Jumamosi, 21 Muharram 1446 | 2024/07/27
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

بسم الله الرحمن الرحيم

 Vipi Khilafah Itakavyo Wadhamini Wanawake Haki Zao za Kielimu

Uislamu hutazama utafutaji elimu ya Kiislamu kuwa faradhi kwa wanawake na wanaume.

Mtume (saw) amesema, «طَلَبُ الْعِلْمِ فَرِيضَةٌ عَلَى كُلِّ مُسْلِمٍ» “Utafutaji elimu ni faradhi kwa kila Muislamu.” [Ibn Majah]

Kutilia maana hali ya juu kwa Mtume (saw) umuhimu wa elimu ya wanawake kumeashiriwa na usomi wa wengi wa wakeze, maswahaba wa kike wa Mtume (saw) (Sahabiyyat), na wanawake wengineo katika zama za utawala wake mjini Madina.

Aisha mke wa Mtume (saw) alipata lakabu ya ‘Faqihi wa kike wa Ummah’ (Faqihat ul Ummah) kutokana na elimu yake ya Hadith na ujuzi katika fiqh ya Kiislamu. Alisimulia zaidi ya Hadith 2200 kutoka kwa Mtume (saw). Aisha (ra) pia alikuwa mwanachuoni mkubwa wa utabibu, fasihi na mashairi.

Mtume (saw) angewafunza wanaume na wanawake kuhusu Uislamu msikitini na katika mijumuiko mingine ya umma. Vilevile alitenga siku moja kila wiki kuwaelimisha wanawake pekee kuhusu Dini yao. Mtume (saw) pia aliweka umuhimu juu ya wanawake kujua kusoma na kuandika, unaoashiriwa katika agizo lake kwa Shifa bint Abdullah la kumfundisha mkewe Hafswa jinsi ya kuandika.

Abu Sa’id al-Khudri (ra) ameripoti kuwa baadhi ya wanawake walimwambia Mtume (saw),

قَالَتِ النِّسَاءُ لِلنَّبِيِّ صلى الله عليه وسلم غَلَبَنَا عَلَيْكَ الرِّجَالُ، فَاجْعَلْ لَنَا يَوْمًا مِنْ نَفْسِكَ‏.‏ «فَوَعَدَهُنَّ يَوْمًا لَقِيَهُنَّ فِيهِ، فَوَعَظَهُنَّ وَأَمَرَهُنَّ»

“Wanaume wametushinda (katika kupata elimu). Basi tujaaliye nasi siku yako moja ili nasi tufaidike vilevile. Mtume (saw) akaweka miadi nao siku moja ambayo angekutana nao, na angewapa mawaidha na kuwaelimisha kuhusu amri za Mwenyezi Mungu (swt).” [Al-Bukhari]

Uislamu pia unawashajiisha wanaume na wanawake kuusoma ulimwengu unaowazunguka na kuleta manufaa kwa wanadamu katika nyanja zote – ikiwemo sayansi, utabibu, viwanda na teknolojia.

Ni utiliaji maanani huu mkubwa wa Uislamu kwa utafutaji elimu ya Kiislamu na aina nyenginezo za elimu unaoweka msingi kwa Khilafah kutambua umuhimu wa elimu ya wanawake.

Mtume (saw) asema,

«وَمَنْ سَلَكَ طَرِيقًا يَلْتَمِسُ فِيهِ عِلْمًا سَهَّلَ اللَّهُ لَهُ بِهِ طَرِيقًا إِلَى الْجَنَّةِ» “Na mwenye kufuata njia katika kuitafuta elimu Mwenyezi Mungu humsahilishia kwa hilo njia ya kwenda Peponi.” [Muslim]

Khilafah huitazama elimu kama haki msingi kwa kila mtu binafsi na vilevile dharura kwa maendeleo ya kijamii na kimada katika mujtama wowote. Imewajibishwa kutoa elimu bila malipo katika viwango vya msingi na upili kwa wavulana na wasichana. Hii hujumuisha masomo kama fanni za Kiislamu, Lugha ya Kiarabu, hesabu, na sayansi za utafiti kama bayolojia, kemia na fizikia. Dola pia itajizatiti kufadhili elimu ya juu bila malipo kwa wanaume na wanawake kwa kadri ya uwezo wake.

“Ni jukumu la Dola kumfundisha kila mtu, mwanamume au mwanamke, vile vitu ambavyo ni muhimu katika maisha ya kawaida. Hii yapaswa kuwa wajibu na kutolewa bila malipo katika viwango vya elimu ya msingi na upili.” (Kifungu cha 178 cha Kielelezo cha Katiba ya Al-Khilafah cha Hizb ut Tahrir)

Ufundishaji wanafunzi wa kiume na wa kike katika shule za dola na za kibinafsi utakuwa kando kando.

Chini ya Khilafah, wavulana na wasichana, wanaume na wanawake wana haki sawa za kielimu. Ubaguzi wowote wa kijinsia au wa raia wake yeyote katika kupata elimu bora umeharamishwa. Fauka ya hayo, wanawake kama ilivyo kwa wanaume wanahitaji kupata elimu ya Kiislamu inayohitajika kuhusiana na maisha ya kisiasa, kiuchumi na kijamii pamoja na mambo mengine ili waweze kutimiza majukumu yao ya Kiislamu, kujihusisha na amali kadha wa kadha za kimujtama na vitendo ambavyo Uislamu umeviruhusu, na kujifunga na hukmu za Kiislamu kama Waislamu na kama raia wa dola. Hivyo basi Khilafah itawajibika kupangilia nidhamu yake ya kielimu ili kuwapa wasichana na wanawake elimu kama hiyo na pia kujizatiti kuondoa taasubi zozote za kimila au vizingiti vya kitamaduni vinavyo dunisha elimu ya wanawake au kuwazuia wasichana kutokana na kutafuta haki zao za kielimu.

“Wanawake wana haki na majukumu sawa kama wanaume, isipokuwa yale yaliyo fafanuliwa na dalili za Kisheria kuwa ya kiume na ya kike. Hivyo basi, mwanamke ana haki ya kufanya biashara, ukulima, na viwanda; kushiriki katika mikataba na miamala; kumiliki aina zote za mali; kuwekeza utajiri wake ima kibinafsi au kupitia wakala, na kutekeleza kibinafsi mambo yote ya kimaisha.” (Kifungu cha 114 cha Kielelezo cha Katiba ya Al-Khilafah cha Hizb ut Tahrir)

Daima dola itajizatiti kuwa dola inayo ongoza duniani katika sayansi, utabibu; teknolojia, viwanda na nyanja nyinginezo kama inavyo wajibishwa na Uislamu, utaisukuma ili kutafuta ubora katika elimu. Hivyo basi itawashajiisha wanawake kuingia katika masomo ya juu na kuwarahisishia katika uteuzi wa taaluma katika nyanja tofauti tofauti, ikiwemo fanni za Kiislamu, utabibu, sayansi, lugha na uhandisi. Yote haya yataimarisha matarajio ya kielimu ya wasichana na wanawake.

Ni wajib juu ya Khilafah kutoa elimu na huduma za matibabu bora zaidi iwezekanavyo kwa raia wake, kwani Mwenyezi Mungu (swt) ameisifu elimu kuwa ‘Msimamizi’ na ‘Mchungaji’ wa watu. Hivyo basi ipo haja ya kuwa na madaktari, wauguzi na walimu wa kike wa kutosha ili kutimiza dori hizi.

Ni katika mazingira haya ya masomo yaliyo wekwa kupitia utabikishaji wa nidhamu ya Kiislamu ndiyo yaliyo hakikisha kuwa elimu ya wanawake imenawiri chini ya Khilafah iliyopita kama itakavyo fanya tena Khilafah inayokuja InshaAllah.

“Mohammed Akram (mwanachuoni wa Kiislamu wa Kihindi wa zama hizi) alianza miaka minane iliyopita kuandika kamusi ya mjaladi mmoja ya wasifu wa maisha ya wanachuoni wa kike wa Hadith, mradi uliomfanya kupekua kamusi za wasifu, vitabu vya kale, rekodi na barua za madrasa kwa ajili ya kupata vyanzo stahiki. ‘Nilidhani labda ningepata wanawake 20 au 30,’ alisema. Mpaka kufikia sasa, amepata wanawake 8,000, kutokea miaka 1,400 iliyopita, na kamusi yake sasa imefikia mijaladi 40 …” (Kipande hiki kimevuliwa kutoka Makala “A Secret History” yaliyo andikwa na Carla Power yaliyo chapishwa katika Jarida la New York, Februari 25, 2007)

Mifano ya wanawake waliofaulu katika nyanja tofauti tofauti za masomo chini ya Khilafah:

Lubna wa Andalus (karne ya 10 Miladi) – Malenga aliye bobea katika nahau, balagha, hesabu na uandishi. Alikuwa mmoja wa waandishi wa dola na aliaminiwa na uandishi wa barua rasmi.

Fakhr al-Nisa Umm Muhammad Shuhdah (karne ya 12 Miladi) – Mtaalamu katika uandishi. Alikuwa akimuandikia Khalifah al-Muqtafi. Yasemekana kuwa katika wakati wake hakukuwa na mtu yeyote mjini Baghdad aliye lingana naye katika ubobeaji wake wa uandishi.

Mpasuaji wa Kituruki wa karne ya 15 Serefeddin Sabuncuoglu amewasifu wapasuaji wa kike mjini Anatolia kutekeleza taratibu za upasuaji kwa wangonjwa wa kike.

Labana wa Kurtuba (karne ya 10 Miladi) – Mjuzi katika hesabu na fasihi. Alikuwa na uwezo wa kutatua hesabu ngumu kabisa za kijometriki na aljebra. Elimu yake pana ya fasihi jumla ilimpa ajira ya kuwa katibu wa Khalifah, al-Hakem II.

Maeriam “al-Astrolabiya” Al-Ijilya (karne ya 10 Miladi) – Mwanasayansi, mvumbuzi, mnajimu na muundaji wa vifaa vinavyotumika kutathmini kisimamo cha jua na sayari. Miundo yake ilikuwa na ubunifu sana kiasi cha kuajiriwa na mtawala wa mji alimoishi.

Zaynab kutoka kabila la Banu Awd (karne ya 10 Miladi) – Mjuzi katika utabibu, hususan katika kutibu vidonda na matatizo ya macho.

Imeandikwa kwa Ajili ya Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir na
Dkt. Nazreen Nawaz
Mkurugenzi wa Kitengo cha Wanawake katika Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir

Imebadilishwa mara ya mwisho mnamoJumapili, 26 Aprili 2020 10:37

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

rudi juu

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu