ni kutoka kwa Mwenyezi Mungu (swt) pekee; hata hivyo, kuhangaikia mali za kushikika ni amri ya Mwenyezi Mungu (swt) ambapo ni lazima tusipuuzie. Na tufahamu sote maamrisho ya kuhangaikia kuitafuta Rizqi, katika muongozo wa kuifahamu Rizqi yenyewe. Mwenyezi Mungu (swt) amesema,

[هُوَ الَّذِي جَعَلَ لَكُمْ الأَرْضَ ذَلُولاً فَامْشُوا فِي مَنَاكِبِهَا وَكُلُوا مِنْ رِزْقِهِ]

“Yeye ndie aliyeidhalilisha ardhi kwa faida yenu, basi tembeeni katika pande zake, na kuleni katika rizki zake.” [Al-Mulk 67: 15].

[فَإِذَا قُضِيَتْ الصَّلاَةُ فَانتَشِرُوا فِي الأَرْضِ وَابْتَغُوا مِنْ فَضْلِ اللَّهِ]

“Na itakapokwisha Swala, tawanyikeni katika nchi mtafute fadhila za Mwenyezi Mungu.” [Al-Jumu’ah 62: 10].

Kupata thamani ya kiroho kupitia kujifunga kwa kile kinachomridhisha Mwenyezi Mungu (swt), kunaifanya shakhsia ya Muislamu kuwa ni shakhsia yenye kuzaa matunda. Anahangaika kwa bidii kubwa kwa ajili ya mahitaji ya familia yake na katika mahitaji ya ziada, akitaka radhi za Mola wake (swt). Hawi katika walio wavivu, wazito, wenye kuchukua mikopo bila hadhari na kutaka misaada, bila kuzingatia kwa makini. Uangalifu huo kwa ajili ya thamani ya kushikika huifanya jamii ya Kiislamu jamii yenye mali, ustawi na uwezo, ambapo mahitaji ya masikini, wale walio katika hali ngumu na katika madeni, huangaliwa kwa kuwepesishiwa hali zao. Kwa hakika, katika zama za Khilafah, ardhi za Waislamu zilikuwa ni vyanzo vya wivu kutokana na maendeleo yake makubwa.

Ama kwa suala la kuwahudumia wanaadamu, wakati tunahangaika kwa ajili ya radhi za Mwenyezi Mungu (swt), hukumu za Uislamu zinatuhakikishia kuwa tumefanikiwa katika thamani ya kibinaadamu, kama kuhifadhi maisha ya mwanaadamu, pamoja na uangalizi na huruma kwa wanaadamu wengine. Mwenyezi Mungu (swt) amelazimisha kuhifadhiwa maisha ya mwanaadamu, bila kuzingatia rangi, kabila au dini. Mwenyezi Mungu (swt) amesema,

  [وَمَنْ أَحْيَاهَا فَكَأَنَّمَا أَحْيَا النَّاسَ جَمِيعًا]

“Na mwenye kumuokoa mtu na mauti ni kama amewaokoa watu wote.” [Surah al-Maaidah 5:32]. Ibn Kathir amesema kutoka kwa Mujahid, "أنجاها من غرق أو حرق أو هلكة" “Ihifadhi kutokana na kuzama au kuungua au kuangamia.” Kwa upande wa mkataba wa ndoa, Uislamu umetuamrisha kukaa kwa wema na wenza wetu. Mwenyezi Mungu (swt) amesema,

[وَمِنۡ ءَايَٰتِهِ أَنۡ خَلَقَ لَكُم مِّنۡ أَنفُسِكُمۡ أَزۡوَٰجٗا لِّتَسۡكُنُوٓاْ إِلَيۡهَا وَجَعَلَ بَيۡنَكُم مَّوَدَّةٗ وَرَحۡمَةً]

“Na katika ishara zake ni kuwa amekuumbieni wake zenu kutokana na nafsi zenu ili mpate utulivu kwao.  Naye amejaalia mapenzi na huruma baina yenu.” [Surah ar-Rum 30:21]. Mtume (saw) amesema, «خِيَارُكُمْ خِيَارُكُمْ لِنِسَائِهِمْ» “Mbora wenu ni yule aliye mbora zaidi kwenu kwa wakeze.” [Ibn Majah].

Kwa hiyo tunaowa na kuishi na wake zetu kwa wema, mapenzi na huruma. Tunapata pia thamani ya kiutu, kupitia kutekeleza agizo la kutaka watoto wengi. Mtume (saw) amesema, «تَزَوَّجُوا الْوَدُودَ الْوَلُودَ فَإِنِّي مُكَاثِرٌ بِكُمُ الْأُمَم»  “Oweni wanawake wenye mapenzi na wenye kizazi, kwani Mimi nitawazidi ummah nyengine kwenu.” [Abu Dawood]. Sisi huwa waangalifu katika kuwashughulikia ndugu zetu na watoto, ima wanaume au wanawake. Mtume (saw) amesema, «مَنْ كَانَ لَهُ ثَلاَثُ بَنَاتٍ أَوْ ثَلاَثُ أَخَوَاتٍ أَوِ ابْنَتَانِ أَوْ أُخْتَانِ فَأَحْسَنَ صُحْبَتَهُنَّ وَاتَّقَى اللَّهَ فِيهِنَّ فَلَهُ الْجَنَّةُ» “Yeyote mwenye mabinti watatu, au dada watatu au mabinti wawili au dada wawili na akasuhubiana nao kwa wema na akamcha Mwenyezi Mungu kuhusu wao, basi Pepo ni juu yake.” [Tirmidhi]. Uislamu umeagiza juu ya watoto kuwahudumia wazee katika umri wowote na maradhi yoyote. Abu Hurayra (ra) ameelezea kuwa mtu mmoja alisema: Mtume wa Mwenyezi Mungu, ni nani miongoni mwa watu anastahiki zaidi kufanyiwa wema? Mtume wa Mwenyezi Mungu akasema, ,«أُمُّكَ ثُمَّ أُمُّكَ ثُمَّ أُمُّكَ ثُمَّ أَبُوكَ ثُمَّ أَدْنَاكَ أَدْنَاكَ» “Mama yako, kisha mama yako, kisha mama yako, kisha baba yako, kisha wa karibu yako zaidi kwa mfuatano.” [Muslim]. Tunahitaji kuwa waangalifu katika kumakinisha fungamano la uhusiano wa damu, kufuatilia jamaa na kushughulikia mahitaji yao kadiri iwezekanavyo. Mtume wa Mwenyezi Mungu (saw) amesema, «خَلَقَ اللَّهُ الْخَلْقَ، فَلَمَّا فَرَغَ مِنْهُ قَامَتِ الرَّحِمُ فَأَخَذَتْ بِحَقْوِ الرَّحْمَنِ فَقَالَ لَهَا مَهْ‏.‏ قَالَتْ هَذَا مَقَامُ الْعَائِذِ بِكَ مِنَ الْقَطِيعَةِ‏.‏ قَالَ أَلاَ تَرْضَيْنَ أَنْ أَصِلَ مَنْ وَصَلَكِ وَأَقْطَعَ مَنْ قَطَعَكِ‏.‏ قَالَتْ بَلَى يَا رَبِّ‏.‏ قَالَ فَذَاكِ لَكِ» “Mwenyezi Mungu ameumba viumbe vyake, na alipomaliza likasimama fuko la uzazi na likashikwa na Mwenyezi Mungu ambapo Mwenyezi Mungu akaliambia, “Kuna nini?” Likasema: najilinda kwake na yeyote anayakata kizazi. Akasema Mwenyezi Mungu (swt) hivyo huridhii kumuunga yule anayekuunga na kumkata yule anayekukata?. Likasema, kwa nini ewe Mola wangu! Mwenyezi Mungu akasema, ‘Basi hilo ni la kwako.” [Al-Bukhari]. Mtume (saw) amesema, ‏«لَيْسَ الْوَاصِلُ بِالْمُكَافِئِ وَلَكِنْ الْوَاصِلُ الَّذِي إِذَا قُطِعَتْ رَحِمُهُ وَصَلَهَا»‏ “Hakuwa mwenye kuunganisha yule anayerudisha fadhila, bali mwenye kuunganisha ni yule ambaye pindi kizazi chake kinapomkata yeye hukiunga.” [Al-Bukhari].

Kupitia kujifunga na Sheria za Uislamu zinazohusu familia na jamaa, hatuwi watu wenye kusaka biashara, faida na kipato tu. Muelekeo wetu wa kifamilia na masuala jumla huwa yenye nguvu kuliko kuwa yameelemewa na ubinafsi. Lazima tuwe waangalifu kwa kumtii Mwenyezi Mungu (swt) katika mambo yote, kuwapatia wanaadamu, majirani zetu na familia zetu haki zao kwa kufuata matendo ya kisharia ambayo yanazalisha thamani ya kiutu. Waislamu hujali zaidi wale waliowazunguka, kuwapa haki zao wengine kabla ya kuzitaka zao wao. Mahusiano baina ya mke na mume sio ya watu wawili binafsi kugombania haki zao kila mmoja, bali ni ushirikiano baina yao ambapo huwa ni vyanzo vya utulivu na mapenzi baina yao. Watu kuwa wazazi hakuzingatiwi kuwa ni muingilio juu ya hamu ya matarajio ya mtu mmoja mmoja, bali ni fursa ya kumkuza mtoto katika wema na uangalifu. Wazee vikongwe hawazingatiwi kuwa ni usumbufu, bali ni fursa ya kupata baraka kutoka kwa Mwenyezi Mungu (swt). Hivyo, jamii ya Kiislamu ina kitengo cha familia ambacho ni ngome, tofauti na jamii ya kisekula, ambapo mafungamano ya mahusiano na huduma kwa mwanaadamu ni yenye kudharauliwa.

Ama kwa upande wa kutafuta maadili, hukmu za Kisharia zinazohusiana na maadili hufanywa kwa lengo la kutaka radhi za Mwenyezi Mungu (swt). Uislamu unatutaka kufikia thamani ya kiroho, kama kusifika na ukweli uaminifu. Mtume (saw) amesema, «إِنَّ مِنْ خِيَارِكُمْ أَحْسَنَكُمْ أَخْلاَقًا» “Mbora wenu ni yule mwenye tabia nzuri zaidi.” [Bukhari]. Mtume (saw) amesema, «أَكْثَرُ مَا يُدْخِلُ اَلْجَنَّةَ تَقْوى اَللَّهِ وَحُسْنُ اَلْخُلُقِ» “Kumcha Mwenyezi Mungu na kuwa na tabia njema ndio mambo yanayoingiza Pepo sana.” [Tirmidhi]. Hivyo tunakuwa wakweli kwa sababu Mwenyezi Mungu (swt) ametutaka kuwa wakweli na tunakuwa waaminifu kwa sababu Mwenyezi Mungu (swt) ametutaka kubeba amana. Hatuwi ni wenye akhlaqi njema kwa sababu ya manufaa yoyote ya kushikika, kama kuwafanya watu wanunue kutoka kwetu au watuchague kwenye nyadhifa fulani. Hii ndio inayotafautisha ukweli wa anayetaka kumridhisha Mwenyezi Mungu (swt) kutokana na yule anayetaka kujiridhisha yeye mwenyewe. Wa mwanzo ni mkweli hasa kwa sababu Mwenyezi Mungu (swt) ametutaka kuwa wakweli, wakati yule mwengine ni mkweli kwa sababu ya maslahi, kwa msingi wa falsafa fisidifu ya Kimagharibi ya kuangalia maslahi. Ukweli sio sera; ni amri kutoka kwa Muumba wa Ulimwengu ambao lazima tuutekeleze. Tutakuwa wakweli hata kama kuna maslahi ya kushikika kwengineko. Tunatii maamrisho ya Mwenyezi Mungu (swt) ya kuwa na akhlaqi njema hadi tupate thamani ya kiakhlaqi, ambayo inasifika kwa ukweli. Mtume (saw) amesema, «عَلَيْكُمْ بِالصِّدْقِ فَإِنَّ الصِّدْقَ يَهْدِي إِلَى الْبِرِّ وَإِنَّ الْبِرَّ يَهْدِي إِلَى الْجَنَّةِ وَمَا يَزَالُ الرَّجُلُ يَصْدُقُ وَيَتَحَرَّى الصِّدْقَ حَتَّى يُكْتَبَ عِنْدَ اللَّهِ صِدِّيقًا وَإِيَّاكُمْ وَالْكَذِبَ فَإِنَّ الْكَذِبَ يَهْدِي إِلَى الْفُجُورِ وَإِنَّ الْفُجُورَ يَهْدِي إِلَى النَّارِ وَمَا يَزَالُ الْعَبْدُ يَكْذِبُ وَيَتَحَرَّى الْكَذِبَ حَتَّى يُكْتَبَ عِنْدَ اللَّهِ كَذَّابًا» “Juu yenu kujifunga na ukweli, kwani ukweli unaongoza kwenye wema. Na hakika wema unaongoza kwenye Pepo. Na hatoacha mtu kusema ukweli na kujitahidi kusema ukweli hadi ataandikwa mbele ya Mwenyezi Mungu kuwa ni mkweli. Jiepusheni na uongo, kwani uongo hupelekea kwenye uovu, na uovu hupelekea kwenye Moto. Na hatoacha mja kusema uongo na kujitahidi kusema uongo hadi ataandikwa mbele ya Mwenyezi Mungu kuwa ni muongo.” [At-Tirmidhi]. Hivyo mfanya biashara atakuwa mkweli katika biashara hata kama utampelekea kwenye hasara ya kushikika, kama atabainisha kasoro katika bidhaa au kumjulisha yule asiye na uelewa wa viwango vya soko na mfano wake.

Kupitia kumtii Mwenyezi Mungu (swt), upatikanaji wa thamani ya kiakhlaqi huwahakikishia Waislamu kuwa ni watu wa juu, waliopambika kwa akhlaqi nyingi zilizo njema zinazoelezwa na Wahyi. Waislamu ni wakweli na sio wadanganyifu. Waislamu ni wakarimu na sio wachoyo. Wao ni wapole na sio wakali. Ni wachangamfu na sio wanyonge na wenye kulalamika. Wanafikra nyofu kwa waumini na sio wenye shuku na shaka. Kukimbilia kwao kwenye akhlaqi njema ni kwa ajili ya kutaka radhi za Mwenyezi Mungu (swt) na sio kwa ajili ya akhlaqi zenyewe, hivyo kujifunga kwao kunakuwa ni endelevu na bila usumbufu. Kukimbilia kwao ni kwa ajili ya kutaka radhi za Mwenyezi Mungu (swt) na sio manufaa ya kushikika au shukran kwa watu, hivyo hakuna unafiki au undumakuwili katika kufuatilia kwao. Hivyo, wote wanakuwa sehemu ya jamii ambayo imejaa ukarimu, ukweli, utulivu na uaminifu, ni jamii ambayo kuishi ndani yake ni furaha.

Hakika ni kuwa Dini ya Uislamu inatowa watu werevu na jamii iliojengeka vyema. Zama za Uislamu ni shahidi wa miaka alfu kumi na tatu ya mpangilio bora wa Uislamu kwa mwanaadamu. Uislamu umetoa kikosi cha watu wengi wenye sifa za kipekee na jamii iliojawa na huruma, utulivu, moyo wa kujifunga kiroho, uchapa kazi wa kusisimua na neema. Wakati Ummah wa Kiislamu ukinyanyuka kutoka kwenye dimbwi la mporomoko wake, ukisubiri kurejea kwa Khilafah kusiko na shaka, na tuwe waangalifu kila mmoja wetu kwa kila tendo letu, kuhakikisha ukamilifu wake, kukamilisha thamani yake, kwa ajili ya radhi za Mwenyezi Mungu (swt). Hakika, sio muda mrefu kabla hatujaiona siku ambayo matendo yote yataonekana, hata kama ni tendo dogo kiasi gani, katika siku ambayo uzito wowote wa jambo zuri utakuwa na afueni kubwa katika mizani. Mwenyezi Mungu (swt) amesema,

[فَمَن يَعْمَلْ مِثْقَالَ ذَرَّةٍ خَيْرًا يَرَهُ]

“Basi anayetenda chembe ya wema atauona.” [TMQ Surah al-Zalzala 99:7]. Mwenyezi Mungu (swt) amesema,

[وَمَنۡ خَفَّتۡ مَوَ ٰزِینُهُۥ فَأُو۟لَـٰۤىِٕكَ ٱلَّذِینَ خَسِرُوۤا۟ أَنفُسَهُمۡ فِی جَهَنَّمَ خَـٰلِدُونَ]

“Na wale ambao mizani zao zitakuwa nyepesi, hao ndio waliozitia khasarani nafsi zao, na katika Jahannamu watadumu.” [TMQ Surah Al-Mu'minoon 23: 103].

Imeandikwa kwa Ajili ya Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir na

Musab Umair - Pakistan

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

rudi juu

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu