Jumamosi, 21 Muharram 1446 | 2024/07/27
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

بسم الله الرحمن الرحيم

 Vichwa vya Habari 17/12/2021

Vichwa vya Habari:

• UAE Yasimamisha Mazungumzo na Amerika juu ya Mauzo ya kutokana na Wasiwasi wa Ubwana wa Nchi

• Amerika Yasema Misheni nchini Afghanistan Imefeli huku Pakistan Ikitoa 'Hifadhi Salama' kwa Taliban

• Putin Apongeza Muundo wa Uhusiano kati ya Urusi na China katika Maongezi ya Simu na Xi

Maelezo:

UAE Yasimamisha Mazungumzo na Amerika juu ya Mauzo ya kutokana na Wasiwasi wa Ubwana wa Nchi

UAE inasimamisha mazungumzo na serikali ya Amerika ili kupata ndege za kivita za F-35 kutokana na "vizuizi vya ubwana wa nchi", afisa mmoja wa Imarati alisema mnamo Jumanne. Akizungumza kwa sharti la kutotajwa jina, afisa huyo wa UAE alisema mazungumzo juu ya uuzaji huo, sehemu ya makubaliano ya dolari bilioni 23 ambayo pia yanajumuisha droni na mabomu mengine ya hali ya juu, yamesitishwa huku nchi hiyo ikitathmini tena mahitaji. "UAE imeifahamisha Amerika kwamba itasitisha mijadala ya kupata F-35," afisa huyo alisema. "Mahitaji ya kiufundi, vikwazo huru vya uendeshaji na uchanganuzi wa faida yamesababisha tathmini upya." Afisa huyo, hata hivyo, aliendelea kuwa na matumaini kabla ya mazungumzo ya ulinzi ya Amerika na UAE mnamo siku ya Jumatano kwamba masuala haya yanaweza kutatuliwa katika siku zijazo. "UAE na Amerika zilikuwa zikifanyia kazi maelewano ambayo yangeshughulikia masharti ya ulinzi wa pande zote kwa ajili ya ununuzi huo. Amerika inasalia kuwa mtoa huduma anayependekezwa na UAE kwa mahitaji ya juu ya ulinzi na mazungumzo ya F-35 yanaweza kufunguliwa tena katika siku zijazo," afisa huyo alisema. Suala lililosalia, mtu mmoja mwenye ufahamu wa mpango huo aliliambia The National, halihusiani na uhusiano wa UAE na China bali ni masuala ya uhuru katika makubaliano ambayo UAE imeibua na ambayo pande hizo mbili zinajaribu kutatua. Afisa mmoja wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Amerika alisema utawala wa Rais Joe Biden bado umejitolea kuuza. "Utawala wa Biden-Harris bado umejitolea kwa uuzaji uliopendekezwa wa ndege za F-35, MQ-9B [droni] na zana hata tunapoendelea na mashauriano ili kuhakikisha kuwa tunaelewana waziwazi majukumu na hatua za Imarati kabla, wakati wa kukabidhi bidhaa na baada ya kukabidhi,” afisa huyo aliambia The National. "Tuna matumaini kwamba tunaweza kutatua masuala yoyote ambayo hayajakamilika na tunatazamia Mazungumzo ya Pamoja ya Kijeshi ya Amerika na Falme za Kiarabu baadaye wiki hii." Msemaji wa Pentagon John Kirby alisisitiza hali ya kimkakati ya uhusiano wa Amerika na UAE. [Chanzo: The National]

Amerika kwa haraka iliweka vikwazo katika mauzo ya F35 baada ya kupata amani kati ya UAE na dola ya Kiyahudi. Ni vigumu kuona Amerika ikigawa teknolojia iliyoendelea kama hii ikizingatiwa ushirikiano wa karibu wa teknolojia wa UAE na China. Na hata kama mkataba utafungwa, UAE itapokea F-35 duni.

Amerika Yasema Misheni nchini Afghanistan Imefeli huku Pakistan Ikitoa 'Hifadhi Salama' kwa Taliban

Seneta wa chama cha Democrat Robert Menendez mnamo siku ya Jumanne aliishutumu Pakistan kwa kuwa na sura mbili na kusema kuwa misheni ya Amerika nchini Afghanistan ilifeli huku Islamabad ikitoa "hifadhi salama" kwa Taliban. Menendez alitoa wito wa mazungumzo mazito na serikali ya Pakistan inayoongozwa na Imran Khan juu ya njia ya kusonga mbele katika uhusiano wa pande mbili. Menendez alikaribisha uteuzi wa Blome kama Balozi mpya wa Amerika nchini Pakistan huku kukiwa na "wakati wenye changamoto" katika uhusiano baina ya Amerika na Pakistan. "Islamabad ilitoa hifadhi salama kwa Taliban licha ya kuwa wanamgambo wake waliwalenga na kuwaua wanajeshi wa Amerika. Tunahitaji kuwa na mazungumzo ya dhati na Serikali ya Pakistan katika njia yetu ya kusonga mbele," Seneta wa New Jersey Menendez, ambaye alikuwa mwenyekiti wa Kamati ya Seneti ya Mahusiano ya Kigeni ya Amerika, alisema kama alivyonukuliwa na ANI. Haswa, mvutano kati ya Washington na Islamabad umeongezeka sana. Siku za hivi karibuni baada ya Pakistan kuamua kususia 'Mkutano wa Demokrasia' ulioandaliwa na Rais wa Amerika Joe Biden. Inaaminika kuwa Pakistan ilikataa mwaliko wa Amerika wa Mkutano wa Kidemokrasia kwa shinikizo la China, ambayo haikualikwa na Washington. Zaidi ya hayo, kufuatia uchukuaji wa Taliban wa mji wa Kabul, Amerika pia ilitangaza kwamba itaangalia uhusiano wake na Pakistan katika jitihada za kuunda dori ambayo Amerika inataka Islamabad iicheze katika mustakabali wa taifa hilo lililoharibiwa na vita. Alipoulizwa kuhusu jinsi Washington inavyoona kujihusisha kwa Islamabad nchini Afghanistan, Waziri wa Mambo ya Nje wa Amerika Antony Blinken mnamo mwezi Septemba alisema kuwa Pakistan ina "maslahi mengi" yakiwemo baadhi ambayo yako katika "mgongano wa wazi" na yale ya Amerika. Blinken aliongeza kuwa ushiriki wa India katika taifa hilo lililoharibiwa na vita umeathiri baadhi ya vitendo "vibaya" vya Pakistan. [Chanzo: Republican.Com].

Ni dhahiri kwamba Amerika haifurahishwi na dori ya Pakistan nchini Afghanistan. Hii pia inaeleza ni kwa nini awamu inayofuata ya IMF inacheleweshwa, huku Amerika ikirundika shinikizo zaidi kwa Islamabad kubadili sera.

Putin Apongeza Muundo wa Uhusiano kati ya Urusi na China katika Maongezi ya Simu na Xi

Rais Vladimir Putin mnamo siku ya Jumatano alipongeza muundo wa uhusiano wa Urusi na China katika mazungumzo ya simu na kiongozi wa China Xi Jinping na kuthibitisha kuwa atahudhuria Michezo ya Olimpiki ya Beijing, huku nchi zote mbili zikikabiliwa na ukosoaji mkubwa kutoka kwa Magharibi. Maongezi hayo ya simu ya video yamejiri siku chache baada ya mawaziri wa mambo ya nje wa G7 kujadili ugomvi wa Moscow dhidi ya Ukraine na ukandamizaji wa Beijing huko Hong Kong na Xinjiang. "Mnamo Februari hatimaye tutaweza kukutana ana kwa ana mjini Beijing," Putin alisema katika matangazo ya televisheni ya taifa ya mazungumzo hayo baada ya kusema kuwa atahudhuria Michezo hiyo, akimtaja Xi "rafiki yake kipenzi". Amerika, Uingereza, Canada na Australia hazipeleki wawakilishi wa kisiasa kwenye Michezo ya Olimpiki kutokana na unyanyasaji wa China dhidi ya Uyghur na Waislamu wengine walio wachache mjini Xinjiang. Beijing na Moscow zilishutumu ususiaji wa kidiplomasia na Putin mnamo Jumatano alisema viongozi wote wawili walipinga "jaribio lolote la kuingiza siasa kwenye michezo na harakati za Olimpiki", ukosoaji ambao Urusi imekuwa ikiutoa mara kwa mara kwa nchi za Magharibi. China na Urusi zote mbili zimeona uhusiano wao na mataifa ya Magharibi ukidorora katika miaka ya hivi karibuni na wamejaribu kuweka mbele umoja zaidi. Mnamo siku ya Jumatano, Putin alimwambia Xi kwamba "muundo mpya wa ushirikiano umeundwa kati ya nchi zetu" unaojumuisha "azimio la kugeuza mpaka wetu wa pamoja kuwa ukanda wa amani ya milele na ujirani mwema". "Ninaona uhusiano huu kuwa mfano halisi wa ushirikiano kati ya serikali katika karne ya 21," kiongozi huyo wa Urusi alisema. Baada ya simu hiyo, mshauri mkuu wa sera za mambo ya nje wa Kremlin Yury Ushakov alisema kuwa mazungumzo kati ya "dola mbili kubwa za kirafiki" yalidumu kwa dakika 90 na yalikuwa "chanya mno". "Wote wawili walisema kuwa uhusiano huo ulikuwa umefikia kiwango cha juu sana," aliwaambia wanahabari. Mazungumzo hayo yamejiri baada ya Urusi na China kuachwa nje katika mkutano wa mkuu wa demokrasia wa Rais wa Amerika Joe Biden wiki iliyopita. Amerika na washirika wake kwa wiki kadhaa wameishutumu Urusi kwa kupanga kuivamia nchi jirani ya Urusi ya zamani Ukraine, na kuonya kuhusu vikwazo vikubwa vilivyoratibiwa iwapo Putin ataanzisha mashambulizi. Makumi ya maelfu ya wanajeshi wa Urusi wamewekwa karibu na Ukraine, ambapo nchi za Magharibi zimemshutumu Kremlin kwa kuunga mkono watu wanaotaka kujitenga wanaoungwa mkono na Moscow tangu 2014. [Chanzo: France24].

Amerika inakabiliwa na mtanziko mkubwa katika kuitia shinikiza Urusi na China. Badala ya kuleta mfarakano kati ya nchi hizo mbili, sera ya Amerika inazisongeza nchi hizo mbili kuwa karibu zaidi.

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

rudi juu

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu