Jumatano, 08 Shawwal 1445 | 2024/04/17
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

بسم الله الرحمن الرحيم

 Hotuba ya Tano Katika Kongamano: ‘Vijana Waislamu …Waanzilishi wa Mabadiliko Msingi’

Kukabiliana na mgogoro wa kitambulisho cha vijana wa kiislamu

Assalamu alaikum wa Rahmatullah wa Barakatahu

(1) Utangulizi:

Dada zangu wapendwa na wageni waheshimiwa, mgogoro wa utambulisho unaoathiri wengi wa vijana wetu wa Kiislamu ni mojawapo ya kadhia sugu mno zenye kuathiri Ummah huu. Na kama ulivyo mgogoro wowote, kukabiliana nao vilivyo na kwa haraka ni wajib. Ni wajib kwani ndiyo itakayoamua mafanikio ya watoto wetu na sisi wenyewe katika maisha haya na maisha ya kesho. Na ni wajib kwani ndio kitovu cha mafanikio ya mustakbali wa Ummah huu na hadhi ya Dini yetu hapa ulimwenguni.

Dada zangu, mwanachuoni mkubwa wa Kiislamu, Imam Ghazali (RH) wakati mmoja alisema, “Mtoto ni amana mikononi mwa wazazi wake. Na moyo wake msafi ni kito cha thamani kisichokuwa dosari, kisichokuwa na mchongo au umbile lolote. Hukubali kuchongwa na kufinyangwa katika mwelekeo wowote. Endapo atalelewa na kufunzwa uzuri, atakulia juu ya hili. Mtoto aina hii atafanikiwa hapa duniani na kesho Akhera na wazazi, walimu na wakufunzi wake wote watashirikiana katika malipo haya. Lakini endapo mtoto huyu atalelewa katika uovu na utepetevu, atageuka kuwa msiba na kutumbukia katika maangamivu, na wanao husika na ulezi wake watashirikiana katika dhambi lake. Endapo atakulia katika uovu na kuachwa bila ya kukanywa, atageuka kuwa msiba na ataangamia.”      

Dada zangu, kwa kweli nyoyo za watoto wetu wanapokuwa wadogo huwa ni safi, zisizo chakachuliwa, mithili ya kito cha thamani. Endapo watazamishwa ndani ya Dini kwa njia sahihi, na kuitambua Haki na kheri inayo tiririka kutokana nayo basi insha Allah watakuwa vijana ambao nyoyo zao ziko imara juu ya haki, wenye yakini na Imani zao za Kiislamu, wenye kujitolea juu ya majukumu yao ya Kiislamu, mashujaa katika kuzungumza Dini yao na dhidi ya batili na dhulma na wenye mapenzi kwa uongofu na kuchukia yale ambayo Mola wao (swt) ameyataja kuwa ufisadi, uchafu, na dhulma. Watakuwa ndio chimbuko la kheri kwa familia zao, jamii zao, mujtama zao, na Ummah huu. Na watakuwa ndio wenye kudhihirisha sifa za kuleta mageuzi ya kweli hapa ulimwenguni, wakibeba majukumu mabegani mwao na kuwezeshwa kwa suluhisho sahihi la Kiislamu la kuuinua Ummah huu na kihakika ulimwengu huu kutokana na matatizo yasiyo idadi na dhulma inayo ukabili leo.   

Lakini lengo hili tutalifikiaje? Vipi tutajenga na kuhifadhi utambulisho wa Kiislamu katika vijana wetu na kuwatayarisha kupambana na changamoto kuu wanazo zikabili katika kushikamana na Dini yao, kuzungumza Dini yao, na kung’ang’ana kwa ajili ya Dini yao?

Leo, ningependa kuzungumzia baadhi ya nukta muhimu na baadhi ya fahamu msingi ambazo zahitaji kujengwa ndani ya vijana wetu ambazo bila shaka ni muhimu mno katika kukabiliana na mgogoro huu wa utambulisho, na kuwawezesha ili kuzishinda changamoto wanazo kumbana nazo barabara insha Allah.

Lakini dada zangu, kwanza kuna swali ambalo ni lazima tulijibu wenyewe – kama wazazi, jamii, na kama Ummah – ikiwa tunataka kukabiliana barabara na mgogoro huu wa utambulisho wa vijana wetu. Nalo ni –tunataka nini haswa kwa watoto wetu? Je, tunauona Uislamu na Uislamu pekee katika nyanja zake zote – kiroho, kiakhlaqi, kijamii, na kisiasa kama njia pekee ya kuwaokoa watoto wetu kutokana na matatizo yanayo umiza roho ambayo vijana wengi wanakumbana nayo leo; njia pekee ya kuwawezesha kutoa mchango wenye natija ya kikweli kwa maendeleo ya wanadamu na hali bora ya ulimwengu huu, pamoja na kuwadhamini mafanikio msingi katika maisha haya na maisha yajayo?

• AU kuna maadili, fikra, tamaduni nyingine ambazo hazikujengwa juu ya Uislamu ambazo tunaunda kwazo mitazamo, matendo, misimamo juu ya mafanikio na matarajio yetu na ya watoto wetu ambazo zinatusababishia kulegeza msimamo kwa Dini yetu, tukisababisha mchanganyiko wa jumbe na mkanganyiko machoni mwa vijana wetu, na hata chuki akilini mwao dhidi ya Uislamu?  

• Vipi kwa mfano, tunaweza kutarajia watoto wetu kuepukana na mahusiano nje ya ndoa, ikiwa tunaruhusu tamthilia, filamu na muziki zinazo pigia debe, kuvutia na kuhamasisha kuhusu uchafu wa mahusiano hayo kuingia ndani ya sebule zetu, au ikiwa tunaruhusu mchanganyiko huru wa wanaume na wanawake katika mijumuiko yetu ya kijamii na harusi kinyume na Uislamu?

• Vipi tutaweza kujenga uhahamu (aqliyya) katika vijana wetu kuwa mafanikio makuu ni kupata Radhi za Mola wetu na kuingia mabustani ya Pepo, ikiwa tunawaruhusu kulegeza msimamo katika swala zao, vazi lao la Kiislamu na majukumu mengineyo ili wafaulu katika elimu au kutafuta ajira au kazi ya kiwango cha juu, ikiwapelekea wao kuamini kuwa kilicho muhimu ni cheo, utajiri na kupata vitu vya kidunia?

• Vipi tutaweza kuwalea vijana wetu kushikamana na matarajio ya Mwenyezi Mungu (swt), ikiwa matarajio yetu ya namna wanavyo vaa, namna ya tabia zao, nani wanaye oana, utiifu wao, mitazamo yao ya kisiasa yamejengwa juu ya maadili yasiyo ya Kiislamu, mila, utaifa, nidhamu ya kidemokrasia iliyotungwa na mwanadamu au matarajio yaliyosemwa na familia au jamii, badala ya lile analo amuru Mwenyezi Mungu (swt)?

• Na vipi tutawapa motisha vijana wetu kuwa mashujaa na kusimama kwa ajili ya Uislamu ikiwa tuna hofu ya kuwashajiisha kuzungumza kwa ajili ya Ummah wao nchini Palestina, Syria na kote ulimwenguni, au dhidi ya mashambulizi juu ya kipenzi chetu Mtume (saw) na Dini, au dhidi ya vita na madhalimu wa Kimagharibi katika ulimwengu wa Waislamu, au katika kuunga mkono Shari’ah au Nidhamu ya Mwenyezi Mungu – Khilafah – kwa kuogopa kuwa watatazamwa kama wenye misimamo mikali na kuwekwa chini ya rada za serikali dhalimu.

• Dada zangu wapendwa, endapo tutawasilisha jumbe za mkanganyiko na kuwa na misimamo miwili miwili kwa vijana wetu kupitia mitazamo, maneno na matendo yetu wenyewe, kamwe hatutaweza kukabiliana barabara na mgogoro wa utambulisho wanaokumbana nao. Hivyo basi, hatua ya kwanza ya kuwaokoa watoto wetu ni kutathmini upya utambulisho wetu wenyewe na kudumu kwetu katika kushikamana na Dini yetu.

(2) Kujenga Itikadi (Aqeedah) kwa Kukinai:

• Baada ya kuelezea nukta hii muhimu ya mwanzo, dada zangu, ni hatua gani muhimu nyenginezo ambazo twahitaji kuchukua ili kukabiliana na mgogoro wa utambulisho katika vijana wetu?

• Kwanza dada zangu, mojawapo ya zawadi za thamani mno ambazo twaweza kuwapa watoto wetu ni uwezo wao wa kutafakari wenyewe kuhusu maisha na ulimwengu, kwa njia ambayo wataweza kutofautisha haki kutokana na batili. Hii yamaanisha kwanza, kuwawezesha kujenga ukweli wa Itikadi ya Kiislamu kwa kukinai kuliko katikiwa kupitia kuwapa dalili nzito za kiakili zinazo jenga yakini ya kuwepo kwa Muumba na kwamba Qur’an ni maneno Yake kwa asilimia 100 – kama alivyo sema Mwenyezi Mungu (swt), 

[إِنَّمَا ٱلۡمُؤۡمِنُونَ ٱلَّذِينَ ءَامَنُواْ بِٱللَّهِ وَرَسُولِهِ ثُمَّ لَمۡ يَرۡتَابُو]

“Hakika Waumini ni wale walio muamini Mwenyezi Mungu na Mtume wake tena wasitie shaka kabisa...” [Al-Hujraat: 15].

• Katika ulimwengu wa leo dada zangu, ambamo vijana wetu wanashambuliwa kwa hotuba katika vyombo vya habari au mitandaoni za kuupinga Uislamu, kushambulia Imani zake, kujenga hofu katika utekelezaji Uislamu, na lile dai kuwa Imani kwa Mungu na dini haingii akilini, iliyopitwa na wakati, ni ya watu wenye akili finyo pekee – kujenga Aqeedah ya Kiislamu kwa kukinai kiakili kuliko katikiwa ni nyeti mno. Ni hili ndilo litakalo badilisha Uislamu kutoka kuwa ni kitu ambacho vijana wengi wanakitazama kama walicho rithi tu kutoka kwa wazazi wao, hadi kuwa ni kitu walicho kikinai kiakili kuwa na majibu sahihi ya maisha na hivyo kinapaswa kupangilia fikra na matendo yao.    

• Ni yakini hii katika Imani ndiyo itakayo fanya Pepo (Jannah) na Moto (Jahannam) kuwa uhalisia usio badilika machoni mwa vijana wetu inshaAllah, na kuhisabiwa na Mwenyezi Mungu kuwa ni fahamu nzito akilini mwao, ikiwapelekea kuishi maisha yao kwa mujibu wa Sheria na Mipaka yake (swt) inshaAllah. NA ni yakini hii katika Imani ambayo pia itajenga ufahamu safi inshaAllah kuwa lengo maishani na mtazamo sahihi wa mafanikio sio kutafuta vyeo vikubwa na starehe fupi za maisha haya, au kukubaliwa na kupata umaarufu miongoni mwa marafiki na mujtama bali ni kupata Radhi za Mwenyezi Mungu (swt) na thawabu zisizo kifani kesho Akhera.

• Hakika dada zangu, katika ulimwengu ulio pagawa na matumizi ya kimada unaojaribu kuwaundia vijana wetu Pepo duniani kwa matamanio na starehe nyingi za kuvutia zinazo kwenda kinyume na Dini yao, au ambapo utafutaji wa mali za dunia hii – simu, kifaa, ala, nguo za kisasa – zimetawala wakati na umakinifu wao – ni muhimu mno tujenge ndani ya vijana wetu hamu ya Pepo inayo wanyanyua juu ya starere fupi za dunia hii na kuwawezesha kuzikubali hukmu za Kiislamu zilizo wekwa juu ya maisha yao – kupitia kudumu kuwakumbusha kuwa zote hizi si chochote isipokuwa ni tone ndani ya bahari ikilinganishwa na starehe zisizo kifani zinazomsubiri kijana mwema Peponi – kama Mtume (saw) alivyosema,

«وَاللَّهِ مَا الدُّنْيَا فِي الآخِرَةِ إِلاَّ مِثْلُ مَا يَجْعَلُ أَحَدُكُمْ إِصْبَعَهُ هَذِهِ - وَأَشَارَ يَحْيَى بِالسَّبَّابَةِ - فِي الْيَمِّ فَلْيَنْظُرْ بِمَ يَرْجِعُ»

“Naapa kwa Mwenyezi Mungu, haikuwa dunia kwa Akhera isipokuwa ni mithili ya mmoja wenu kutia kidole chake hiki – na akaashiria kwa kidole cha shahada – ndani ya bahari kisha aangalie atakacho baki nacho kidoleni hicho.”

• Dada zangu wapendwa, ni kukinai huku katika Aqeedah na kuwa na hamu ya Pepo ndio yaliyo mpelekea kijana mchungaji dhaifu Abdullah ibn Masud (ra) kuwasomea Qur’an Maquraysh, akijua kwamba watampiga; ndiko kuliko mpelekea kijana Jafar ibn Abi Twalib (ra) kuzungumza kwa niaba ya Waislamu katika mahakama ya Mfalme wa Habasha, bila ya kutishwa na uwepo wa watu walio na ufasaha zaidi katika Maquraysh walio tumwa kuzungumza dhidi ya waumini. Na dada zangu, ni kukinai huku ndiko ambako inshaAllah kutawajaza vijana wetu ushujaa wa kushikamana na Imani zao za Kiislamu katika hali yoyote ile; kusimama dhidi ya shinikizo la wandani wao, hawahofii kubandikwa majina au kuwa tofauti na marafiki zao au hata kubaguliwa kutokana na vazi lao, matendo yao au rai zao za Kiislamu, na kuzungumza kwa ajili ya Uislamu pindi unapo shambuliwa.

 (3) Kuvunja Kivutio cha Mfumo Huru wa Kisekula wa Kimaisha:

• Hatua ya pili ya kukabiliana na mgogoro huu wa utambulisho katika vijana wetu, dada zangu, ni kujenga njia ya kutafakari kwa kudadisi ndani yao inayo wawezesha kutenganisha uongo kutokana na ukweli kuhusiana na fikra zilizo tawala na simulizi zinazo washambulia kutoka katika vyombo vya habari au mujtama na kupambana nazo kwa hekima. Kuwawezesha kupuuzilia mbali uongo dhidi ya Uislamu na kuvunja kivutio cha mfumo huru wa kisekula wa kimaisha ni muhimu mno katika wakati ambao vijana wetu wanafanywa wahisi kuwa Uislamu ndio chanzo cha matatizo yao mengi na ghasia duniani, na kwamba mfumo huru wa kimaisha wa Kimagharibi ndio njia ya furaha na mafanikio, na ustawi na ufanisi katika hii dunia.

• Twahitaji kuwaonyesha – kuwa Uislamu sio uliosababisha janga la mihadarati, ulevi, usumbufu, magenge, uhalifu wa bunduki na tabia nyingine za kiuhalifu zilizo waathiri vijana leo bali ni maadili huria yanayo pigia debe muondoko wa kimaisha wa starehe za kibinafsi na kufuata matamanio ya mtu bila ya kujali matokeo. Uislamu sio uliovunja haiba na Imani ya wasichana wengi wadogo kwa sababu hawawezi kujilinganisha na muonekano wa wasanii na viigizo wengine bali ni muundo wa urembo wa Kimagharibi usio wa kihakika ambao umenasibishwa na mafanikio. Uislamu sio unao wafanya vijana wengi kuhisi kufeli au kuchukuliwa kama walio laaniwa wanapo shindwa kudumu katika fesheni za simu au bidhaa bali ni thaqafa ya kimada ya kirasilimali inayo sawazisha thamani ya mtu binafsi na mali za kidunia. Sheria za kijamii za Kiislamu sizo zilizo unda mila ya utovu wa heshima kwa wasichana na wanawake, ikipelekea ghasia na dhulma za kijinsia bali ni mujtama zinazo tukuza uhuru wa kijinsia na kuruhusu hadhi ya wanawake kudunishwa kupitia kuwafanya kuwa vyombo vya ngono katika sekta ya burudani na unadi bidhaa. Na Uislamu sio ulio zalisha umasikini mkubwa na ukosefu wa ajira, ukosefu wa usawa katika utajiri, na huduma duni za elimu na matibabu kote duniani bali ni nidhamu ya sumu ya kirasilimali ndiyo iliyo sambaratisha uchumi, kuzizonga na madeni makubwa yenye riba, na kuwapendelea matajiri kuliko masikini.

• Sambamba na haya dada zangu, pia tunahitaji vijana wetu wafahamu na kuunganisha kwa hekima na dalili kwa wale wanao wazunguka, kuwa sio sura ya kimakosa ya mfumo wa Kiislamu inayo chochea ugaidi bali ni hasira zilizo chochewa na uingiliaji mambo wa Kimagharibi na vita vya kikoloni katika ulimwengu wa Waislamu ambavyo vimeuwa maelfu ya Waislamu. Tunahitaji wao wajadili kwa uwazi kuwa ni Imani hizo hizo za Kiislamu ndizo zinazo wasukuma kutekeleza Uislamu ambazo pia zinawawajibisha kuwaheshimu wazazi na walimu, kuamiliana na wanawake kwa hadhi, kuepuka uhalifu, kutia juhudi kwa ajili ya manufaa ya wanadamu na kupinga ghasia dhidi ya wasiokuwa na hatia au kuwanyanyasa walio katika dini nyingine. Na twahitaji vijana wetu kufahamu na kusema kwa imani kuwa si katika misimamo mikali kuzungumzia kuhusu dhulma za serikali au kuzungumza kwa niaba ya wanyonge, au kulingania Shari’ah ya Kiislamu au Khilafah kutabikishwa katika ardhi zetu ambayo itabadilisha udikteta kwa uangalizi kwa watu, kuzibadilisha dola za kiaskari kwa uwajibikaji na uadilifu katika usimamizi, na ambayo itatumia utajiri wa ardhi zetu kwa ajili ya mahitaji ya watu kuliko kujaza mifuko ya serikali za kigeni, mashirika malafi au kwa kipote cha mabwenyenye wachache.   

• Dada zangu, tunahitaji kuwafanya watoto wetu kuchukua umiliki wa midahalo hii na kutawala simulizi kuhusiana na Uislamu na mifumo mingine ya kimaisha ndani ya mujtama zao, wakijihami kwa ukweli.

 (4) Kuufahamu Uislamu kama Dini Iliyo na Suluhisho la Matatizo ya Kimaisha na Kujenga Fahari Katika Thaqafa na Historia ya Kiislamu:

• Na mwisho dada zangu, katika ulimwengu ambao Uislamu unaonyeshwa kama uliopitwa na wakati, katili, na wenye kukandamiza wanawake na dini nyingine, na kitu cha kihistoria kisicho endana na maisha ya kisasa, ni muhimu mno tuwajenge vijana wetu kuwa na imani katika Dini yao na kuitazama kama inayo endana na maisha yao na ulimwengu huu wa karne hii ya 21, kuliko kuwa ni mkusanyiko tu wa ibada na hukmu. Hili twaweza kulipata pekee kupitia kuwafanya waufahamu Uislamu kama Dini kamilifu iliyo na misingi, sheria na suluhisho kwa matatizo ya kileo ya kimaisha – kiroho, kiakhlaqi, kijamii, kisiasa, kimahakama, kielimu, katika uchumi, na yasiyokuwa haya – kwani Mwenyezi Mungu (swt) asema, [مَّا فَرَّطۡنَا فِى ٱلۡكِتَـٰبِ مِن شَىۡءٍ] “Hatukupuuza Kitabuni kitu chochote...” [Al-Anaam: 38]

Na kwa hili, pia kujenga fahari katika thaqafa na historia ya Kiislamu na yale iliyoleta kwa wanadamu na yale iliyo faulu katika dunia hii ya uadilifu, ufanisi, ustawi, maendeleo ya kisayansi, ubinadamu, kulinda haki za wanawake na dini za wachache, mafanikio ya kiusomi, na nidhamu za elimu na matibabu za kiwango cha juu wakati wa zama za utawala wake juu ya ardhi zetu za Waislamu, chini ya kivuli cha Khilafah tukufu.

• Waonyesheni kuwa ni sheria za nidhamu ya kiuchumi ya Kiislamu ndizo zinazo shikilia ufunguo wa ugavi sawa wa utajiri na uundaji wa uchumi ulio nawiri – kama ilivyo onyeshwa kupitia Khilafah ya Umar bin Abdul Aziz aliye arifiwa na afisa wake nchini Iraq kuwa hata baada ya pesa za dola kutumika kukidhi haja za watu, kulipa madeni yao, kuwasaidia kifedha katika ndoa zao, bado kulisalia pesa katika hazina. Umar kisha akamuagiza kuitumia ziada hii kuwasaidia watu kulima ardhi zao. Subhanallah!

• Twahitaji kuwaonyesha vijana wetu kuwa ni Dini ya Kiislamu pekee ndiyo inayo pinga uhuru wa kijinsia, kuharamisha udhalilishaji na uchukuaji wa wanawake kuwa vyombo vya ngono, na kuasisi mpangilio mpana wa sheria ili kudhibiti mahusiano kati ya wanaume na wanawake ili kuhifadhi hadhi yao, ambayo yaweza kutatua janga la ghasia na unyanyasaji wa kijinsia wa wanawake unao athiri ulimwengu leo.

• Na, twahitaji kuwaonyesha watoto wetu kuwa ni nidhamu ya Kiislamu pekee inayopinga taasubi ya kimada na ya kikabilia katika kushughulikia matatizo ya wanadamu na ambayo inatumikia kwa ikhlasi mahitaji ya wanadamu ndio inayoweza kutatua mgogoro wa wakimbizi – kama ilivyo dhihirishwa kwa vitendo vya Khilafah Uthmaniyya mnamo 1492, pindi Khalifah Bayezid wa pili alipotuma msafara wake wote wa majeshi kwenda kuwaokoa Mayahudi 150,000 wa Ulaya waliokuwa wakiteswa na Wakristo wakati wa Uchunguzi wa Kihispania na kuwakaribisha katika ardhi za Khilafah na kuamiliana nao kwa usawa kama raia, na kuwaruhusu kujiimarisha. 

• Dada zangu, ni kwa kujenga fahari hii katika thaqafa na historia ya Kiislamu ndani ya vijana wetu, na kuufahamu Uislamu kama Dini pana iliyo na suluhisho kwa matatizo yote ya wanadamu katika zama zote na mahali popote ndio itakayo wawezesha kupambana na mashambulizi dhidi ya Dini yao, kupinga ajenda ya Kimagharibi ya kuupa sura mpya Uislamu, kukuza ndani yao imani katika utambulisho wao wa Kiislamu, na kuwawezesha kuzungumza kwa ajili ya Uislamu kwa hekima na kauli thabiti.

• Lakini fauka ya hayo, dada zangu, ni katika kutambua maumbile halisi ya Uislamu ndiyo yatakayo jenga ndani ya vijana wetu hisia kubwa ya majukumu mbele ya Ummah huu na hakika mbele ya wanadamu baada ya kutambua nguvu kubwa iliyopo mikononi mwao ya kuleta mabadiliko halisi katika ulimwengu huu kupitia Dini hii, ikiwapatia sababu stahiki ya kung’ang’ania ambayo kihakika yaweza kujenga mustakbali bora wa ardhi zao na ulimwengu huu, ikiwemo kudhamini matarajio yao ya kielimu na kiuchumi; sababu ambayo haitapoteza nguvu zao, kusaliti matumaini yao, na kuzima ari yao, wala si sababu ambayo itawahusisha katika ghasia tasa kama njia ya mabadiliko ya kisiasa bali vita vya kifikra ili kusimamisha Dini hii katika utawala, kwa kufuata Sunnah ya Mtume (saw).

• Dada zangu wapendwa, yote haya ndio yatakayo wajenga vijana wetu wa Kiislamu kuwa “Waanzilishi wa mabadiliko halisi”, wakiwezeshwa kwa Uislamu, ukiunganishwa na hamu na nguvu nyingi ambazo vijana wetu wanazo katika kuleta tofauti halisi hapa ulimwenguni lakini kwa njia inayo wapatia Radhi za Mola wao na kuwadhamini malipo makubwa kesho Akhera. Na ni kupitia kuwalea vijana wetu kusimama kwa changamoto hii kuu ndio pia inshaAllah itarahisisha kurudi kwa haraka kwa dola ya Khilafah Rashida kwa njia ya Utume, ambayo dada zangu ndio uongozi utakao hudumikia kama mlinzi wa kweli wa utambulisho wa Kiislamu wa watoto wetu – dola itakayo wazamisha ndani ya maadili matukufu ya Kiislamu na kuzalisha mazingira ambayo daima yatawakumbusha kuhisabiwa kwao na Mwenyezi Mungu na umuhimu wa kujitolea kwa ajili ya Akhera, dola ambayo vyombo vyake vya habari na nidhamu yake ya elimu zitakuza maadili na matendo mema, kukuza uchaMungu (Taqwa) wa vijana wetu na mapenzi yao kwa Dini yao. Itaunda vijana wengi walio na utambulisho wa kipekee wa Kiislamu watakao dhihirisha tabia  zao tukufu na waja wa Mwenyezi Mungu wenye kujitolea, kubeba mizigo ya Ummah wao mabegani mwao, wapinzani wakali wa dhulma, na wenye kuwakilisha sifa za viongozi wa wanadamu. 

• Dada zangu, vita vya kulinda utambulisho wa Kiislamu wa kizazi chetu kijacho kamwe havitashindwa pasina kusimamishwa kwa haraka nidhamu hii – Khilafah kwa njia ya Utume. Kwa hivyo kuongezea juu ya ujenzi wa fahamu za Kiislamu ndani ya vijana wetu leo, pia vile vile tutulize makini yetu na kutia juhudi zetu katika kuregesha dola hii tukufu katika ardhi zetu na kupitia kwayo kuunda kizazi cha vijana ambacho ndicho chanzo cha fahari kwa Ummah huu na ambao wanasimama kama mfano na chanzo cha matarajio kwa vijana wa ulimwengu huu.

Mwenyezi Mungu (swt) asema, [وَرِضۡوَٲنٌ۬ مِّنَ ٱللَّهِ أَڪۡبَرُ ذَٲلِكَ هُوَ ٱلۡفَوۡزُ ٱلۡعَظِيمُ] “...na Radhi za Mwenyezi Mungu ndio kubwa kuliko yote. Huko ndiko kufuzu kukubwa.” [At-Taubah: 72]

Imeandikwa na
Dkt. Nazreen Nawaz
Mkurugenzi wa Kitengo cha Wanawake Katika Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir

Imebadilishwa mara ya mwisho mnamoJumapili, 12 Aprili 2020 07:31

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

rudi juu

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu