Jumatatu, 16 Muharram 1446 | 2024/07/22
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

Afisi ya Habari
Kenya

H.  16 Rabi' I 1438 Na: 1438/03 H
M.  Alhamisi, 15 Disemba 2016

 Taarifa kwa Vyombo vya Habari

Urasilimali Umezigeuza Hospitali kuwa Mapango ya Mauti!

Mgomo unaoendelea wa madaktari na wauguzi sasa unaingia wiki yake ya pili, ukiwaacha wagonjwa wasio na hatia kufariki bila ya huduma katika hospitali zote za umma. Lengo kuu nyuma ya mgomo huu, ni kuilazimisha serikali kutekeleza makubaliano ya 2013 ya kuwalipa madaktari mabaki ya malipo yao pamoja na nyongeza ya asilimia 300 kwa mishahara yao. Chama cha kisiasa cha Kiislamu Hizb ut Tahrir / Kenya, kingependa kufafanua yafuatayo: 

Kuwa sasa ni wazi kama usiku wa mbalamwezi kuwa Kenya imekuwa ni nchi ya migomo miongoni mwa wafanyakazi wa umma. Hali hii ya kusikitisha ni fedheha kwa serikali yoyote inayodai kusimamia hali nzuri ya watu wake; ilhali haijali kuhusu raia wake wenyewe ambao wamezongwa na mzigo wa ushuru; huku ikiwaacha kuteseka katika hospitali za umma kwa kuwanyima haki yao msingi ya matibabu.   

Sekta ya matibabu kama ilivyo sekta nyingine yoyote ya umma katika serikali zote za kirasilimali haisimamiwi kwa uangalifu wa kutosha. Badala yake daima hupuuzwa kwani sio lengo kwa serikali hizi za kirasilimali kusimamia hali nzuri ya watu bali hali nzuri ya kipote fulani tu cha watu wenye ushawishi na matajiri pekee. Hii ndio dhati na uhalisia wa wanasiasa wa kirasilimali katika utawala na upinzani, kila wanapokuwa wagonjwa, hawapotezi muda kusafiri ng'ambo kutafuta matibabu bora na yaliyoendelea! Wakati huo huo hawajali kuhusu hali nzuri ya wafanyakazi, wakiwanyima raia wao madawa. Upande mwingine, wanafuja mabilioni ya pesa za umma kwa ajili ya kampeni za vyama vyao vya kisiasa, ili kuendelea kushinda uchaguzi. Natija yake, hospitali za umma zinakumbwa na uhaba wa madawa na upungufu wa wauguzi.

Tungependa kusisitiza kwa unyenyekevu hapa, urasilimali haugandamizi tu wafanyikazi na vibarua wadogo wadogo pekee, umeenda mbali zaidi kwa kuyafanya manufaa kuwa ndio kipimo pekee cha vitendo vya mwanadamu. Kipimo hiki ndicho kinachofaa kulaumiwa kwa kufanyiwa mnada maisha ya mwanadamu kwa ajili ya mapato ya kifedha. 

Madaktari na wafanyikazi wengineo, bado hata baada ya kuomba mishahara minono, wangali wanaendelea kuomba rushwa kutoka kwa wagonjwa ili kuwapa matibabu mazuri. Hali hii kwa jumla imezigeuza hospitali chini ya minyororo ya nidhamu ya kirasilimali kuwa mtego wa mauti.

Tungependa kusisitiza kuwa matibabu ni mojawapo ya haki msingi kwa umma ambayo yahitaji uangalifu mkubwa na umakini. Huduma hii haipaswi kuchukuliwa kama fadhila; badala yake ni wajibu juu ya serikali kuwapa raia wake. Hivi ndivyo haswa nidhamu ya utawala ya Kiislamu inavyo iangalia kadhia ya matibabu, kupitia kumlazimisha mtawala/Khalifah kusimamia moja kwa moja kazi yake kwani ni mojawapo ya haki za raia. 

Mtume Muhammad (saw) asema:

«الإِمَامُ رَاعٍ وَهُوَ وَمَسْؤُولٌ عَنْ رَعِيَّتِهِ»

“Mtawala ni mchungaji na ataulizwa juu ya raia wake.”

Shabani Mwalimu
Mwakilishi kwa Vyombo vya Habari wa Hizb ut Tahrir Kenya

Hizb-ut Tahrir: Afisi ya Habari
Kenya
Address & Website
Tel:  +254 707458907
E-Mail: [email protected]

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu