Logo
Chapisha ukurasa huu

Afisi ya Habari
Kenya

H.  8 Safar 1443 Na: 1443/03 H
M.  Jumatano, 15 Septemba 2021

 Taarifa kwa Vyombo vya Habari

Bei ghali ya Mafuta: Kufeli Kiujumla Kwa Mfumo wa Ubepari wa Kiushuru

Kama ilivyotarajiwa, kwa mara nyengine tena bei ya mafuta imepanda maradufu kuwahi kushuhudiwa katika historia ya Kenya baada ya serikali kusitisha mpango wake wa kulipia gharama za bidhaa za petroli ulioanzishwa mwezi Aprili mwaka huu kama njia ya kuepusha hasira za raia dhidi ya gharama kubwa za maisha. Mamkala ya Kudhibiti Kawi na mafuta EPRA iliondosha mapungufu ya bei ya mafuta yaliyouzwa katika mwezi uliopita hadi Septemba 14; Ksh 7.10 kwa petrol, Ksh 9.90 kwa Dizeli na kwa mafuta ya taa Ksh 11.36. Jijini Nairobi lita moja ya petrol sasa ni Ksh 134.72 baada ya bei ya awali ya Ksh 127.14. Bei ya Dizeli iliokuwa Ksh 107.66 sasa imepanda hadi Ksh.115.60 na mafuta ya taa sasa yakiuzwa kwa Ksh.110.82 kutoka kwa Ksh.97.85 hapo awali.

Kinachotamausha, ni kwamba kupanda huku kwa bei kunakuja wakati ambapo maeneo ya kaskazini na pwani ya nchi yanakodolewa na baa la nja kutokamana na ukame uliotangazwa kuwa ni janga la kitaifa. Gharama ya juu ya mafuta huathiri pakubwa karibu sekta zote za uchumi na huwa na athari kubwa kwa gharama za maisha. Hii ni dhahiri shahiri kwamba mataifa ya kibepari huzidishia raia wake maumivu zaidi na viongozi wake hawajali kikweli maslahi ya raia wanaodai kuwaongoza.

Kuhusu suala la kupanda kwa bei ya mafuta, hii husababishwa na mambo mawili nayo: ukiritimba katika uzalishwaji wa rasilimali hii na suala la utozwaji ushuru katika viwanda vya kawi. Kimataifa, maeneo yanayozalisha mafuta yanamilikiwa na makampuni makubwa ya Kimagharibi ndani ya mwavuli wa shirika la nchi zinazosafirisha mafuta duniani (OPEC). Ukiritimba wa mali hii yenye thamani kubwa ya kiuchumi umefanya mataifa ya ulimwengu wa tatu uwe chini ya matakwa ya OPEC kwenye suala la uzalishaji wa mafuta, usambazwaji wake na hata bei. Mabepari ndio hutumia OPEC kama zana ya kudhibiti na kupelekea masuala yote ya biashara ya mafuta. Uhalisia huu kimakusudi huwa hauzungumziwi bali hupuuzwa na Warasilimali wa Kimagharibi. Ama kuhusu utozaji ushuru hili liko bayana kwani serikali huweka ushuru mwingi katika bidhaa za mafuta. Muhimu kubainika kwamba katika mfumo wa Kirasilimali njia rahisi ya serikali kupata mapato yake ni kupitia kutoza ushuru wa mafuta. Kwa hali yetu hapa Kenya kwa mfano hukusanya jumla ya shilingi 57 za ushuru wa Petroli, Shilingi 45.47 kwa Dizeli na shilling 39.5 kwa mafuta ya taa. Ongezeko hili la bei ni jaribio jengine la serikali kuokoa uchumi wake unaoendelea kudorora huku mfumuko wa bei ukiwa asilimia 6.6 dhidi ya dolari. Kuanguka kwa thamani ya shilingi ni dalili wazi ya kusuasua kwa hali ya uchumi hasa ikizingatiwa uchumi wa Kenya unategemea uagizaji mno wa bidhaa na kufanya kuweko mwanya mkubwa baina ya bidhaa zinazoagizwa kutoka nje na zile zinazosafarishwa nje kwa shilingi hali inayofanya serikali iweze kutoza bidhaa za mafuta. Yasikitisha tukitabiri kwa hali hii tata ya kiuchumi huenda ikapelekea marufuku ya uagizwaji wa bidhaa zisizokuwa na umuhimu kama njia ya kujaribu kunasua mdororo wa shilingi na uchumi dhidi ya makali ya Dolari.

Kwa hali hii tulioangazia, ni wazi kwamba utawala wowote unaopeleka mfumo wake kwa misingi ya mikopo ya uchapishaji pesa za makaratasi ni wenye kusababishia maafa zaidi kwa raia wake. Isitoshe, uchumi nchi yoyote leo umefungwa na matakwa na maoni ya serikali kuu duniani – Marekani. Ongezeko la bei ya mafuta na tatizo lolote la kiuchumi litatatuliwa tu na Dola ilio huru kikweli inayotekeleza Mfumo wa Kiuchumi wa Kiislamu uliobaini kwamba mali kama vile Maji, Malisho na Kawi yote haya ni mali ya umma kama ilivyosimuliwa na Ibn Majah kwamba Mtume SAAW alisema:

«الْمُسْلِمُونَ شُرَكَاءُ فِي ثَلَاثٍ:‏‏‏‏ فِي الْمَاءِ وَالْكَلَإِ وَالنَّارِ»

“Waislamu wana ushirika kwa mambo matatu: Katika Maji, Malisho na Kawi.

Shabani Mwalimu

Mwakilishi kwa Vyombo Vya Habari wa Hizb ut Tahrir

Kenya

Hizb-ut Tahrir: Afisi ya Habari
Kenya
Address & Website
Tel:  +254 707458907
E-Mail: mediarep@hizb.or.ke

Template Design © Joomla Templates | GavickPro. All rights reserved.