Jumapili, 15 Muharram 1446 | 2024/07/21
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

بسم الله الرحمن الرحيم

Viongozi wa Kidini na Sakata la Mkataba wa DP World Tanzania

(Imetafsiriwa)

Habari:

Mnamo Juni 10, 2023, Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania liliidhinisha makubaliano kati ya serikali Tanzania na Dubai ambayo yataruhusu kampuni ya kimataifa ya Dubai ya DP World kuendesha bandari za Tanzania, hususan bandari ya jiji la Dar es Salaam.

Maoni:

Makubaliano hayo yaliibua maoni tofauti kwa watu jumla, ambapo wanaounga mkono mkataba huu ambao wengi wao ni chama tawala na wafuasi wake wanautaja kuwa ni mkataba bora, huku wanaopinga mkataba huu ambao wengi wao ni upinzani na wafuasi wao wakiutaja mkataba huu kuwa ni mbaya usiofaa.

Mjadala huu pia uliwaibua baadhi ya viongozi wa dini ambao wameibuka na kukosoa makubaliano haya, kama vile Askofu Mstaafu wa Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Polycarp Kadinali Pengo, wakati akihojiwa na chaneli ya YouTube ya Baraza la Maaskofu wa Kanisa Katoliki Tanzania, alisema: “Mtanzania akishindwa huwezi kumtupa na kusema unaweza kupata fedha nyingi kwa kumleta mgeni” (Mwananchi 18/06/2023)

Kusema kwamba viongozi wa Kikristo wanajali maslahi ya umma na ustawi wa watu si kweli, kwa mfano, Bwana Pengo wakati wa utawala uliopita wa Raisi John Magufuli ambapo watu wengi walikuwa wakiuawa, kuteswa, kufungwa jela na kuwekwa kizuizini kwa kubambikiwa kesi, si tu kuwa hakujali, bali alikuwa muungaji mkono na mfuasi mkubwa wa utawala wa Magufuli kiasi kwamba alikuwa anashangaa kwa nini watu walimuita (Magufuli) kuwa ni dikteta.

Mwezi Novemba 18, 2019, katika kikao baina ya viongozi wa dini na aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam wakati huo, Paul Makonda, Kadinali Pengo alidai kuwa watu wanaouzungumzia utawala wa Magufuli kuwa haujali mambo ya watu na badala yake umejikita katika kuendeleza vitu kama vile barabara, reli nk, walikuwa wakipotosha umma, alisema (zaidi): “Kumezuka maneno kwamba Rais wetu ni dikteta… yale anayoyafanya (Magufuli) anashughulikia kuendeleza vitu kuliko kuendeleza watu.” (Mwananchi 18/11/2019)

Ni jambo la kushangaza kwamba, wakati viongozi wa Kikristo wanakosoa makubaliano kati ya Dubai na Tanzania kuwa ni makubaliano yasiyo ya haki na yasiyo na ukomo wa muda, lakini wamekuwa kimya kwa miaka mingi juu ya makubaliano kati ya serikali na taasisi za kidini za Kikristo. Katika Mkataba huu mahususi wa Maelewano (memorandum of understanding) uliofanyika tangu mwaka 1992 kati ya serikali na Kanisa una upendeleo kwa Wakristo na taasisi zao ambapo serikali inatumia fedha za umma kusaidia vituo vya afya vya kanisa jambo ambalo hawakufanyiwa Waislamu. Waislamu wanafahamu kuwa serikali inatumikia maslahi ya Wakristo kwa gharama ya Waislamu na wananchi wengine.

Licha ya ukweli kwamba makubaliano kati ya Tanzania na kampuni ya kimataifa ya DP World si ya haki kwa vile yapo juu ya misingi ya kibepari, viongozi wa Kanisa hawana haki ya kimaadili ya kukosoa, kwa kuwa hawapo kwa ajili ya maslahi ya watu, kwa kuunga kwao mkono makubaliano ya kinyonyaji na ya kibaguzi yaliyopo kati yao na serikali. Mkataba wa Maelewano (MoU) kati ya serikali na Kanisa unapendelea kundi moja katika jamii (Wakristo) kati ya makundi mawili makuu ya kidini nchini (Waislamu na Wakristo) ikifahamika kwamba Waislamu huenda ndio wengi zaidi katika wakaazi.

Zaidi ya hayo, inajulikana kwa hakika kwamba Ukristo ni dini ya kiroho tu isiyo na masuluhisho ya mambo ya kidunia, hivyo wafuasi wake daima hutoa ufumbuzi na masuluhisho ya kimaslahi ya kibepari kwa vile dini yao haina mfumo wa kisiasa au wa kiuchumi.

Kuhusiana na baadhi ya viongozi wa Kiislamu wanaopendekeza na kuunga mkono mkataba wa ubinafsishaji wa bandari kwa kampuni ya DP World, wamejitokeza tu kupinga kihamasa ikiwa ni kukabili uchochezi unaofanywa na viongozi wa Kikristo bila kutoa suluhisho la kimfumo la Kiislamu kana kwamba Uislamu haujatoa ufafanuzi wala hukmu yoyote kuhusu mali/huduma za umma. Kwa kweli, walipaswa kutoa suluhisho la wazi kwa suala hili kwa mujibu wa vyanzo vya Kiislamu ambavyo vimesheheni bahari ya uchambuzi na maelezo ya kutosha juu ya sheria za bidhaa / mali / huduma za umma.

Kwa mujibu wa Uislamu, bandari ni miongoni mwa mali/bidhaa/huduma za umma ambazo ziko chini ya umiliki wa umma. Ni haki ya watu wote kunufaika na mali za umma na usimamizi wake huweza kukabidhiwa kwa Khalifah (Dola), kisha matunda yake yanarudishwa kwa Umma.

Kwa hiyo, aina zote za mali ambazo zimejumuishwa katika kundi la umiliki wa umma ikiwa ni pamoja na bandari ni haramu kwa watu binafsi kudhibiti, kunufaika na kumilikiwa kibinafsi. Hivyo, ubinafsishaji wa mali za umma ni kitendo kilichokatazwa / haramu. Mtume Muhammad (saw) amesema:

الْمُسْلِمُونَ شُرَكَاءُ فِي ثَلَاثٍ فِي الْكَلَإِ وَالْمَاءِ وَالنَّارِ

“Waislamu ni washirika (wana haki sawa) katika mambo matatu; ardhi ya malisho, maji na moto” (Abu Daawuud).

Ubinafsishaji ni sera ya kiuchumi ya kibepari ambayo husababisha na kuleta uharibifu mwingi katika nyanja ya kijamii na kiuchumi, hufanya mali kuzunguka tu kati ya matajiri, watu binafsi na kampuni. Kwa hivyo, wengi hawawezi kufaidika na mali hizi za umma, na mgawanyo wa mali unazidi kutokuwa na usawa kama tunavyoshuhudia leo hii kwamba matajiri 1% wanamiliki mali ya ulimwengu karibu theluthi mbili.

Imeandikwa kwa Ajili ya Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir na

Said Bitomwa

Mwanachama wa Afisi ya Habari ya Hizb ut Tahrir Tanzania

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

rudi juu

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu