Jumapili, 15 Muharram 1446 | 2024/07/21
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

Afisi ya Habari

H.  10 Dhu al-Hijjah 1444 Na:
M.  Jumatano, 28 Juni 2023

 Pongezi za Idd Al-Adha Al-Mubaraka 1444 H

(Imetafsiriwa)

Allahu Akbar, Allahu Akbar, Allahu Akbar, La Ilaha Ila Allah, Allahu Akbar, Allahu Akbar, Wa Lillahi Alhamd

Bismillahi Ar-Rahman Ar-Rahim. Sifa njema zote ni Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa walimwengu wote, na rehma na amani zimshukie mbora wa Mitume, bwana wetu Muhammad na jamaa zake na maswahaba zake wote.

Hizb ut Tahrir inatoa pongezi za dhati na baraka nyingi kwa Umma wa Kiislamu kwa mnasaba wa Idd al-Adha iliyobarikiwa, ikimwomba Mwenyezi Mungu Mtukufu aifunike kwa siku za furaha, raha na utulivu, na kuuzunguka kwa baraka zake.

Vile vile ninafurahi kutoa pongezi zangu na pongezi za Mkuu wa Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir na ndugu na dada wote wanaofanya kazi katika idara na vitengo vyake kwa Amiri wa Hizb ut Tahrir, mwanachuoni mkubwa Ata Bin Khalil Abu Al-Rashtah, Mwenyezi Mungu amhifadhi, nikimwomba Mola aukirimu Umma wa Kiislamu kwa ushindi na tamkini mikononi mwake.

Umma wa Kiislamu unasherehekea ujio wa Idd al-Adha iliyobarikiwa, kwani ni sherehe inayojumuisha fahamu ya kujitolea muhanga na kutoa ambako Uislamu unapanda katika nyoyo za Waislamu.

Idd al-Adha inatukumbusha sadaka na kujitolea kulikofanywa na mitume na wale waliowafuata kwa ajili ya kuuinua Uislamu. Katika Idd hii iliyobarikiwa, Hizb ut Tahrir inapata fursa ya kuwakumbusha Ummah umuhimu wa maana hizo kuu katika nyakati hizi zenye changamoto.

Katika miaka ya hivi karibuni, changamoto mpya zimeibuka na mashambulizi yanayolenga kitambulisho cha Umma wa Kiislamu.

Baada ya matumaini mapya ya kuregea tena Uislamu katika uhai, haswa kwa matukio ya mapinduzi ya Kiarabu, waandamanaji waliimba, "Kiongozi wetu wa milele, ni bwana wetu Muhammad." Magharibi ilianza majaribio yake ya kuzima matumaini haya katika nyoyo za vijana wa kiume na wa kike wa Ummah. Kwa hivyo, shambulizi la hivi sasa linalotekelezwa na mkoloni Kafiri Magharibi linalenga kudhuru ari ya Waislamu na kujenga hali ya kukata tamaa miongoni mwao kutokana na uwezekano wa kuregea kwa maisha bora ya Kiislamu.

Jambo jipya wakati huu katika shambulizi la Kafiri mkoloni Magharibi ni kwamba ni shambulizi linalolenga kitambulisho cha Kiislamu, lakini si kwa njia ya wazi au ya moja kwa moja, bali kwa kudunisha fahamu za Kiislamu katika nyanja zote za maisha. Ambapo Magharibi inatamani kuvunja utashi wa Ummah na kueneza shaka na mfadhaiko katika nyoyo za Waislamu badala ya kuibua azma yao kwa vitendo vya wazi vya moja kwa moja. Shambulizi hili limedhihirika kwa njia nyingi. Miongoni mwa njia muhimu zaidi ni jaribio la kulazimisha sera ya uhalalishaji mahusiano na umbile la Kiyahudi katika ujumbe uliofichwa ambao madhumuni yake ni kubatilisha fahamu ya jihad ili kuikomboa Ardhi Iliyobarikiwa. Vile vile ilionekana katika juhudi zisizo na kikomo na za kasi za kueneza madhihirisho wa uasherati na upotovu katika ardhi ya Misikiti Miwili Mitukufu (Balad al-Haramain), kwani watawala wa Nyumba ya Saud wako makini kubadilisha sura kutoka kwa Uislamu madhubuti hadi kwa usekula mpotovu, katika juhudi za kuwafahamisha Waislamu juu ya kushindwa kwao kuyahami matukufu yao. Kadhalika, uchochezi wa miungano midogo ya kikabila dhidi ya Umma wa Kiislamu ambao umeishi chini ya bawa lake kwa karne nyingi, kama jaribio la kuondoa hisia za Waislamu kwamba wao ndio mabwana wa nchi na wale wanaohusika na mamlaka yake, usalama na walio ndani yake. Vitendo vyote hivi ni vya kukusudia, na lengo lao ni kuimarisha hali ya kilisekula na kanuni zake, ili kupandikiza ukataji tamaa katika nyoyo za vijana wa Umma wa Kiislamu kutokana na uwezekano wa kuregea kwa Khilafah.

Kuhusiana na hili, msimamo wa Idd al-Adha na mojawapo ya fikra zake kuu kuhusu kujitolea muhanga kwa ajili ya Mwenyezi Mungu na kusimama imara katika njia ya haki, Hizb ut Tahrir inautaka Umma wa Kiislamu, hususan watu wenye ushawishi, kusimama dhidi ya shambulizi hili uchafu huu linaloelekezwa na Magharibi na kutekelezwa na watawala wa Waislamu.

Ama minong’ono ya Shetani ambayo inaihangaisha Magharibi ili kuzuia kuibuka kwa Chemchemi nyingine katika Umma wa Kiislamu, bado ingali inaungulika kila inapowaona watu wa Ummah huu wakizidisha heshima yao kwa Dini yao, na shauku yao ya kutekeleza maisha kamili ya Kiislamu kama ilivyokuwa katika zama za Maswahaba watukufu chini ya Khilafah Rashida. Umma wa Kiislamu unaitazama Magharibi na unaona dhahiri kufeli kwake kuziyeyusha jamii zake, chuki yake ambayo haifichiki tena kwa Uislamu na Waislamu, ulafi wake uliopora mali ya ardhi za Kiislamu na kuharibu uchumi wa dunia nzima, na wazimu wake kwa kule kushindwa kutofautisha kati ya wanawake na wanaume!

Kama ambavyo Umma umejua kwamba Magharibi ndio muungaji mkono mkuu wa watawala wao madhalimu, pia umefikia kutambua upotovu wote wa Magharibi na fahamu yake kuhusu maisha na umeanza kutafuta njia ya tatu, na sio nyengine isipokuwa ni Uislamu ambao unawakilishwa na Khilafah Rashida ya pili kwa njia ya Utume, hata kama Ummah usingetaja suluhisho hili kwa jina halisi, dira yake inaelekeza kwayo katika kila macheo na mtihani.

Mwenyezi Mungu (swt) asema: وَاللهُ مُتِمُّ نُورِهِ وَلَوْ كَرِهَ الْكَافِرُونَ﴿ “Na Mwenyezi Mungu atakamilisha nuru yake ijapo kuwa makafiri watachukia.” [As-Saf: 8].

Hivyo, ni dhahiri kwamba Ummah umeuchagua Uislamu kama uhalisia usioepukika na Khilafah kama mfumo wa utawala.

Rai jumla ya imeundwa na kupata ardhi yenye rutuba ya kuibuka dola ya Kiislamu, na hapa chochote kilichosalia ila kwa watu wenye nguvu na ulinzi katika Ummah kuinusuru. Kwani mabadiliko yananing’inia shingoni mwao, kwa kuwa wana uwezo wa kuyaondoa mamlaka kutoka kwa watawala vibaraka na kuyaregesha kwa Ummah, na haya bila shaka ndiyo mabadiliko ya nafsi ambayo inalazimu mabadiliko kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Mwenyezi Mungu (swt) asema: إِنَّ اللهَ لاَ يُغَيِّرُ مَا بِقَوْمٍ حَتَّى يُغَيِّرُواْ مَا بِأَنفُسِهِمْ﴿. “Hakika Mwenyezi Mungu habadili yaliyoko kwa watu mpaka wabadili wao yaliyomo naf- sini mwao.” [Ar-Ra‘ad: 11].

Basi Mcheni Mwenyezi Mungu! Mcheni Mwenyezi Mungu katika Waislamu, enyi watu wenye nguvu na ulinzi! Mcheni Mwenyezi Mungu katika dunia yenu kabla hamjafunga kurasa zenu ndani yake na mkaiacha ilhali mumemuasi Mwenyezi Mungu na Mtume na walio amini! Tunamuomba Mwenyezi Mungu azijaalie furaha za Idd hii yenye baraka kuwa ndio kiashirio cha siku za ushindi na tamkini. Vile vile tunakuahidini katika Hizb ut Tahrir kwamba tunashikamana na njia ya Utume na tuko imara katika njia ya kazi nzito ya kusimamisha Khilafah. Tunamuomba Mwenyezi Mungu atuongoze sisi na nyinyi katika yale yanayopata ushindi na tamkini yake. Mwenyezi Mungu (swt) asema: إِنَّ اللهَ بَالِغُ أَمْرِهِ قَدْ جَعَلَ اللهُ لِكُلِّ شَيْءٍ قَدْراً﴿ “Hakika Mwenyezi Mungu anatimiza amri yake. Mwenyezi Mungu kajaalia kila kitu na kipimo chake.” [At-Talaq: 3].

Allahu Akbar, Allahu Akbar, Allahu Akbar, La Ilaha Ila Allah… Allahu Akbar, Allahu Akbar, Wa Lillahi Alhamd

Idd Mubarak kwenu, Wa Assalam Alaikum wa Rahmtullahi wa Barakatuh.

Mhandisi Salah Eddine Adada

Mkurugenzi wa Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir

Hizb-ut Tahrir: Afisi ya Habari
Address & Website
Tel: 

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu