Jumatatu, 11 Dhu al-Hijjah 1445 | 2024/06/17
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

Afisi ya Habari
Wilayah Afghanistan

H.  12 Dhu al-Qi'dah 1445 Na: Afg. 1445 H / 25
M.  Jumatatu, 20 Mei 2024

Taarifa kwa Vyombo vya Habari
Da’wah ya Khilafah ni Wajibu wa Kiislamu kwa Waislamu wote, na Wale Wanaowatesa Wabebaji Dawah hii ni Wahalifu!

(Imetafsiriwa)

Maafisa wa kijasusi wa mkoa wa Herat wamewaweka kizuizini wabebaji Dawah watatu wa Hizb ut Tahrir kwa 'kosa la kulingania Khilafah na umoja wa Ummah' katika mwezi unaoendelea (Mei) wa mwaka huu. Maafisa hao wa ujasusi, walipokuwa wakijaribu kumkamata mmoja wa wabebaji Dawah, wamemzuilia kimakosa kaka yake aliyekuwa akiregea nyumbani kutoka Msikitini. Wakati mbebaji Dawah huyo alipokwenda kwa Idara ya Ujasusi kumwachilia huru kaka yake na kujisalimisha yeye mwenyewe, maafisa wa ujasusi waliwaweka ndugu wote wawili kizuizini, kinyume na kanuni za Sharia na mila za kawaida za nchi. Kimsingi, kwa mtazamo wa Kiislamu na kisheria, mtuhumiwa anapojisalimisha kwa mamlaka, mtu aliyekamatwa kimakosa lazima aachiliwe huru mara moja. Kando na hayo, mbebaji Dawah mwengine alikamatwa alipokuwa akisimamia Tafsiri ya Qur'an katika moja ya Misikiti huko Herat. Kwanza, maafisa wa ujasusi wa Herat waliwapiga waliwachapa na kisha kuwatesa wabebaji Dawah wawili kwa njia ya kuwafunika kitambaa usoni na kuwamwagia maji almaarufu 'waterboarding' huku wakimkosesha pumzi mwengine kwa mfuko wa plastiki.

Tunalaani vitendo hivyo vya unyanyasaji dhidi ya wabebaji Dawah wa Kiislamu kwa maneno makali zaidi na tunachukulia kuwa ni kinyume na kanuni na maadili ya kibinadamu na Sharia. Kwa hakika mateso hayo yamekuwa yakitekelezwa kihistoria katika jela za wavamizi kama vile Abu Ghraib, Guantanamo na Bagram; na kwa bahati mbaya, matendo haya ya kikatili yanaonekana kutumiwa na baadhi ya duara za kijasusi kama kitendo cha kuiga tabia ya yale yanayoitwa magereza ya kinyama.

Je, maafisa wa ujasusi wana hoja gani ya kuwatesa wabebaji Dawah hao? Rai ya kifiqhi ya nyingi ya madhehebu ya Kiislamu yanasisitiza uharamu wa kuwatesa wahalifu, achilia mbali kuteswa kwa wabebaji Dawah. Uongozi wa serikali hii pia umeamuru kwa uwazi kutotumia mateso magerezani. Lakini katika magereza yanayohusiana na idara ya upelelezi, maagizo haya yanakiukwa waziwazi. Je, kwa kufanya vitendo hivyo visivyo vya Kiislamu, ina maana kwamba vyombo vya kijasusi vimegeuka kuwa taasisi ya kiholela au je vimewahi kushikamana na kanuni za Sharia? Kwa sababu wale wanaodai kuwa wanatekeleza Uislamu, imani na Jihad, matendo yao na tabia zao lazima zifungwe na Sharia, sio matamanio ya Nafsi zao.

[إِنَّ الَّذِينَ فَتَنُوا الْمُؤْمِنِينَ وَالْمُؤْمِنَاتِ ثُمَّ لَمْ يَتُوبُوا فَلَهُمْ عَذَابُ جَهَنَّمَوَلَهُمْ عَذَابُ الْحَرِيقِ]

“Hakika walio wafitini Waumini wanaume na Waumini wanawake, kisha hawakutubu, basi watapata adhabu ya Jahannamu na watapata adhabu ya kuungua.” [Al Buruj: 10]

Tunatambua kwamba ndani ya serikali hii na pia ndani ya uongozi wa juu wa Idara ya Ujasusi, kuna maafisa wenye ikhlasi ambao wanapinga mateso kama haya. Lakini kimya chao na kufeli kuwakataza wenzao kufanya maovu hayo kutasaidia kueneza fitna hii kwa upana. Kwa hiyo, wakati wa ghadhabu ya Mwenyezi Mungu (swt), hakuna tofauti itakayokuwa kati ya wenye ikhlasi na wasio na ikhlasi - kila mtu atapatwa na ghadhabu na adhabu ya Mwenyezi Mungu (swt).

[وَاتَّقُوا فِتْنَةً لَا تُصِيبَنَّ الَّذِينَ ظَلَمُوا مِنْكُمْ خَاصَّةً وَاعْلَمُوا أَنَّ اللَّهَ شَدِيدُ الْعِقَابِ]

Na jikingeni na Fitna ambayo haitowasibu walio dhulumu peke yao kati yenu. Na jueni kuwa Mwenyezi Mungu ni Mkali wa kuadhibu.” [Al-Anfal: 25]

Baadhi ya maafisa wa serikali hii wanafikiri kwamba uhai wa utawala unategemea kupiga marufuku vyama na kuwakandamiza wabebaji Dawah wa Kiislamu. Mtazamo na fikra kama hizo sio tu kwamba ni kinyume na hukmu na maadili ya Uislamu, bali pia zitakuwa na matokeo mabaya kwa jamii. Shughuli za pamoja na zenye mwelekeo wa chama ni matukio ya kimaumbile na ya lazima ndani ya jamii yoyote ya binadamu. Historia imeonyesha kuwa jamii zimepata mdororo mkubwa na kudumaa pale walipopiga marufuku ‘vyama, vinavyofanya kazi ya kuamsha watu’. Asia ya Kati, Saudi Arabia na Iran ni mifano ya wazi ya ukatili huu. Katika nchi hizi, licha ya utabikishaji wa sera za chuki dhidi ya Uislamu, serikali hizo zimewasalimisha wananchi kwenye sera zao zisizo halali na zisizo za Kiislamu na hata kuwaondolea ujasiri wa kuamrisha “maruf” hasa kutokana na kukandamizwa kwa shughuli za vyama vya kisiasa.

Kwa kweli, bila ya shughuli za ‘vyama vya mwamko,’ jamii itanyimwa mapambano ya kifikra, kisiasa na kijihadi, na watu watakuwa chambo cha ajenda za wageni. Kwa hakika, ni faradhi kwa Waislamu kupambana kwa pamoja chini ya chama kwa ajili ya kusimamisha Khilafah kwa njia ya Utume. Kwa msingi huu, Hizb ut Tahrir imekuwa ikijitahidi kimataifa kwa lengo la kusimamisha Khilafah ambayo shughuli zake zinaanzia Indonesia hadi Morocco. Magereza na mateso hayataimarisha tu azma thabiti na ustahimilivu wa wabebaji Dawah wake bali pia yataongeza nishati zao kuendeleza wajibu huu kwa shauku isiyoyumba.

Afisi ya Habari ya Hizb ut Tahrir katika Wilayah Afghanistan

Hizb-ut Tahrir: Afisi ya Habari
Wilayah Afghanistan
Address & Website
Tel: 
http://hizb-afghanistan.org/
E-Mail: info@hizb-afghanistan.org

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu