Jumamosi, 21 Muharram 1446 | 2024/07/27
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

بسم الله الرحمن الرحيم

 «يَا مَعْشَرَ الشَّبَابِ، مَنِ اسْتَطَاعَ مِنْكُمُ البَاءَةَ فَلْيَتَزَوَّجْ»

“Enyi Mabarobaro! Yeyote Mwenye Uwezo Miongoni Mwenu Basi na Aoe”

(Imetafsiriwa)

Allah (swt) aliwaumba wanadamu na kuifanya ndoa kuwa njia ya kuongeza kizazi; Allah (swt) aliita ndoa katika Quran “ahadi madhubuti” ili kuashiria umuhimu wake.

وَأَخَذْنَ مِنكُم مِّيثَاقًا غَلِيظًا﴿ “… na wao wanawake wamechukua kwenu ahadi iliyo madhubuti?” [An-Nisa’: 21]

Mtume (saw) alimkemea kila yule anayekataa kuoa kwa sababu yoyote ile, hata kama sababu hii ni Qiyam ul-Layl (kusimama usiku kwa ajili ya ibada) au kufunga. Mtume (saw) amesema:

«...وأَتَزَوَّجُ النّساء، فَمَنْ رَغِبَ عَنْ سُنَّتِي فَلَيْسَ مِنِّي»“…na mimi naoa wanawake, basi yeyote anaye kwenda kinyume na Sunnah yangu si katika mimi.”

Imam Ahmad (Rahimahullah) amesema: “Kukataa kuoa si katika Uislamu, yeyote anaye kushauri usioe; amekulingania kwa chengine kisichokuwa Uislamu”.

Kuzembea katika kuoa ni kinyume na Sunnah, na kinyume na umbile asili; na mlango wa kueneza ufisadi na uchafu, na maovu, Allah utuepushe. Kujiweka mbali na ndoa pasi na sababu halali hupunguza wasiwasi na kutoridhika, kwa sababu ndoa huleta utulivu, amani, kujali na mapenzi.

وَمِنْ آيَاتِهِ أَنْ خَلَقَ لَكُمْ مِنْ أَنْفُسِكُمْ أَزْوَاجًا لِتَسْكُنُوا إِلَيْهَا وَجَعَلَ بَيْنَكُمْ مَوَدَّةً وَرَحْمَةً إِنَّ فِي ذَلِكَ لَآيَاتٍ لِقَوْمٍ يَتَفَكَّرُونَ﴿

“Na katika Ishara zake ni kuwa amekuumbieni wake zenu kutokana na nafsi zenu ili mupate utulivu kwao. Na amejaalia mapenzi na huruma baina yenu. Hakika katika haya bila ya shaka zipo Ishara kwa wanao fikiri.” [Ar-Rum: 21]

Ndoa hukubaliana na umbile la mwanadamu na huhakikisha kuendelea kubakia kwa wanadamu, urithi duniani, kuongezeka kwa vizazi, na ufanisi katika ardhi; hutimiza ahadi ya Mtume (saw) ya kuongezeka kwa idadi ya uzaanaji (wa Umma huu) mbele ya mataifa mengine siku ya Qiyama.

Lakini tunapouangalia Ulimwengu wa Kiislamu, tunaona idadi kubwa ya wanawake na wanaume wadogo ambao hawako ndoani, na utafiti wa hivi majuzi waonyesha kuwa thuluthi moja ya idadi ya wanawake wadogo ambao hawajaolewa katika biladi za Kiarabu wamefikia umri wa miaka 30. Kwa mfano, asilimia ya wanaume ambao hawajaoa nchini Misri wa kati ya umri wa miaka 18 na 29 ilikuwa takriban asilimia 37.4 ya idadi jumla ya watu, ikilinganishwa na asilimia 16.4 ya wanawake katika sensa ya 2017, kwa mujibu wa takwimu ya sensa ya Misri. Kwa mujibu wa baadhi ya takwimu, Palestina ilipata asilimia ya chini kabisa ya asilimia 7, Bahrain asilimia 25, Yemen asilimia 30, Kuwait, Qatar na Libya asilimia 35, Misri na Morocco asilimia 40, Saudi Arabia na Jordan asilimia 45, Algeria asilimia 51, Tunisia asilimia 65, Iraq na Syria asilimia 70, Imarati asilimia 75, huku Lebanon ikirekodi asilimia kubwa zaidi ikifika asilimia 85. (Albawaba

Asilimia hizi kubwa si za kuridhisha, zinazopelekea maovu, fitna na kupotoka, yanayoathiri familia na mujtamaa. Na hawa vijana wadogo hudhani kuwa wanaishi maisha ya utulivu kando na matatizo ya kifamilia na kwamba maisha yao yako huru na hofu na matatizo ya kifamilia, lakini wamekosea kwa sababu ikiwa watajizuia nafsiya zao, wataishi kwa fadhaiko, wasiwasi na kuteseka kwa maisha ya uchungu na watanyimwa starehe ya ndoa na neema ya watoto ambayo ni neema kubwa zaidi ambayo Allah amewapa wanadamu. Ikiwa hawatajizuia nafsiya zao, watageukia haramu na madhambi, kuachana na Dini, maadili mema, na usafi wa tabia. 

Kwa sababu hii, sababu za kucheleweshwa kwa ndoa au kujiepusha nayo zinapaswa kuangaliwa kwa makini ili kuondoa vikwazo hivyo na kuwasahilishia hili vijana wa kiume na wa kike. Vyenginevyo, Haram itabadilishwa kuwa Halal, na ufisadi, zinaa na madhambi yataenea katika familia na mujtamaa, na Umma utawekwa mbali na mwamko na kurudi tena kwa Uislamu; katiba, njia na dola yake.  

Ikiwa tutaangalia sababu za kucheleweshwa kwa ndoa, tutaona kuwa wakati mwengine zinatofautiana kutoka nchi moja hadi nyengine, lakini asili yake ni moja nayo ni kutotekelezwa kwa hukmu za kisheria, miongoni mwa sababu hizi kubwa ni:

Gharama kubwa ya mahari na gharama kubwa ya ndoa katika mambo yasiyo na umuhimu, yanaifanya ndoa kuwa ngumu au kukaribia kutowezekana kwa vijana wengi nayo hupelekea kuichelewesha, au hugeuka kuwaoa wanawake wa kigeni ambao haiwagharimu wao chochote, ambapo huongeza idadi ya wanawake ambao hawajaolewa. Hili ni kinyume na lile ambalo Allah amelipanga ili kurahisisha gharama za ndoa. Mtume (saw) amesema,

«أَعَظَمُ النِّسَاءِ بَرَكَةً أَيْسَرُهُنَّ مَئُونَةً» “Wanawake wenye Baraka nyingi zaidi ni wale walio na mahari ya chini kabisa.”

Hii ni bila ya kutaja masharti mengi na matakwa ya kimada ya vijana wa kike na familia zao, na kutilia maanani upande wa kimada katika uchaguzi wa mume na kutotilia maanani sifa nyenginezo muhimu kama Dini, tabia na uwezo. Ash-Shari’ alisisitiza kuangalia sifa mbili kuu katika mume. Mtume (saw) amesema:

«إِذَا أَتَاكُمْ مَنْ تَرْضَوْنَ دِينَهُ وَخُلُقَهُ فَزَوِّجُوهُ إِلَّا تَفْعَلُوا تَكُنْ فِتْنَةُ فِي الأَرْضِ وَفَسَادٌ كَبِيرٌ»“Atakapo wajilieni yule ambaye mumeridhia Dini na akhlaqi yake basi muozeni! Ikiwa hamutafanya hivyo kutakuweko na fitna katika ardhi na ufisadi mkubwa” [Tirmidhi]

 Hapana shaka kuwa Allah amedhamini kuwasaidia waja wake waumini ili waowane, Mtume (saw) amesema:

«ثَلَاثَةٌ حُقَّ عَلَى اللهِ عَوْنُهُمْ: الْمُجَاهِدُ فِي سَبِيلِ اللهِ وَالْمُكَاتِبُ الَّذِي يُرِيدُ الأَدَاءَ وَالنَّاكِحُ الَّذِي يُرِيدُ الْعَفَافَ»“Watu watatu Allah ni haki awasaidie: anayepigana Jihad katika njia ya Allah, na mtumwa ambaye anataka kujikomboa, na yeyote anayetaka kuhifadhi nafsiya yake kwa ndoa.” [Tirmidhi]

Inashangaza sana kumpata mtu amemuozesha binti yake kwa mtu asiye swali na asiye muogopa Mola wake, kwa ajili ya mali yake na wingi wa pesa zake na kumkataa mtu mwema kwa ajili ya umasikini wake!!

Tatizo hili linachochewa zaidi na kukosekana dola ya Kiislamu ambayo ingechunga mambo ya watu, na kwa mfumo wa kirasilimali ambao tunaishi ndani yake, kama vile kuenea kwa ukosefu wa ajira, mapato ya chini, kuenea pakubwa kwa ufisadi na ubaguzi wa kikabila, ambayo huwafanya wale wanaotaka kuoa kushindwa kuanzisha maisha ya familia. 

Miongoni mwa vigezo muhimu vinavyozuia ndoa na kuichelewesha kwa vijana wengi wa kiume na wa kike ni athari ya vyombo fisidifu vya habari vinavyo ongozwa na kushawishiwa na fahamu za Kimagharibi, fikra zake msingi, miondoko ya kijamii, fikra na mitazamo iliyo mbali na sheria za Uislamu; ambayo husambazwa kwa watoto wa Kiislamu kupitia katika musalsala tofauti tofauti, filamu na vipindi. Hii ni ikiongezewa na udhaifu wao katika kushikamana na dini na kukosekana kwa sheria na mipaka katika nidhamu hii inayopelekea kuporomoka kwa maadili na akhlaqi, na uwazi usio na mipaka. Hivyo basi, baadhi wameanzisha mahusiano haramu na kutafuta matakwa yaliyo haramishwa na ndoto hadaifu na mangati ya mapenzi feki na haja ya wapenzi kuwa na uhusiano kabla ya ndoa ili wajuane!! Hii ni mojawapo ya fitna kubwa, Allah atuhifadhi, au hamu yao ya uhuru na wala sio kutenda kwa uwajibikaji au kukinai kwengine kiakili kusiko kuwa na dalili katika sheria na kusikopaswa kutegemewa.

Kutokana na kanuni zilizotungwa na kibinadamu za kirasilimali katika biladi za Kiislamu, ambazo zinatawaliwa kwa manufaa na maslahi, na ambapo mahusiano ya kifamilia na ulezi sahihi na mafungamano ya kifamilia yameyeyuka, idadi ya wanawake wadogo huhisi kutishika na hofu ya mustakbali. Hivyo basi, kwa mujibu wao watatafuta silaha ya kulinda mustakbali wao; nayo ni elimu na kazi, hata kama itagongana na ndoa yao na cheo chao cha mama. Lau hukmu za Kiislamu zingetekelezwa, hawange hisi hivi kwa sababu Uislamu unadhamini ulinzi, uangalizi na usalama wao katika dori zao zote maishani. Pia ni lazima tusisahau hadaa ya usawa na uwezo wa kiuchumi, inayo wafanya wanawake kufikiria uhuru na kutafuta mafanikio na shakhsiya yao ya kibinafsi kupitia kutafuta umaarufu katika mujtamaa, na hivyo basi fikra ya tabaka na usawa wa kitamaduni kuibuka kati ya wanandoa na kuwa kipimo cha wanawake kukitumia kuchagua mtu wa kuolewa naye, huenda kisipatikane, na kupelekea kucheleweshwa kwa ndoa au kutooa kabisa. Wakati mwengine familia ndio sababu ya kuchelewa kwa ndoa ya binti yao au kutekeleza “Al Adhl” (kuzuia mabinti kuolewa) ili kufikia matakwa yao na kunufaika kimada. 

Ili kutatua tatizo au kupunguza athari yake ni lazima tuondoe sababu zake, ni lazima tuanze kusisitiza umuhimu wa ndoa na udharura wake kwa vijana wa kiume na wa kike, na ni lazima tuonyeshe hatari za kuepukana na ndoa au kuifanya kuwa ngumu. Na kisha ni lazima tufanye kazi ili kusahilisha ndoa kupitia yafuatayo:

Kupunguza gharama za ndoa, kupunguza mahari, kupunguza matakwa ya ndoa, na kuwakubali wale tuliowakinai Dini na akhlaqi zao, hata kama wanapesa kidogo, na kwa kuzingatia maneno ya Allah (swt):

وَأَنْكِحُوا الْأَيَامَى مِنْكُمْ وَالصَّالِحِينَ مِنْ عِبَادِكُمْ وَإِمَائِكُمْ إِنْ يَكُونُوا فُقَرَاءَ يُغْنِهِمُ اللَّهُ مِنْ فَضْلِهِ وَاللَّهُ وَاسِعٌ عَلِيمٌ﴿

“Na waozeni wajane miongoni mwenu na wema miongoni mwa watumwa wenu na wajakazi wenu. Wakiwa mafukara Allah atawatajirisha kwa fadhila zake. Na Allah ni Mwenye wasaa na Mjuzi.” [An-Nur: 32]. Na Hadith ya Mtume (saw):

«إِنَّ مِنْ يُمْنِ الْمَرْأَةِ تَيْسِيرَ خِطْبَتِهَا، وَتَيْسِيرَ صَدَاقِهَا، وَتَيْسِيرَ رَحِمِهَا» “Hakika katika Baraka ya mwanamke: ni wepesi wa posa yake, na wepesi wa mahari yake, na wepesi wa kizazi chake (kushika mimba na kuzaa kwake).”

Na katika maneno ya Umar (ra) amesema: “Musiongeze mahari ya wanawake, lau kama ingekuwa ndio utukufu wa Dunia na Akhera au ingekuwa ni uchaMungu wa Akhera basi Mtume wa Allah angestahiki zaidi hilo kuliko nyinyi (lakini Yeye (saw) hakuongeza mahari).” [Imesimuliwa na wapokezi watano na kuthibitishwa na Tirmidhi]

Na sisi twamwambia yule anayemzuia binti yake au dadake kuolewa, kutokana na tamaa ya pesa au kazi yake, licha ya kupata posa kutoka kwa mwanamume mwema na kukubali kwao posa hiyo: kwamba hili limeharamishwa na sheria. Allah (swt) asema:

فَلاَ تَعْضُلُوهُنَّ أَن يَنكِحْنَ أَزْوَاجَهُنَّ إِذَا تَرَاضَوْاْ بَيْنَهُم بِالْمَعْرُوفِ﴿ “…basi musiwazuie kuolewa na waume zao (watalaka wao) endapo baina yao wamekubaliana kwa wema” [Al-Baqara: 232].

Ama kuhusu vijana waliozembea katika ndoa kwa sababu ya fikra na fahamu potofu ambazo ziko mbali na Uislamu, tunawaambia: Muogopeni Allah na mujue kuwa wakati unapita na matamanio yanamalizika na kujilaumu na huzuni pekee ndio zitasalia, na utulivu na amani zitakuja pekee kupitia kuoa mwanamke mwema au mume mwema.

وَمِنْ آيَاتِهِ أَنْ خَلَقَ لَكُمْ مِنْ أَنْفُسِكُمْ أَزْوَاجًا لِتَسْكُنُوا إِلَيْهَا وَجَعَلَ بَيْنَكُمْ مَوَدَّةً وَرَحْمَةً إِنَّ فِي ذَلِكَ لَآيَاتٍ لِقَوْمٍ يَتَفَكَّرُونَ﴿

“Na katika Ishara zake ni kuwa amekuumbieni wake zenu kutokana na nafsi zenu ili mupate utulivu kwao. Na amejaalia mapenzi na huruma baina yenu. Hakika katika haya bila ya shaka zipo Ishara kwa wanao fikiri.” [Ar-Rum: 21]

Na wala musiige kile mukionacho katika musalsala na vipindi haribifu vilivyojaa fahamu na suluki fisidifu zilizo mbali na Dini, akhlaqi na maadili yenu, ambavyo vimeletwa kwetu ili kutufisidi, kwa sababu wanaogopa kurudi tena kukubwa kwa Uislamu kama ulivyokuwa wakati wa zama za kuwepo dola yake imara.

Ama kwa wewe, binti yangu na dadangu, unapaswa kumkubali mume anayemridhisha Allah na Mtume wake, na wala usifadhilishe asiyekuwa na uwezo kwa mwenye uwezo kwa ajili ya pesa au jina au cheo unachokitaka, au kwa fadhila unazozitaka, au kwa matarajio ya kidunia, ili upate Baraka za Allah. Vilevile, masomo au kazi yako si muhimu kuliko ndoa yako na cheo chako cha mama, na hakuna mgongano baina ya hayo, ikiwa utaweza kuweka mizani kati ya hayo. Dori yako ya kwanza katika maisha haya ni kuwa mama na mke nyumbani, na kutafuta pato ni jukumu la mwanamume (mume). Ni lazima atimize mahitaji yako yote. Hili halipunguzi cheo na hadhi yako, bali kinyume chake, hii ni dori yako na Wallahi ni dori muhimu sana, na miongoni mwa majukumu magumu ambayo wanaume hawawezi kuyafanya, ni kumjenga mwanadamu, nyumba yako na familia yako haviwezi kufidiwa na cheti au kazi au chochote.   

Hapa tungependa pia kuzindua kuhusu hukmu ya kisheria kuwa kukosekana kwake kumepelekea ongezeko la idadi ya wanawake ambao hawajaolewa. Hukmu hii iliharibiwa kwa musalsala, filamu uandishi duni wa waandishi duni wa kiume na wa kike; hii ni familia ya wake wengi, ambayo ni hukmu ya sheria kutokana na hukmu za Allah na kutokana na Sunnah ya Mtume (saw), ambayo ni suluhisho zuri la ongezeko la idadi ya wanawake ambao hawajaolewa, twahitaji kufafanua sheria hii. Vilevile mwenye wake wengi ni lazima amche Allah na kuhakikisha uadilifu, kilicho haribu sheria ya wake wengi ni kukosa uadilifu kwa wenye wake wengi. Wengi wao huegemea kwa baadhi ya wanawake (wake) na watoto wao kwa gharama ya wanawake (wake) wengine na watoto wao, hili liliwafanya wanawake kuchukia uke wenza na wengine wengi wanaogopa hili kwa nafsi zao na binti zao. Baadhi yao wafadhilisha kubaki bila ya kuolewa kuliko kuolewa na mtu mwenye wake ambaye huenda akakosa uadilifu kwake au kwa mke mwengine kwa sababu yake kwa kuhisi kuwa dhambi.  

Na tunatamatisha kwa maneno ya Mtume (saw):

«يَا مَعْشَرَ الشَّبَابِ، مَنِ اسْتَطَاعَ مِنْكُمُ البَاءَةَ فَلْيَتَزَوَّجْ، فَإِنَّهُ أَغَضُّ لِلْبَصَرِ وَأَحْصَنُ لِلْفَرْجِ، وَمَنْ لَمْ يَسْتَطِعْ فَعَلَيْهِ بِالصَّوْمِ، فَإِنَّهُ لَهُ وِجَاءٌ»

Enyi Mabarobaro! Yeyote Mwenye Uwezo Miongoni Mwenu Basi na Aoe, kwani hakika yake ni huziba macho na kuhifadhi tupu (kutokana na zinaa), na ambaye hana uwezo basi ni juu yake kufunga, kwani hakika saumu ni kinga kwake.”

Imeandikwa kwa Ajili ya Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir na

Muslimah Ash-Shami (Umm Suhaib)

Imebadilishwa mara ya mwisho mnamoJumapili, 12 Aprili 2020 07:15

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

rudi juu

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu