Logo
Chapisha ukurasa huu

بسم الله الرحمن الرحيم

 Dori Yetu Katika Vita vya Ukraine ni Kufichua Propaganda

(Imetafsiriwa)

Vita katika Ukraine vimeiweka Magharibi katika mapambano dhidi ya adui wake wa muda mrefu – Urusi. Vyombo vya habari, maafisa na waungaji mkono wa Urusi na Magharibi, wamepamba moto kuzishinda nyoyo na akili za walimwengu. Vita vya propaganda kwa namna nyingi vimekuwa ni muhimu zaidi kuliko vita halisi katika uwanja wa mapambano kwa kuwa vinaathiri hisia na kuvutia uungaji mkono kwenye malengo yao. Kutokana na hili, ni muhimu katika masiku na wiki zijazo, sisi Waislamu kuchukua nafasi ya wazi na kuongoza bila uegemezi wa upande wowote, nafasi za uchambuzi wa umakinifu.

Masimulizi ya Wamagharibi ni kuwa mchokozi Urusi imeivamia dola huru, ya kidemokrasia na lazima izuiliwe. Katika karne ya 21, matendo kama haya ya kale hayana nafasi; yanapingana na sheria za kimataifa pamoja na mpango wa kanuni za kimataifa. Putin ni muovu na amenuia kutenda matendo yake bila hadhari juu ya ubwana wa dunia na lazima azuiwe.

Masimulizi ya Urusi ni kuwa, tokea kuvunjika kwa Umoja wa Kisovieti mnamo 1991, Urusi imekumbwa na balaa na imekuwa ikidhalilishwa. Tokea kuvunjika kwa Umoja wa Kisovieti, Magharibi kupitia NATO na EU imejitanua hadi mipaka ya Urusi. Wakati Umoja wa Kisovieti ulipofanya kama hayo na kujitanua hadi Cuba mnamo 1962, Amerika ilijitayarisha kuingia kwenye vita vya nyuklia, hivyo leo hii vipi Urusi iwaangalie Wamagharibi wakijitanua hadi mipakani mwake? Urusi imelazimika kujibu na imeivamia Ukraine kwa lengo hili kupeleka ujumbe kwa Wamagharibi kuwa sasa imetosha.

Tunapoangalia masimulizi yote haya mawili, kuna dosari nyingi katika hoja na masuala mengi kuyahusu.

Vita hivi vitaelekea kutambulika daima kwa kuonyesha unafiki wa wazi na undumila kuwili wa Wamagharibi. Wanapiga mayowe juu ya sheria za kimataifa dhidi ya Urusi lakini hili wameliweka upande linapokuja suala la Iraq au Wazayuni wanapojitanua na kuuwa Waislamu. Wamagharibi wanapiga kelele kuhusu mpango wa sheria za kimataifa, lakini ilikuwa ni Bush na Blair waliozikanyaga na kuzitupa ndani ya pipa la taka la historia. Wamagharibi wanazungumza kuhusu kulinda haki na uhuru wa watu wa Ukraine, lakini baada ya miongo miwili ya ‘kuwakomboa’ watu wa Iraq na Afghanistan, maisha yao yamekuwa mabaya zaidi hivi leo kuliko kabla ya ‘kukombolewa’.

Fainali ya Ligi ya Mabingwa imeondoshwa kutoka Urusi na waziri wa kigeni wa Uingereza ameeleza katika taarifa kuwa, anaunga mkono moja kwa moja watu wa Uingereza kupigana Ukraine. EU imekuwa na mikutano juu ya namna bora zaidi ya kuwashughulikia wakimbizi wa Ukraine wanaoikimbia nchi wakati Urusi ikiivamia. Formula 1 Grand Prix imefanyika karibuni nchini Saudi Arabia licha ya kuwa nchi hii inatekeleza mauwaji nchini Yemen. Waislamu wengi Uingereza bado wapo jela kwa kuwaunga mkono ndugu zao na dada zao dhidi ya utawala dhalimu wa Bashar al-Assad. Na imekuwa wazi zaidi hivi sasa kuwa raia wanaokimbia vita kutoka Ukraine sio sawa na Waislamu wanaokimbia kutoka nchi zilizovurugwa kwa vita.

Kutowiana huku ni kwa sababu maslahi ya taifa na sio kiwango maalum cha maadili ndicho Wamagharibi huamulia kwacho juu ya vita halali na kipi sahihi na kipi sio sahihi.

Baadhi huona kuwa kwa sababu Urusi imesimama dhidi ya Amerika hufikiria kuwa adui wa adui yangu ni rafiki yangu. Tukiwa Waislamu, lazima tutambue kuwa Crimea na sehemu za Kusini ya Ukraine zilikuwa ni ardhi za Waislamu. Wauthmaniya walijitanua kwenye Bahari Nyeusi na iliwasaidia Waislamu wa Tatar walioeneza Uislamu hadi Urusi na Caucasia. Ilikuwa ni kwa sababu hii ndipo Warusi muda wote wamekuwa katika vita na Waislamu. Kutoka kwa Ivan Katili hadi kwa Stalin, watawala wa Urusi wamekuwa wakifanya mauwaji ya kuendelea dhidi ya Waislamu. Vladimir Putin katika Chechnya na karibuni nchini Syria pia wana damu ya Waislamu mikononi mwao; yeye sio rafiki wa Waislamu na ana rekodi sawa na Waingereza na Amerika kwa Waislamu; hao wote wana damu ya Waislamu mikononi mwao.

Urusi hivi leo sio kama Umoja wa Kisovieti na haina cha kuwapa Waukraine au Waislamu. Urusi chini ya Ukomunisti ilikuwa na ujumbe wa kiulimwengu, lakini leo haina cha kutoa na hiyo ndio sababu ya kuvamia nchi nyengine ili kuzishinda nyoyo na akili zao.

Huku Urusi na Magharibi zote zikisukuma propaganda zao, hali katika maeneo yao yote inaeleza hadithi tafauti. Wamagharibi wanajaribu kuonyesha kuwa wanalinda Haki za Binaadamu na mamlaka ya kitaifa, na Urusi inajaribu kuonyesha kuwa wao ni nguvu inayopaswa kuzingatiwa. Imani juu ya demokrasia, ubepari na uaminifu wa Magharibi upo kwa kiwango cha chini kabisa. Kutokuwepo kwa usawa, ufisadi na uwakilishi serikalini wa asilimia moja tu umepelekea imani katika tabaka la kisiasa kufikia chini kuliko wakati wowote. Kwa upande wa Urusi tabaka tawala linalazimu kutumia nguvu ili kubakisha mamlaka yake kwenye utawala.

Ujumbe wetu tukiwa Waislamu unahitaji kuwa hivi, uongozi wa Urusi na uongozi wa Magharibi umewatelekeza watu wao na hivyo hawana haki ya kudai kuwaongoza wengine. Wamagharibi hawawezi kuwa ni kigezo kwa ulimwengu wa Kiislamu na tunahitaji kuchukua hatima yetu mikononi mwetu na tuwe mwanga unaong'aa uwezao kutoa mfumo mbadala kwa ulimwengu chini ya uongozi wa Dola ya Khilafah.

Imeandikwa Kwa Ajili ya Afisi Kuu ya Habari ya Hizb Ut Tahrir na

Adnan Khan

Template Design © Joomla Templates | GavickPro. All rights reserved.