Jumatano, 29 Shawwal 1445 | 2024/05/08
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

بسم الله الرحمن الرحيم

Kinyang'anyiro cha Uagizwaji wa Pombe ni Kielelezo cha Maangamizi ya Utalii Zanzibar

(Imetafsiriwa)

Habari:

Mnamo tarehe 04 Aprili 2024 Mahakama Kuu ya Zanzibar ilitupilia mbali Kifungu cha 33(1) cha Sheria ya Kudhibiti Vileo (LCA), ikikiita kifungu hicho ni kinyume cha Katiba. Sheria hiyo iliyopitishwa mwaka 2020, ilipunguza idadi ya kampuni zinazoruhusiwa kuagiza pombe kutoka nje. Kifungu hicho kilidhibiti vibali vya kuingiza vileo viwe kwa ajili ya makampuni yanayomilikiwa na Wazanzibari na kuweka idadi jumla ya makampuni hayo iwe matatu tu.

Maoni:

Uamuzi huu wa mahakama ulikuja kufuatia shauri lililowasilishwa mahakamani na kampuni ya QMB kwamba waliagiza bidhaa ili kuepusha usumbufu kabla ya kibali chao cha awali kumaliza muda, na ombi lao la kukihuisha kibali hicho lilikataliwa. Uamuzi huu wa mahakama ulitengua uamuzi wa Bodi ya Kudhibiti Vileo Zanzibar (ZLCB) wa kutoa leseni kwa makampuni matatu mapya ya kuingiza vileo ambayo ni: Kifaru, Bevko na Zanzi Imports na kuchelewesha kuhuisha vibali kwa waagizaji watatu wa awali- QMB One Stop, Scotch Store na ZMMI.

Lazima ieleweke bayana kwamba uamuzi wa bodi wa kudhibiti waagizaji wa pombe haukutokana na sababu za kulinda maadili au maslahi yoyote ya Ummah, lakini huenda ulitokana na rushwa na ushiriki wa baadhi ya vigogo katika makampuni mapya yaliyopewa vibali kuagiza pombe. Uamuzi huo wa Mahakama unaongeza ushindani katika soko la pombe na uingizaji wake Zanzibar. Unailazimisha Bodi ya Kudhibiti Vileo Zanzibar (ZLCB) kuyapa makampuni mengi zaidi haki ya kuagiza pombe kutoka nje ya nchi. Tukio hili ni dhahiri kuwa inaonyesha taswira ya kusikitisha ya kuzorota kwa maadili na silka njema ndani ya Zanzibar.

Uislamu umekuwa sehemu ya utamaduni wa Zanzibar tangu watu wa visiwa hivi walipoukubali Uislamu kati ya karne ya 7 na 8 Miladi, huku Zanzibar ikiwa na wakaazi Waislamu 99.9%.

Hivyo, ni zaidi ya aibu ya kiwango cha juu kwa serikali ambayo asilimia 99.9 ya wakaazi wake ni Waislamu kujizatiti katika kueneza ulevi unaopelekea uharibifu kwa utamaduni wa Kiislamu ndani ya Zanzibar kwa ajili ya maslahi binafsi tu na kuuvutia utamaduni wa kikoloni wa Kimagharibi kwa jina la utalii.

Zanzibar kama zilivyo biladi nyingine nyingi za Waislamu imebarikiwa kuwa na rasilimali nyingi ikiwemo gesi asilia, kuzungukwa na Bahari ya Hindi nk. lakini imelazimishwa kutegemea sekta ya utalii kama chanzo chake kikuu cha mapato, na umekuwa utalii unachangia asilimia 90 ya mapato ya nje ya visiwa hivyo.

Utalii umekuwa chanzo kikubwa cha mporomoko wa maadili ndani ya Zanzibar, watalii kutoka nchi za Magharibi wamekuwa wakiingiza visiwani humo uchafu na maadili maovu yatokanayo na mfumo wa kibepari kama vile ulevi, matumizi ya dawa za kulevya, ushoga, uasherati, mavazi yasiyo ya staha nk. Kwa kweli utalii umeporomosha maadili ya Kiislamu ya Zanzibar na umekuwa chanzo cha maafa katika ardhi zetu.

Uamuzi wa mahakama unatilia mkazo ukweli wa mtazamo wa kidemokrasia katika nyanja mbili: Kwanza, maadili ya kisekula ni yenye kupuuza mwongozo wa kiungu na badala yake huipa akili dhaifu ya mwanadamu nguvu za kusimamia mambo ya wanadamu.

Pili, serikali za kisekula hazijali ustawi wa watu wao, kutokana na ukweli kwamba pombe inachangia zaidi ya 21.7% ya ajali za barabarani nchini Tanzania, lakini badala ya kufanya juhudi kubwa za kukomesha, uingizaji wake ndio unahamasishwa na kuimarishwa.

Uislamu una suluhisho adhimu na madhubuti kwa kila tatizo la mwanadamu ikiwemo ulevi. Suluhisho la Kiislamu kwa jambo hilo ni rahisi, la kivitendo na la busara. Uislamu unakataza ulevi kwa namna yoyote ile, Mwenyezi Mungu (swt) anasema katika Quran Tukufu:

 [يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُواْ إِنَّمَا الْخَمْرُ وَالْمَيْسِرُ وَالأَنصَابُ وَالأَزْلاَمُ رِجْسٌ مِّنْ عَمَلِ الشَّيْطَانِ فَاجْتَنِبُوهُ لَعَلَّكُمْ تُفْلِحُونَ]

“Enyi mlioamini! Bila ya shaka ulevi, na kamari, na kuabudu masanamu, na kupiga ramli, ni uchafu katika kazi ya shet'ani. Basi jiepusheni navyo, ili mpate kufanikiwa.” [Al Maidah 5: 90]

Kupitia katazo hili, dini, mali, utu na jamii kwa ujumla italindwa kwa ajili ya maslahi mapana ya ustawi wa binadamu.

Imeandikwa kwa Ajili ya Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir na

Said Bitomwa

Mwanachama wa Afisi ya Habari ya Hizb ut Tahrir Tanzania

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

rudi juu

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu