Jumatatu, 25 Rabi' al-thani 1446 | 2024/10/28
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

بسم الله الرحمن الرحيم

Sakata ya Genge la Watoto Wachanga nchini Uturuki

(Imetafsiriwa)

Habari:

Maelezo ya kutisha ya sakata ya “genge la watoto wachanga” nchini Uturuki yametikisa taifa. Watu, wakiwemo madaktari, wauguzi na wafanyikazi wa hospitali, walifanya njama ya uhamishaji watoto wachanga wagonjwa hadi hospitali za kibinafsi kwa pato la kifedha. Angalau watoto 12 walipoteza maisha kutokana na vitendo vya genge hilo, kwani utunzaji muhimu ulipuuzwa kwa ajili ya faida. Kutokana na uhalifu huu wa kutisha uliopangwa, washukiwa 22 kati ya 47 walikamatwa, hospitali 10 za kibinafsi jijini Istanbul zilifungwa, na katika siku zilizofuata, ilifichuliwa kuwa uhalifu huu ulifanyika katika majimbo mengine manne. Baada ya Genge la Watoto Wachanga, sakata ya Genge la Usafishaji Figo (Dialysis) pia iliibuka... Ufisadi katika sekta ya afya ni mauaji yanayotekelezwa na serikali dhidi ya watu wake kwa mikono yake yenyewe.

Maoni:

Dola ya kibepari inaziona huduma muhimu kwa afya ya umma kama “sekta” miongoni mwa sekta za mapato zinazotoa faida kwa uchumi na serikali. Mfumo wa kibepari, ambao unazingatia tu thamani za kimada, ima imepuuza thamani za kibinadamu, kiakhlaki na kiroho chini ya jina la uhuru usio na kikomo au kuzigeuza kuwa njia za mapato. Hivyo, umegeuza huduma ya afya, ambayo inapaswa kuwepo ili kuwaweka watu hai, kuwa chombo cha ukandamizaji badala ya huduma kwa binadamu. Ufisadi huu wa kutisha unaotumia vibaya hospitali, dawa, vifaa tiba, madaktari, wauguzi na wakunga kama ala za kuzalisha pato kwa sekta ya afya, umezaa zimwi la katili anayekula binadamu na hakawii hata kunyonya damu ya watoto wasio na hatia. Huduma ya afya, bila ubaguzi, kamwe haijawahi kuwa ni haki inayopatikana kwa kila mtu katika nchi yoyote ya kibepari.

Umegeuza maadili kama vile ubinadamu, huruma, huduma, kuweka binadamu hai, na kuboresha ubora wa maisha kuwa huduma za kipekee, zilizotengewa wale wanaolipa pesa za kutosha. Ushahidi mwingine, unaothibitisha kuwa huduma za afya ni bidhaa ya kibiashara, ni kwamba huduma za afya, ambazo umma umenyimwa kufaidika kwa usawa, bure na kwa ubora, hutolewa kwa “wateja” wa kigeni kwa njia ya utalii wa kimatibabu. (Kwa mfano, katika robo ya pili ya 2024, zaidi ya watu elfu 800 walikuja Uturuki kupokea huduma za afya, wengi wao kutoka nchi “tajiri” za Magharibi. (Takwimu kutoka USHAŞ). Kwa maana nyengine, huduma bora za afya kwa bei nafuu hutolewa kwa karibu watalii wa afya milioni 3 kila mwaka!)

Genge la watoto wachanga ni sehemu ndogo ya uovu wote unaofanywa na zimwi hili la ubepari ambalo huzalisha uhalifu na ukatili. Siku hadi siku mfumo unaotawala wa kibepari huzalisha uhalifu wa kikatili zaidi na zaidi, mithili ya matukio kutoka kwa filamu za kutisha. Tunaliona hilo kwa upande wa Gaza, ambapo dunia nzima inatazama mauaji ya halaiki kwa ajili tu ya kulinda maslahi ya mabepari wachache. Wakati huo huo idadi na aina ya uhalifu uliofanywa nchini Uturuki ndani ya mwaka mmoja sio tofauti na mazingira ya vita. Wiki 3 tu zilizopita, mhalifu mwenye umri wa miaka 19 aliwaua wasichana wawili katika kuta za Edirnekapı jijini Istanbul. Alimkata kichwa mmoja wa wasichana aliowaua, akatupa kichwa chake chini ya kuta za kihistoria za jiji hadi kwenye miguu ya mama yake, kisha akajiua kwa kuruka kutoka kwa kuta hizo. Siku chache baadaye, mwili wa msichana Narin mwenye umri wa miaka 8, ambaye alikuwa ametoweka kwa siku 19, ulipatikana chini ya mto. Mama yake, kaka yake mkubwa, na ami yake ndio washukiwa wa mauaji hayo. Siku chache zilizopita, mwili wa msichana mwanafunzi wa chuo kikuu Rojin mwenye umri wa miaka 21, ambaye alikuwa ametoweka kwa siku 18, ulipatikana.

Kwa mujibu wa data ya Wizara ya Sheria; mnamo 2021, zaidi ya uhalifu milioni 1.5 ulifanyika dhidi ya kinga ya mwili, pamoja na mauaji, kushambuliwa na kujeruhi. Idadi ya uhalifu unaofanywa dhidi ya mali kama vile wizi, unyang'anyi, uporaji na ulaghai ni karibu milioni 2.5. Mnamo 2021, watu elfu 127 walipeleka mashtaka mahakamani wakidai kudhulumiwa kijinisa. Takriban elfu 45 kati yao ni watoto. Kila siku, malalamishi 123 yanawasilishwa kwa mamlaka za mahakama kwa madai ya unyanyasaji wa kijinsia.

Zaidi ya hayo, takwimu za mahakama zinaonyesha kuwa kuna zaidi ya washukiwa milioni 15 na zaidi ya waathiriwa/walalamishi milioni 10 nchini Uturuki. (T.R. Wizara ya Sheria, Takwimu za Haki, 2021) Ni wazi kwamba takwimu hizi zinaongezeka kila uchao.

Data zote hizi zinaonyesha kuwa watu nchini Uturuki wanaishi katika mazingira yasiyo salama sawa na watu wa Gaza, Palestina au eneo lolote la mizozo duniani. Hakika, hakuna mvua ya mabomu inayonyesha juu ya vichwa vyetu  nchini Uturuki. Miili haijachanwa kwa mabomu, nyumba hazigeuzwi kuwa vifusi, mashamba kuyaunguzwi na mabomu... Lakini uhuru, tamaa ya mali, na ulafi wa mfumo wa kisekula, wa kibepari, wa kidemokrasia unaua wanadamu! Mwili wa mwanadamu - hata kama ni mtoto mchanga - unachukuliwa kuwa aina ya bidhaa, ambazo zinaweza kununuliwa na kuuzwa, kuchanwa kwa tamaa za kingono za kinyama, na kuangamizwa kwa pesa! Nyumba zetu hazigeuzwi kuwa kifusi chini ya mabomu... Kinyume chake, majengo mapya yanajengwa kila siku... Lakini familia zinazoishi humo zimeharibiwa... Mashamba na wanyama wetu hawaunguzwi na mabomu, bali yanafanywa yasiyoweza kutumika - kupitia makubaliano ya kimataifa kama vile makubaliano ya Paris - kwa ajili ya kuwalisha mabepari walafi, kupitia kuharibu kilimo na ufugaji, na hatimaye kuleta maafa makubwa. Nchi inasukumwa katika njaa na kiu hatimaye.

Maadamu tunaendelea kutulia tuli kwa ajili ya watawala hawa vibaraka wa mfumo huu wa kikoloni wa kibepari, waweke imani yao yote katika demokrasia na usekula na miundo yake ya utawala; na maadamu tunaendelea kuwa na matumaini ya kupata kheri yoyote kutoka kwao, maadamu tunaendelea kuomba msaada kutoka kwao, Mwenyezi Mungu (swt) ataendelea kutuma maafa zaidi na zaidi. Ukumbusho mdogo tu kwamba maafa haya kwa hakika ni rehma ya Mola wetu kwetu... Anayatuma haya, si kwa ajili ya kuwaadhibu waja wake waumini, bali kuwaamsha kwa sababu ya rehma zake kwa waja wake walioamini, bali ni kuwaadhibu madhalimu kupitia mikono ya waumini.

Kwa hivyo, ili tuwe miongoni mwa waliookolewa, duniani na kesho akhera, na ili kuondokana mfumo wa unyonyaji damu, unaochukia binadamu wa kibepari, na kukomesha jinai kote duniani, hatuna budi kuweka mtazamo unaohitajika wa Kiislamu kwa wale, ambao wana nguvu juu yetu, haraka iwezekanavyo.

[وَمَا أَصَابَكُم مِّن مُّصِيبَةٍ فَبِمَا كَسَبَتْ أَيْدِيكُمْ] “Na misiba inayo kusibuni ni kwa sababu ya vitendo vya mikono yenu.” [Ash-Shura 30]

Kwa kuwa tayari tumehukumiwa kuishi katika mazingira ya vita, kwa kuwa maisha yetu wala ya watoto wetu tunaowapenda sio salama kuliko maisha yetu, wala mali zetu, heshima yetu, dini yetu, au imani yetu, basi hatuna budi kupambana mithili ya mujahidina katika vita na kufanya kazi kwa bidii kubadilisha mazingira haya. Kwa sababu hii, ni lazima tujitahidi ima kuwarekebisha watawala wetu au kuwabadilisha. Rasulullah (saw) amesema,

«أَفْضَلُ الْجِهَادِ كَلِمَةُ حَقٍّ عِنْدَ سُلْطَانٍ جَائِرٍ»

“Jihad (kupigana katika njia ya Mwenyezi Mungu) ni kusema neno la haki mbele ya mtawala jeuri.” [Abu Daoud].

[يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُواْ اسْتَجِيبُواْ لِلّهِ وَلِلرَّسُولِ إِذَا دَعَاكُم لِمَا يُحْيِيكُمْ وَاعْلَمُواْ أَنَّ اللّهَ يَحُولُ بَيْنَ الْمَرْءِ وَقَلْبِهِ وَأَنَّهُ إِلَيْهِ تُحْشَرُونَ]

“Enyi mlio amini! Muitikieni Mwenyezi Mungu na Mtume anapo kuitieni jambo la kukupeni uzima wa milele. Na jueni kuwa Mwenyezi Mungu huingia kati ya mtu na moyo wake, na kwamba hakika kwake Yeye tu mtakusanywa.” [Al-Anfal 24]

Imeandikwa kwa Ajili ya Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir na
Zehra Malik

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

rudi juu

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu